Tuesday, April 29, 2014

BARAZA LA MADIWANI MBINGA LAMTIMUA OFISA ELIMU SEKONDARI, LASEMA LIMEZINGATIA TAMKO LA WAZIRI

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa.

Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

HATIMAYE Baraza la Madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, limemaliza mzizi wa fitina kwa kumkataa aliyekuwa Ofisa elimu wa wilaya hiyo Hanji Yusuph Godigodi na kusema kuwa hawataki kumuona ndani ya wilaya hiyo, akiendelea kufanya kazi za utumishi wa umma.

Kukataliwa kwa Ofisa huyo kumefuatia baraza hilo kuketi kama kamati kwa muda wa nusu saa kujadili suala hilo, likizingatia tamko lililotolewa na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa, Februari 7 mwaka huu wakati alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo.

Jukumu la kuketi kama kamati lilifuatia kuwepo kwa mchezo mchafu ambao ulikuwa ukisukwa chini kwa chini na baadhi ya vigogo wa ngazi ya mkoa huo na wilaya, kwa lengo la kutaka kumrejesha madarakani Ofisa huyo ili aendelee na kazi yake kama kawaida.

Majaliwa alitoa tamko la kumvua madaraka kwa kumshusha cheo Ofisa huyo wa elimu sekondari wilayani humo, na wenzake sita ambao ni walimu wakuu wa shule za sekondari, kufuatia kushindwa kutekeleza majukumu yao ya kazi na kufanya ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 268 za maendeleo ya elimu ya sekondari.

NGAGA AWAPASULIA JIPU MADIWANI MBINGA



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amewataka Madiwani wa Halmashauri ya wilaya hiyo wasiwe watu wa kugeuka geuka, pale wanapoweka misimamo au misingi muhimu ya maendeleo ya wananchi wa wilaya hiyo.

Ngaga alisema kuwa kumekuwa na baadhi ya Madiwani wamekuwa wakishindwa kusimamia makubaliano halali ya vikao husika, badala yake muda mwingi huishia kulumbana na kuzungumzia mambo ambayo hayana tija kwa wananchi.

Kauli hiyo ya Mkuu wa wilaya Mbinga, ilitolewa leo alipokuwa akizungumza na Madiwani wa Halmashauri ya wilaya hiyo katika kikao cha baraza la madiwani hao kilichoketi leo, kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.

“Hii tabia sipendi, tujenge misimamo yetu katika vikao tusiende na manufaa ya mtu mmoja mmoja, tushirikiane katika hili ili mambo yetu yaende vizuri”, alisisitiza.

Friday, April 25, 2014

HALMASHAURI ZA AGIZWA KUONGEZA VYANZO VYA MAPATO

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Senyi Ngaga, akisisitiza jambo wakati alipokuwa akifungua mkutano wa ALAT wa mkoa huo, katikati ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo Allanus Ngahy na wa mwisho ni Katibu mkuu wa ALAT wa mkoa wa Ruvuma Mohamed Maje. (Picha na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

HALMASHAURI za wilaya mkoani Ruvuma zimeagizwa kuongeza vyanzo vipya vya mapato, ambavyo vitaweza kusaidia kuendesha halmashauri hizo na kuhudumia wananchi badala ya kutegemea ruzuku kutoka kwa wafadhili au serikali kuu.

Agizo hilo lilitolewa na Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga alipokuwa akifungua mkutano wa Jumuiya ya Serikali za Mitaa (ALAT)  ambao ulifanyika juzi katika ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani humo.

Ngaga alisema viongozi wa Halmashauri wasipokuwa wabunifu katika kuongeza mapato, hawataweza kwenda mbele na kutimiza malengo ya kuhudumia jamii ikiwemo ujenzi wa miundombinu kama vile barabara na miradi ya kilimo.

Wednesday, April 23, 2014

ALAT RUVUMA YALALAMIKIA MWENENDO WA BUNGE MAALUM LA KATIBA

Mwenyekiti wa ALAT mkoa wa Ruvuma, Oddo Mwisho. akisisitiza jambo kwenye kikao chao walichoketi leo Mbinga mjini. Anayefuatia ni mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo Allanus Ngahy na Katibu mkuu wa ALAT mkoani humo Mohamed Maje.

Na Kassian Nyandindi,

Ruvuma.

WAJUMBE wa jumuiya ya Serikali za mitaa (ALAT) mkoani Ruvuma, wamesikitishwa na mwenendo wa Bunge maalum la katiba ambalo linaendelea sasa mjini Dodoma, kwa kile walichoeleza kuwa hali hiyo inawakatisha tamaa wananchi.

Walisema asilimia kubwa ya wajumbe wa bunge hilo wamekuwa wakitumia muda mwingi nafasi wanazopewa bungeni, kutetea maslahi yao binafsi na sio kuisaidia jamii ambayo iliwaamini waende huko kutetea na kuwasilisha matatizo ya wananchi.

Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa ALAT wa mkoa huo Oddo Mwisho alipokuwa akisoma taarifa ya maendeleo ya jumuiya hiyo mbele Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, wakati wa mkutano wao wa siku moja uliofanyika kwenye ukumbi mdogo wa Halmashauri ya wilaya hiyo mkoani humo.

“Mheshimiwa mgeni rasmi pamoja na kukushukuru wewe binafsi kukubali kuwa mgeni wetu, tunakuomba utufikishie salamu zetu kwa serikali hasa kuhusu mwenendo wa Bunge letu la katiba unaoendelea bungeni hivi sasa sisi wanajumuiya hii hatufurahishwi nao”, alisema Mwisho.

Tuesday, April 22, 2014

ALAT RUVUMA YAANZA ZIARA YAKE YA KIKAZI WILAYANI MBINGA

Wajumbe wa Jumuiya ya serikali za mitaa (ALAT) mkoani Ruvuma, wakikagua moja kati ya jengo la kusomea watoto katika shule ya wasichana Kigonsera, iliyopo wilayani Mbinga ambayo inatarajia kuanza kuchukua wanafunzi watakaosoma masomo ya sayansi.

Mwenyekiti wa ALAT mkoa wa Ruvuma Oddo Mwisho aliyeinama upande wa kushoto, akiangalia moja kati ya meza ambayo itatumika kusomea wanafunzi wa masomo ya sayansi kwenye shule ya sekondari ya wasichana iliyopo katika kata ya Kigonsera wilayani Mbinga.

Baadhi ya Wajumbe wakiangalia mahindi yaliyolimwa na kikundi cha Muungano kilichopo kata ya Kigonsera wilayani humo.

Upande wa kulia aliyevaa suti nyeusi, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Hussein Ngaga akitoa maelezo mafupi kwa Wajumbe wa ALAT wa mkoa huo, juu ya maendeleo ya ujenzi wa Kituo kikuu cha magari ya abiria ambacho kimejengwa Mbinga mjini. Rais Jakaya Kikwete anatarajia kukifungua mapema mwezi Mei mwaka huu. (Picha zote na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAJUMBE wa Jumuiya ya Serikali za mitaa (ALAT) mkoani Ruvuma leo wameanza ziara ya kikazi kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani Mbinga mkoani humo.

Aidha licha ya kutembelea miradi hiyo wanatarajia ifikapo Aprili 23 mwaka huu, watafanya kikao chao kujadili maendeleo ya mkoa huo na kuweka mikakati madhubuti ya kusukuma mbele gurudumu la maendeleo, kwa faida ya wananchi wa mkoa huo na Taifa kwa ujumla.

Leo wakiwa katika ziara ya kukagua miradi hiyo wilayani Mbinga, wameweza kujionea shule ya Sekondari ya wasichana (Mbinga girls Secondary school) iliyopo katika kata ya Kigonsera wilayani humo ambayo itaanza kuchukua wanafunzi hivi karibuni.

Shule hiyo ni ya mchepuo wa masomo ya sayansi, inauwezo wa kuchukua wanafunzi 80 watakaosoma hapo na wenye kipaji cha masomo hayo.

Thursday, April 17, 2014

JELA MIAKA 30 KWA KOSA LA UBAKAJI



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MAHAKAMA ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imemhukumu kwenda jela kutumikia kifungo cha miaka 30 mkazi mmoja wa kijiji cha Mhekela wilayani humo, baada ya kupatikana na kosa la kubaka msichana mwenye umri wa miaka 14.

Hukumu hiyo ilitolewa na Hakimu Joackimu Mwakyolo mbele ya mwendesha mashtaka msaidizi wa Polisi Inspekta Nassib Kassim ambapo ilielezwa Mahakamani hapo kuwa, ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka umeona kwamba mshtakiwa anastahili kupewa adhabu ya kwenda jela kutumikia kifungo hicho. 

Mwakyolo alisema Wilson Ndunguru (32) ambaye ni mshtakiwa wa kosa hilo, alimbaka msichana mwenye umri wa miaka 14 mkazi wa mtaa wa Jimboni Mbinga mjini.

Saturday, April 12, 2014

MKUU WA MKOA RUVUMA ASEMA HAKUNA ATAKAYEWEZA KUFUTA AGIZO LA SERIKALI

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya waziri Mkuu Tawala za mikoa na Serikali za mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa upande wa kushoto, akiweka sahihi katika kitabu cha wageni alipowasili katika ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga ambaye ameketi upande wa kulia katika ziara yake ya kikazi wilayani humo.(Picha na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu amesema, hakuna mtu atakayeweza kutengua maamuzi yaliyotolewa na serikali juu ya kuvuliwa madaraka kwa aliyekuwa Ofisa elimu wa shule za sekondari wilayani Mbinga, na Walimu wakuu sita wa shule hizo ambao walihusika katika matumizi mabaya ya fedha za serikali.

Kauli hiyo ya Mwambungu ilifuatia Mwandishi wa habari hizi alipofanya naye mahojiano juu ya malalamiko yaliyotolewa na Wadau wa elimu wa wilaya hiyo kwa nyakati tofauti wilayani humo, baada ya kuona kumekuwa na njama zinazofanyika chini kwa chini katika jitihada za kutaka kuwarejesha madarakani watuhumiwa hao wanaodaiwa kutafuna fedha hizo.

“Hakuna anayeweza kufuta agizo hili lililotolewa na serikali hatua zitachukuliwa na uamuzi utabaki palepale”, alisema Mwambungu.

Serikali mnamo Februari 7 mwaka huu kupitia Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya waziri Mkuu Tawala za mikoa na Serikali za mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa, alichukua hatua ya kumvua madaraka kwa kumshusha cheo aliyekuwa Ofisa elimu Sekondari Hanji Yusuph Godigodi kwenda kuwa mwalimu wa kawaida akafundishe darasani na wenzake sita ambao ni walimu wakuu wa shule za sekondari, kufuatia kushindwa kutekeleza majukumu yao ya kazi na kufanya ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 268 za maendeleo ya elimu ya sekondari wilayani humo.

Friday, April 11, 2014

AGIZO LA WAZIRI TAMISEMI LA PUUZWA NJAMA ZAUNDWA KUWAREJESHA MADARAKANI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete.




















Na Kassian Nyandindi,

Ruvuma.


OFISI ya Katibu tawala mkoa wa Ruvuma na Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani humo, zimeshushiwa shutuma nzito kufuatia kudaiwa kupuuza na kutotekeleza kwa haraka agizo lililotolewa na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya waziri Mkuu Tawala za mikoa na Serikali za mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa, Mwandishi wetu amebaini.

Uchunguzi umebaini kuwa shutuma hizo zimetolewa baada ya kuonekana wazi kuwa kumekuwa na mchezo mchafu ambao unaendelea sasa, wa kutaka kutengua agizo hilo lililotolewa na Waziri huyo Februari 7 mwaka huu, juu ya kuvuliwa madaraka kwa baadhi ya viongozi wa idara ya elimu sekondari wilayani humo.

Uamuzi wa Serikali wa kumvua madaraka kwa kumshusha cheo aliyekuwa Ofisa elimu Sekondari Hanji Yusuph Godigodi na wenzake sita ambao ni walimu wakuu wa shule za sekondari, ulifuatia kushindwa kutekeleza majukumu yao ya kazi na kufanya ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 268 za maendeleo ya elimu ya sekondari wilayani humo.

Fedha hizo zilizotafunwa zililenga kufanya kazi ya kununua vitabu kwa shule za sekondari wilayani Mbinga, lakini inashangaza kuona kwamba utekelezaji husika kama serikali ilivyopanga haukufanyika.

Katika fedha hizo shilingi milioni 108 ilibidi zitumike kununua vitabu hivyo, na zinazobakia zifanye shughuli zingine za maendeleo husika katika shule hizo.

Tuesday, April 8, 2014

BENKI YA NMB YAENDELEA KUTOA MSAADA, YASISITIZA WANANCHI KUFUNGUA AKAUNTI

Timu ya uongozi wa benki ya NMB, katikati ni Meneja wa Kanda ya kusini Lillian Mwinula (aliyeketi kutoka upande wa kulia) na aliyesimama ni Meneja wa benki hiyo tawi la Litembo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma Victor Msoffe wakiwa wamewasili katika ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Nyasa Ernest Kahindi, ambaye ameketi upande wa kushoto. Wa kwanza kutoka kulia ni Mganga Mkuu wa wilaya hiyo John Papalika.

Mkuu wa wilaya ya Nyasa Ernest Kahindi (katikati) akipokea msaada wa vyandarua na mashuka ya kulalia wagonjwa katika hospitali ya wilaya hiyo, kutoka kwa Meneja wa NMB Kanda ya kusini Lillian Mwinula.

Meneja wa benki ya NMB Kanda ya kusini Lillian Mwinula, akizungumza na uongozi wa hospitali ya Nyasa (hawapo pichani) wakati wa makabidhiano ya vyandarua na mashuka ya kulalia wagonjwa katika hospitali hiyo. Kutoka kulia ni Meneja wa NMB tawi la Litembo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma Victor Msoffe. (Picha zote na Gwiji la matukio Ruvuma)
Na Kassian Nyandindi,

Nyasa.

ZOEZI la utoaji wa mashuka na vyandarua katika Hospitali ikiwa ni lengo la kuwasaidia wagonjwa waweze kuwa na mazingira mazuri ya kulala pale wanapolazwa wodini, leo limeendelea kufanyika wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, ambapo benki ya NMB hapa nchini kupitia tawi lake la Mbinga imetoa msaada huo wilayani humo.

Jumla ya mashuka 30, vyandarua nane na foronya 30 vimetolewa na benki hiyo na kukabidhi kwa uongozi wa hospitali ya wilaya hiyo huku makabidhiano hayo yakishuhudiwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Ernest Kahindi.

Wilaya hiyo ambayo inakabiliwa na changamoto lukuki katika sekta ya afya ikiwemo uhaba wa majengo ya kutolea huduma hiyo muhimu vilevile  magodoro, mashuka na mablanketi ya kulalia wagonjwa zinahitajika jitihada za makusudi zifanyike kwa haraka ili kuweza kunusuru hali hiyo.

Monday, April 7, 2014

CCM MBINGA YAPONGEZA JITIHADA ZA UDHIBITI UTOROSHWAJI ZAO LA KAHAWA, YATOA MSIMAMO WA SERIKALI MBILI KATIBA IJAYO

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Juma Mpeli.

















Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

SERIKALI wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, imepongezwa kwa jitihada zake za kudhibiti biashara haramu ya magendo ya kahawa iliyokuwa ikifanyika wilayani humo na wafanyabiashara wajanja, na kuwasababishia wakulima wa zao hilo washindwe kusonga mbele kimaendeleo.

Juu ya udhibiti huo, imeelezwa kuwa hivi sasa wakulima wataweza kuuza kahawa yao kwa bei nzuri na kuwafanya waweze kuwa na kipato na hata wilaya, kuweza kukusanya mapato yake kwa urahisi.

Hayo yalisemwa na Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga mkoani humo, Juma Mpeli alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Alisema Halmashauri kuu ya chama hicho hapa wilayani, imepokea taarifa kutoka kwa uongozi wa wilaya ya Mbinga juu ya mipango waliyonayo ya kilimo cha zao la kahawa, na kuunga mkono jitihada hizo ambazo zinaendelea kufanywa ikiwemo suala hilo la kudhibiti utoroshwaji wa zao la kahawa.

UMOJA WA WAZAZI MBINGA WAITAKA JAMII KUTILIA MKAZO SUALA LA ELIMU NA UPANDAJI MITI KATIKA VYANZO VYA MAJI


Aliyevaa shati la kijani ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbinga mkoa wa Ruvuma, akiwa ameongozana na viongozi wenzake wa chama, wakiangalia mchezo wa ngoma ya asili iitwayo Mhambo katika maadhimisho ya sherehe za umoja wa Wazazi zilizofanyika hapa wilayani kijiji cha Mundeki kata ya Myangayanga wilayani humo. (Picha zote na Gwiji la matukio Ruvuma)
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

UMOJA wa Wazazi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, umewataka wananchi wa wilaya hiyo kutunza na kuendeleza mazingira kwa maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Aidha imesisitizwa kuwa katika kufanikisha hilo, viongozi wa serikali waliopo katika maeneo mbalimbali katika vijiji na kata wahakikishe kwamba wanahamasisha watu kupanda miti iliyo rafiki ya maji, katika vyanzo vya maji na vilele vya milima.

Rai hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa wilaya ya Mbinga, Christantus Mbunda alipokuwa mgeni rasmi akihutubia katika maadhimisho ya sherehe za umoja huo yaliyofanyika katika kijiji cha Mundeki kata ya Myangayanga wilayani humo.

NMB YATOA MSAADA HOSPITALI NA SHULE YA MSINGI YA WATAKA WAZAZI KUWAFUNGULIA AKAUNTI WATOTO WAO

Meneja wa NMB Kanda ya kusini, Lillian Mwinula akisisitiza jambo wakati wa kukabidhi msaada wa madawati, shuka na vyandarua alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma. Upande wa kushoto ni Meneja wa benki hiyo tawi la Mbinga Lugano Mwampeta na kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri  ya wilaya ya Mbinga Oscar Yapesa.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Oscar Yapesa upande wa kulia, akipokea msaada wa vyandarua kutoka kwa Meneja wa NMB Kanda ya kusini Lillian Mwinula.

Baadhi ya akina mama Wajawazito nao wakishuhudia makabidhiano ya vyandarua na mashuka katika hospitali ya wilaya ya Mbinga.

Upande wa kulia Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga Oscar Yapesa akipokea msaada wa madawati 50 kutoka kwa Meneja wa Kanda ya kusini wa NMB, Lillian Mwinula kwa ajili ya matumizi kwa wanafunzi wa shule ya msingi Komboa iliyopo kata ya Ruanda wilayani humo.

Wanafunzi wa shule ya Msingi Komboa wakiimba wimbo wa kushukuru mara baada ya kukabidhiwa madawati hayo.


Lillian Mwinula ambaye ni Meneja wa NMB Kanda ya kusini, akiwa pamoja na wanafunzi wa shule ya msingi Komboa mara baada ya kuwakabidhi madawati.

Wanafunzi wa shule ya msingi Komboa iliyopo kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakiwa wameketi katika madawati hayo, mara baada ya kukabidhiwa na benki ya NMB. (Picha zote na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.


BENKI ya NMB tawi la Mbinga mkoa wa Ruvuma, imetoa msaada wa Madawati 50 yenye thamani ya shilingi milioni tano kwa shule ya msingi Komboa iliyopo kata ya Ruanda wilayani humo, ikiwa ni lengo la kuboresha mazingira ya kusomea wanafunzi katika shule hiyo.

Sambamba na hilo pia imetoa msaada wa mashuka 30 na vyandarua 10 katika hospitali ya wilaya hiyo, kwa ajili ya akina mama wajawazito ambao husubiri siku ya kujifungua na kupata matibabu katika hospitali hiyo.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi vitu hivyo Meneja wa benki hiyo Kanda ya kusini, Lillian Mwinula alisema NMB kila mwaka imejiwekea utaratibu wa kurudi kwa wananchi pale inapopata faida yake, kwa njia ya kutoa misaada ya aina mbalimbali.

Wednesday, April 2, 2014

WANAFUNZI WAPIGA MKUU WA SHULE NA KUSABABISHA UHARIBIFU WA MALI, SHULE YAFUNGWA KWA MUDA



Na Kassian Nyandindi,

Songea.

WANAFUNZI wa shule ya sekondari ya Village School of Tanzania (VST) iliyopo katika kijiji cha Unango wilayani Mbinga  mkoa wa Ruvuma wamefanya fujo kwa kumpiga  mkuu wao wa shule, na kuvunja baadhi ya samani za shule  hiyo huku wakisababisha  uharibifu mkubwa wa mali za shule na walimu wao.

Kamanda wa Polisi wa mkoa huo Akili Mpwapwa  alisema kuwa  tukio hilo limetokea mwishoni mwa wiki iliyopita majira ya saa za usiku katika kijiji hicho.

Alisema kuwa siku hiyo ya tukio  wanafunzi wa kidato cha tatu na nne  wa shule hiyo walifanya fujo na kusababisha mali za shule pamoja na za walimu wao kuharibiwa  ambapo nyumba mbili za walimu  zilivunjwa milango na madirisha.

Wanafunzi  hao walivunja kompyuta na kuchana  vitabu mbalimbali  na nguo za walimu wao na kusababisha fedha shilingi milioni mbili kupotea.