Monday, April 7, 2014

CCM MBINGA YAPONGEZA JITIHADA ZA UDHIBITI UTOROSHWAJI ZAO LA KAHAWA, YATOA MSIMAMO WA SERIKALI MBILI KATIBA IJAYO

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Juma Mpeli.

















Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

SERIKALI wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, imepongezwa kwa jitihada zake za kudhibiti biashara haramu ya magendo ya kahawa iliyokuwa ikifanyika wilayani humo na wafanyabiashara wajanja, na kuwasababishia wakulima wa zao hilo washindwe kusonga mbele kimaendeleo.

Juu ya udhibiti huo, imeelezwa kuwa hivi sasa wakulima wataweza kuuza kahawa yao kwa bei nzuri na kuwafanya waweze kuwa na kipato na hata wilaya, kuweza kukusanya mapato yake kwa urahisi.

Hayo yalisemwa na Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga mkoani humo, Juma Mpeli alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Alisema Halmashauri kuu ya chama hicho hapa wilayani, imepokea taarifa kutoka kwa uongozi wa wilaya ya Mbinga juu ya mipango waliyonayo ya kilimo cha zao la kahawa, na kuunga mkono jitihada hizo ambazo zinaendelea kufanywa ikiwemo suala hilo la kudhibiti utoroshwaji wa zao la kahawa.


Mpeli alifafanua kuwa CCM hivi sasa imejiwekea mikakati ya kupita katika kila kata kuhamasisha wakulima, kuuza kahawa yao kwenye vyama vya ushirika na kazi hiyo itaanza kufanyika mapema mwanzoni mwa mwezi Mei mwaka huu.

“Sisi kama chama cha mapinduzi tunaipongeza sana serikali yetu hapa wilayani, kwa hatua hizi walizozichukua katika kudhibiti tatizo hili sugu ambalo lilikuwa linafanywa na wafanyabiashara ambao hawa watakii mema wakulima wetu”, alisema.

Pia aliwataka wakulima kuacha biashara ya kahawa mbichi ambayo huuzwa kwa njia ya magendo, huku akisisitiza ukoboaji ufanywe katika mitambo ili waweze kupata kahawa iliyokuwa bora na yenye bei nzuri mnadani.

Kadhalika aliongeza kuwa hivi sasa katika msimu wa mavuno ya zao hilo uonjaji wa kahawa utafanyika hapa Mbinga, badala ya Moshi na zao hilo kibiashara kuitwa X – Mbinga tofauti na miaka ya nyuma lilikuwa likiitwa X – Makambako kutokana na kuhifadhiwa katika maghala ya Makambo mkoani Iringa, ambako hata uzalishaji wa kahawa haupo.  

Pamoja na mambo mengine akizungumzia msimamo wa chama hicho, Mpeli aliwaeleza waandishi wa habari kuwa hivi sasa wamekuwa na mambo matatu ambayo chama kinasimamia hapa wilayani Mbinga ambayo ni msimamo juu ya muundo wa katiba, uchaguzi wa serikali za mitaa ambao unatarajiwa kufanyika hivi karibuni pamoja na sherehe za kuzaliwa kwa chama hicho ambazo zitafanyika kitaifa mwakani hapa mkoani Ruvuma.

Katibu huyo alisema msimamo wao ni kuwa na serikali mbili na kufafanua kuwa, hata katika kuzihudumia ni rahisi tofauti na kuwa na serikali tatu ambayo aliita ni tegemezi na itakuwa mzigo kwa taifa.

Hata hivyo alitoa wito kwa wanachama wa chama hicho watulie, wasikilize na kufuata misimamo ya chama huku akiongeza juu ya suala la uchaguzi wa serikali za mitaa nalo wazingatie matakwa ya chama kwa faida ya Watanzania wote.

No comments: