Saturday, October 5, 2013

MWAMBUNGU ALIAGIZA JESHI LA POLISI MKOANI RUVUMA KUWACHUKULIA HATUA MADEREVA WAZEMBE

Kamanda wa Polisi mkoani Ruvuma, Deusdedith Nsimeki.


























Na Muhidin Amri,
Songea.


JESHI la polisi mkoani Ruvuma, limeagizwa kuwachukulia hatua madereva wazembe wanaosababisha vifo vya watu wasiokuwa na hatia kunakotokana na matumizi mabaya ya barabara, kwa kuendesha vyombo vya moto huku wakiwa wanaongea na simu au kusikiliza muziki wawapo barabarani.


Hatua hiyo ya serikali inatokana na ongezeko kubwa la ajali za barabarani mara kwa mara, kunakosababishwa na madereva wazembe wasiozingatia sheria kwa kuongea na simu au kwa kusikiliza muziki kwa kuweka vifaa masikioni, hali inayomfanya dereva kukosa umakini katika matumizi ya barabara na chombo anachokiendesha.


Agizo hilo limetolewa juzi mjini Songea na Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu alipokuwa akifunga kozi  fupi za udereva, ufugaji bora wa kuku na urembo katika chuo cha VETA Songea, ambapo kozi hizo ni mara ya kwanza kutolewa katika vyuo vinavyomilikiwa na mamlaka  stadi ya  elimu na ufundi stadi(VETA) nyanda za juu inayojumuisha mikoa ya Iringa, Njombe na Ruvuma.


“Polisi kuweni wakali kwa madereva wazembe, nataka kuona mkoa wa Ruvuma tunapunguza ajali kwa kiasi kikubwa hawa madereva wanaoendesha na kusikiliza simu siwahitaji katika mkoa wangu,  kwani wanasababisha kupungua kwa nguvu kazi ya taifa hili”, alisema Mwambungu.


Kadhalika amewataka madereva kuwa makini na matumizi ya barabara na kuomba kuwajali na kuwathamini wenzao wanaotumia barabara hizo hususani waenda kwa miguu.


Aidha amewahakikishia kwamba wafugaji wa kuku mkoani Ruvuma kwamba kuna soko kubwa la kitoweo hicho, lakini tatizo kubwa ni kwa wafugaji wenyewe ambao  hawako makini na wanashindwa kuzingatia kanuni za ufugaji bora ili waweze kuzalisha kuku hao kwa wingi.


Pamoja na mambo mengine akizungumzia kozi ya urembo Mwambungu aliipongeza VETA kwa ubunifu wa kuibua kozi hiyo, ambayo itasaidia  kuongeza ajira kwa wasichana na wavulana wa mkoa wa Ruvuma.


No comments: