Friday, October 11, 2013

SAKATA LA MAANDAMANO MGODI WA MAKAA YA MAWE, WATU SABA WAPANDISHWA KIZIMBANI

Washtakiwa ambao wanatuhumiwa kufanya maandamano haramu, wakiwa katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wakisubiri kusomewa mashtaka yao.  (Picha na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

WATU saba wakazi wa kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani humo kwa tuhuma ya kufanya maandamano haramu, kuziba barabara na kuharibu mali.

Katika mahakama hiyo mwendesha mashtaka msaidizi wa polisi Inspekta Nassibu Sued Kassim, alidai mbele ya Hakimu Joackimu Mwakyolo kuwa tukio hilo lilitokea Oktoba 10 mwaka huu majira ya saa 2 asubuhi.

Inspekta Kassim alidai mahakamani hapo kuwa watuhumiwa hao vilevile walishambulia kibanda cha walinzi wa kampuni ya Tancoal Energy, ambayo inafanya shughuli za uchimbaji wa makaa ya mawe kijijini hapo na kusababisha hasara ya shilingi milioni 2.

Aliwataja washtakiwa hao kuwa ni Siprian Mhagama, Jackson Nkwera, Ambrose Mhagama, George Nkondora, Theodos Komba, Angelus Mgaya na Martin Mapunda.

Kesi hiyo itakuja kutajwa tena Oktoba 24 mwaka huu na washtakiwa wamenyimwa dhamana baada ya Mwendesha mashtaka huyo kuiomba mahakama kuwa endapo watapatiwa dhamana, watuhumiwa hao wanaweza kuvuruga ushahidi kutokana na shauri hilo bado linaendelea kwa uchunguzi na baadhi ya watuhumiwa wengine bado wanatafutwa na jeshi la polisi kutokana na kutokomea kusikojulikana.

No comments: