Tuesday, April 29, 2014

BARAZA LA MADIWANI MBINGA LAMTIMUA OFISA ELIMU SEKONDARI, LASEMA LIMEZINGATIA TAMKO LA WAZIRI

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa.

Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

HATIMAYE Baraza la Madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, limemaliza mzizi wa fitina kwa kumkataa aliyekuwa Ofisa elimu wa wilaya hiyo Hanji Yusuph Godigodi na kusema kuwa hawataki kumuona ndani ya wilaya hiyo, akiendelea kufanya kazi za utumishi wa umma.

Kukataliwa kwa Ofisa huyo kumefuatia baraza hilo kuketi kama kamati kwa muda wa nusu saa kujadili suala hilo, likizingatia tamko lililotolewa na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa, Februari 7 mwaka huu wakati alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo.

Jukumu la kuketi kama kamati lilifuatia kuwepo kwa mchezo mchafu ambao ulikuwa ukisukwa chini kwa chini na baadhi ya vigogo wa ngazi ya mkoa huo na wilaya, kwa lengo la kutaka kumrejesha madarakani Ofisa huyo ili aendelee na kazi yake kama kawaida.

Majaliwa alitoa tamko la kumvua madaraka kwa kumshusha cheo Ofisa huyo wa elimu sekondari wilayani humo, na wenzake sita ambao ni walimu wakuu wa shule za sekondari, kufuatia kushindwa kutekeleza majukumu yao ya kazi na kufanya ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 268 za maendeleo ya elimu ya sekondari.


Sambamba na hilo aidha mtumishi mmoja wa Mamlaka ya mji mdogo wa Mbinga ambaye ni Prosper Luambano naye amekataliwa na baraza hilo kutokana na kutotekeleza majukumu yake ya kazi ipasavyo, na kumtaka Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga kuchukua hatua mara moja, ya kumhamisha kumpeleka kituo kingine cha kazi nje ya wilaya hiyo.

Maamuzi hayo ya kuwakataa Watumishi hao yametolewa leo na Mwenyekiti wa Baraza la madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga Allanus Ngahy, katika kikao cha baraza hilo kilichoketi kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa.

Wakuu wa shule za sekondari wilayani Mbinga ambao nao walivuliwa madaraka na Waziri Majaliwa na kushushwa vyeo vyao ni William Hyera ambaye ni wa shule ya sekondari Maguu, Clemence Sangana anatoka shule ya sekondari Mkuwani, Method Komba Langilo sekondari, John Tillia Ukilo sekondari, Leonard Juma Luli Sekondari huku akimtaja kwa jina moja mwalimu Konga ambaye yupo sekondari ya Kihangimahuka.

Kwa mujibu wa tamko hilo ambalo lilitolewa na Waziri huyo aliagiza kuwa Ofisa elimu wa sekondari wa wilaya hiyo Hanji Yusuph Godigodi na Wakuu wa shule hizo, anawavua madaraka waliyonayo kwa kuwashusha cheo na kwenda kuwa walimu wa kawaida wakafundishe (Wakashike chaki) darasani ili iwe fundisho kwa watumishi wengine ambao wenye utovu wa nidhamu, na ambao hawataki kuzingatia maadili ya utumishi umma.

Kufuatia rungu hilo ambalo limewaangukia watumishi hao, katika nafasi ya Ofisa elimu sekondari wilaya ya Mbinga hivi sasa inashikiliwa na Lucy Mwalukyosa ambaye atakuwa kaimu Ofisa elimu sekondari wa wilaya hiyo, na kwa upande wa shule za sekondari walimu ambao walikuwa wasaidizi ndio watakao kuwa Wakuu wa shule hizo kama ilivyoagizwa na Naibu Waziri wa TAMISEMI alipokuwa ziarani hivi karibuni wilayani Mbinga.


No comments: