Monday, April 7, 2014

UMOJA WA WAZAZI MBINGA WAITAKA JAMII KUTILIA MKAZO SUALA LA ELIMU NA UPANDAJI MITI KATIKA VYANZO VYA MAJI


Aliyevaa shati la kijani ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbinga mkoa wa Ruvuma, akiwa ameongozana na viongozi wenzake wa chama, wakiangalia mchezo wa ngoma ya asili iitwayo Mhambo katika maadhimisho ya sherehe za umoja wa Wazazi zilizofanyika hapa wilayani kijiji cha Mundeki kata ya Myangayanga wilayani humo. (Picha zote na Gwiji la matukio Ruvuma)
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

UMOJA wa Wazazi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, umewataka wananchi wa wilaya hiyo kutunza na kuendeleza mazingira kwa maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Aidha imesisitizwa kuwa katika kufanikisha hilo, viongozi wa serikali waliopo katika maeneo mbalimbali katika vijiji na kata wahakikishe kwamba wanahamasisha watu kupanda miti iliyo rafiki ya maji, katika vyanzo vya maji na vilele vya milima.

Rai hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa wilaya ya Mbinga, Christantus Mbunda alipokuwa mgeni rasmi akihutubia katika maadhimisho ya sherehe za umoja huo yaliyofanyika katika kijiji cha Mundeki kata ya Myangayanga wilayani humo.

Mbunda alisisitiza pia watu waache tabia ya kukata miti ovyo na kuagiza Watendaji wa vijiji na kata kusimamia sheria za utunzaji mazingira, kwa kuwaelimisha wananchi na kuchukua hatua pale wanapoona uharibifu unafanyika.

Awali Mwenyekiti wa umoja wa Wazazi wilayani hapa, Imelda Mapunda naye alisema kuna umuhimu kwa wazazi wa wilaya hiyo kuendelea kuweka mkazo katika suala zima la elimu ikiwemo kupeleka watoto wa shule, na kutoa michango kwa wakati.

Mapunda alisema usimamiaji kikamilifu katika utekelezaji wa sera ya malezi mema kwa watoto na vijana ni jambo ambalo halipaswi kufanyiwa mzaha, hivyo jamii iungane kwa pamoja katika kulitekeleza hilo.

Pamoja na mambo mengine alieleza kuwa msimamo wa chama na jumuiya za CCM kwa pamoja kuhusu rasimu ya pili ya katiba, wao wanahitaji uwepo wa serikali mbili za Jamhuri ya muungano nasio vinginevyo.



No comments: