Wednesday, October 2, 2013

SOPHIA SIMBA AKEMEA UNYANYASAJI WA WATOTO, AWATAKA PIA AKINA MAMA WA UWT KUJISHUGHULISHA NA KILIMO, BIASHARA NA KUJIUNGA KATIKA VIKUNDI

Kutoka kulia Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Sophia Simba akizungumza na Wanachama wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma (Hawapo pichani) wakati alipokuwa katika ziara yake ya siku mbili wilayani humo. Katikati ni Mwenyekiti wa CCM wilayani humo Christantus Mbunda na wa mwisho kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Ruvuma Kuruthum Mhagama.

Sophia Simba akifurahi baada ya kushika mbogamboga, wakati alipokuwa akikagua shughuli za ujasiriamali zinazofanywa na akina mama wa UWT wilayani Mbinga.

Sophia Simba akipokea maelezo juu ya namna ya utengenezaji wa sabuni za kufulia nguo na kuoshea vyombo, ambazo hutengenezwa na kundi la akina mama wajasiriamali kutoka UWT wilayani Mbinga.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto(Upande wa kulia) Sophia Simba, akipokea pia maelezo juu ya utengenezaji kinywaji aina ya 'Matengo Wine' ambacho huzalishwa na akina mama hao wa UWT wilayani humo. (Picha zote na Gwiji la Matukio mkoani Ruvuma)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
WANAWAKE wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wametakiwa kuwa makini katika kuendesha maisha yao kwa kujishughulisha na kilimo, biashara na kujiunga na vyama vya akiba na mikopo ili waweze kuepukana na kujiingiza kwenye anasa ambazo zinachangia maambukizi ya virusi vya ukimwi.
 
Sambamba na hilo wameshauriwa kushirikiana na kuchukua hatua katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku kwa kufanya kazi kwa bidii.

Rai hiyo ilitolewa na Waziri wa Maendeleo ya jamii, Jinsia na watoto Sophia Simba wakati alipokuwa akizungumza leo na Wanachama wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kwenye uwanja wa ofisi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) mjini hapa.

Simba yupo katika ziara yake ya siku mbili wilayani Mbinga, kwa lengo la kuwatembelea wanawake wa Umoja huo na kukagua shughuli mbalimbali za ujasiriamali, ambazo huendeshwa na akina mama hao wilayani humo.

“Ndugu zangu sasa ni wakati wa kujituma na kufanya kazi kwa bidii,   wanawake wengi tumekuwa tukijiingiza kwenye anasa kutokana na kutokuwa na ajira kama njia ya kujipatia kipato, yatupasa tubadilike tuachane na mambo haya”, alisema Simba.
 
Alisema huu ni wakati wa wanawake kujikwamua kiuchumi kwa kujiunga kwenye SACCOS ambazo zitawasaidia kuwajengea uwezo kwa kupata mikopo ya kuanzisha na kuimarisha miradi yao.
 
Aidha alieleza kuwa wanawake wanapaswa kujiendeleza kielimu na kwamba huu ni wakati wa kupambana na maisha badala ya kushindana kwa mambo yasiyo ya msingi.


Waziri huyo pia alikemea kitendo cha akina mama kuwapiga na kunyanyasa watoto wadogo, na kuwataka vitendo hivyo kuachana navyo.

“Naomba mjue haki ya mtoto anapaswa kulindwa na sio kunyanyaswa, nahitaji tuwe karibu sana na watoto wetu kwa kuwapatia malezi bora na sio kuwapiga”, alisisitiza.
 
Hata hivyo aliwataka wanawake kutambua kuwa wao ni kiungo muhimu katika jamii hivyo ni vyema serikali, ikawawekea vipaumbele mbalimbali ili waweze kujikwamua kimaisha kwa kuwa asilimia kubwa wao ndio walezi wa familia.

No comments: