Wednesday, January 25, 2017

BENKI YA CRDB KUWAFUNGULIA MASHTAKA MBINGA KURUGENZI SACCOS

Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

MENEJA Mahusiano wa benki ya CRDB Kanda ya Nyanda za juu kusini, Hassanaly Japhary amesema kuwa ameshangazwa na kauli ya Wajumbe wa bodi ya Chama cha ushirika Mbinga Kurugenzi SACCOS, kwamba hawazitambui baadhi ya nyaraka za benki hiyo ambazo zilitumika kuwapatia mkopo wa shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuwakopesha wanachama wa ushirika 

Alifafanua kuwa kauli hiyo ya kushangaza ilitolewa na Wajumbe hao katika mkutano wao maalumu uliofanyika mjini hapa na kwamba benki hiyo, haipo tayari kuchafuka kwa mambo hayo badala yake itafungua mashtaka dhidi ya matumizi mabaya ya fedha za mkopo huo, yaliyofanywa na Wajumbe hao kwa kujinufaisha wao binafsi badala ya kuwakopesha wanachama wa SACCOS hiyo.

Hassanaly alisema hayo juzi alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari mara baada ya kusomwa taarifa ya ukaguzi juu ya mwenendo wa Chama hicho cha ushirika ambayo ilibainisha wizi wa fedha zilizotokana na mkopo huo shilingi milioni 405,204,514 katika mkutano mkuu maalumu wa wanachama, uliofanyika kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa.

“Benki hatupo tayari kuchafuka kwa mambo haya, sisi kama benki nasi tutahakikisha tunafungua mashtaka mahakamani dhidi ya wizi huu uliofanyika hapa Mbinga katika SACCOS hii ili tuweze kurejesha fedha zetu”, alisisitiza Hassanaly.

CCM RUVUMA YAENDELEA KUVIBWAGA CHINI VYAMA VYA UPINZANI

Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Ruvuma, kimeibuka na ushindi wa kishindo baada ya wagombea wake wa nafasi za udiwani kushinda katika kata mbili ya Tanga, iliyopo Manispaa ya Songea na Maguu wilayani Mbinga mkoani humo.

Uchaguzi huo ulifanyika Januari 22 mwaka huu ambapo katika kata ya Maguu msimamizi wa uchaguzi huo, Caspary Mahay alimtangaza Manfred Kahobela kuwa mshindi kupitia tiketi ya CCM baada ya kujizolea kura 2,355 na kumbwaga chini Bahati Mbele wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) aliyepata kura 1,717.

Katika kata ya Tanga msimanizi wa uchaguzi huo, Tina Sekambo alimtangaza Agaton Goliyama kwa tiketi ya Chama cha mapinduzi kuwa mshindi baada ya kupata kura 1,867 huku akiwashinda wagombea wa Chama cha demokrasia na maendeleo Vinitan Soko aliyepata kura 722, ACT Wazalendo Swaiba Mapunda kura 2 na Adolf Ngonyani wa CUF aliyepata kura 15.

Sunday, January 22, 2017

BREAKING NEWS: WAJUMBE WA BODI MBINGA KURUGENZI SACCOS WASWEKWA RUMANDE KWA TUHUMA YA WIZI WA MAMILIONI YA FEDHA

Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

WATUMISHI saba wanaotoka katika Halmashauri ya mji wa Mbinga, wilaya ya Mbinga na Nyasa mkoani Ruvuma ambao pia ni Wajumbe wa bodi ya Chama cha ushirika Mbinga Kurugenzi SACCOS iliyopo mkoani hapa, wamekamatwa na kuwekwa mahabusu wakituhumiwa kuiba shilingi milioni 405,204,514 za wanachama wa chama hicho na kusababisha hasara kubwa kwa SACCOS hiyo kushindwa kujiendesha kwa manufaa ya wanachama.

Cosmas Nshenye Mkuu wa wilaya ya Mbinga.
Aidha hatua hiyo ya kukamatwa kwa Wajumbe hao ilitolewa na Mrajisi msaidizi wa vyama vya ushirika mkoani humo, Biezery Malila baada ya kusomwa taarifa ya ukaguzi juu ya mwenendo wa chama hicho cha ushirika ambayo ilibainisha wizi wa fedha hizo katika mkutano mkuu maalumu wa wanachama, uliofanyika Januari 21 mwaka huu kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa.

“Kwa masikitiko makubwa ndugu zangu naomba niwaeleze kwamba mwenendo wa chama hiki sio mzuri kwa kuwa wajumbe wa bodi hii wameshiriki kwa namna moja au nyingine kukiuka taratibu za uendeshaji wa chama hiki, hivyo wanapaswa kuwajibika kwa mujibu wa sheria na taratibu husika za vifungu vya uendeshaji wa vyama vya ushirika”, alisema Malila.

Mrajisi huyo wa vyama vya ushirika mkoa wa Ruvuma alifafanua kuwa fedha hizo ambazo wajumbe hao wanadaiwa kujinufaisha kwa matakwa yao binafsi zilitokana na mkopo wa shilingi milioni 500 uliotolewa na benki ya CRDB kwa ajili ya kukopeshwa wanachama lakini cha kushangaza waliamua kuzitumia kinyume na taratibu husika.

Pia alimtaja mtuhumiwa mwingine wa nane ambaye sio mtumishi wa serikali na ni Meneja wa SACCOS hiyo kuwa ni, Raymond Mhagama ambapo ametoroka kufuatia kuwepo kwa kesi ya ubadhirifu wa fedha hizo na kwamba madai yake ya kutoroka huko yamefunguliwa Kituo kikuu cha Polisi wilaya ya Mbinga na kwamba, anatafutwa popote pale alipo ili aweze kukamatwa na kujibu tuhuma hizo zinazomkabili mbele yake.

MANISPAA SONGEA YAPITISHA BAJETI SHILINGI BILIONI 63 KWA AJILI YA MAENDELEO YA WANANCHI

Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

BARAZA la Madiwani katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma limepokea, kujadili na kupitisha bajeti ya mwaka 2017/2018 zaidi ya shilingi bilioni 63.7 kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo ya wananchi katika halmashauri hiyo.

Akiwasilisha bajeti hiyo Mchumi Mkuu wa Manispaa hiyo, Raphael Kimary alibainisha kuwa kati ya fedha hizo zaidi ya shilingi bilioni 16 ni kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambazo ni ruzuku kutoka serikali kuu na shilingi bilioni 1.785 ni fedha pia za utekelezaji maendeleo ya wananchi.
Mchumi Mkuu wa Manispaa ya Songea, Raphael Kimary akiwasilisha bajeti.

Kwa mujibu wa Kimary alieleza kuwa fedha za matumizi ya kawaida ambazo ni ruzuku kutoka serikali kuu zimetengwa zaidi ya shilingi bilioni 3.893 na matumizi ya kawaida kutoka vyanzo vya ndani zimetengwa shilingi bilioni 1.533.

Alisema kuwa mishahara ya watumishi wametenga shilingi bilioni 40 na nguvu za wananchi zimetengwa shilingi milioni 175.

WAKAZI MANISPAA SONGEA WATAKA MKANDARASI AMALIZE UJENZI WA BARABARA KWA WAKATI ULIOPANGWA

Na Mwandishi wetu,     
Songea.

BAADHI ya wakazi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wameuomba uongozi wa Manispaa hiyo kumuhimiza Mkandarasi wa kampuni ya Lukoro Construction Limited, ambayo imepewa kazi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami mjini hapa kukamilisha ujenzi huo kwa wakati uliopangwa.

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini hapa wakazi wa maeneo ya Matarawe, Bombambili, Mateka na Matogoro walisema kuwa licha ya kuwa kazi hiyo inayofanywa na mkandarasi huyo inaendelea kufanyika, lakini bado jitihada zinahitajika kuona namna ya kumaliza ujenzi huo mapema wakidai kuwa mvua zitakapoanza kunyesha kwa wingi zinaweza kusababisha kuchelewa kukamilisha ujenzi huo.

Amina Komba mkazi wa eneo la Matarawe alisema kuwa Kampuni ya ukandarasi ya Lukoro kwa muda mrefu ilianza kutengeneza barabara ya kutoka Bombambili hadi Mwembechai, lakini mpaka sasa bado haijakamilika licha ya kuwa kuna baadhi ya maeneo ya barabara hiyo imeanza kuharibika.

John kapinga mkazi wa eneo la Mateka naye alisema kuwa licha ya Kampuni hiyo kuanza kujenga barabara ya kutoka shule ya sekondari ya wasichana ya Songea hadi Matogoro haijakamilika nayo ujenzi wake kwa kiwango hicho cha lami.

Saturday, January 21, 2017

SONGEA WAIOMBA WIZARA KUWAPELEKEA WALIMU MASOMO YA SAYANSI

Na Kassian Nyandindi,   
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, inakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu wa masomo ya sayansi na hisabati katika shule za sekondari jambo ambalo linarudisha nyuma, maendeleo ya mkoa huo kwa watoto wanaopenda kusoma masomo hayo.

Aidha imeelezwa kuwa mahitaji ya walimu wa masomo ya sayansi katika Manispaa hiyo ni walimu 375 ambapo waliopo sasa ni 132 tu, hivyo kuwa na upungufu wa walimu 243.

Ofisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo amewaeleza waandishi wa habari kuwa Manispaa ina ziada ya walimu 192 wa masomo ya sanaa, katika shule za sekondari ambapo mahitaji ya walimu katika masomo hayo ni 536 wakati walimu waliopo ni 728.

MANISPAA SONGEA YAWEKA MKAKATI KUIMARISHA USAFI WA MAZINGIRA

Na Muhidin Amri,      
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imedhamiria kuhakikisha kwamba inaongeza kasi juu ya suala la usafi wa mazingira katika Manispaa hiyo ambapo imejiwekea mkakati wa kununua kijiko kimoja cha kuzolea taka, kwa shilingi milioni 170 ili kuweza kurahisisha kazi ya uzoaji taka kwenye maeneo mbalimbali.

Ofisi za halmashauri ya mji wa Songea.
Aidha katika bajeti ya mwaka 2016/2017 imeweza kutenga fedha hizo ambazo watahakikisha kifaa hicho kinanunuliwa mapema, kwa lengo la kuufanya mji wa Songea uendelee kuwa safi wakati wote.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Ofisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo alisema kuwa pamoja na kuweka mikakati hiyo pia wamekuwa wakihamasisha wananchi kutokiuka kanuni na sheria za afya zilizowekwa ambazo zinaifanya jamii iendelee kuishi bila kushambuliwa na magonjwa ya mlipuko kutokana na kuzingatia masuala ya usafi.

Friday, January 20, 2017

MKUU WA WILAYA NAMTUMBO ATISHIWA KIFO

Na Kassian Nyandindi,      
Namtumbo.

MKUU wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Luckness Amlima ametishiwa kifo kwa maneno na mwananchi mmoja wa wilaya hiyo Gerold Haulle wakati alipokuwa akitekeleza zoezi la kuwahamisha wananchi wanaofanya shughuli za kibinadamu kwenye chanzo cha maji, ambacho ni tegemeo kubwa kwa hifadhi ya maji kwa wakazi wa mji wa Namtumbo.

Ofisa habari wa wilaya hiyo Yeremias Ngerangera alisema kuwa tukio hilo lilitokea Januari 19 mwaka huu majira ya mchana wakati Mkuu huyo wa wilaya alipokuwa ofisini kwake na mwananchi huyo, akimhoji na kumtaka asitishe shughuli zake za kilimo ambazo amekuwa akizifanya kwenye chanzo kikuu cha maji ya mto Rwinga uliopo wilayani humo.

Ngerangera alifafanua kuwa hatua ya kumtaka Haulle aondoke kwenye chanzo hicho cha maji kimefuatia kuwepo kwa malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi na Mamlaka ya maji ya wilaya hiyo kwamba, amekuwa akikataa kuondoka kwenye chanzo na kukaidi maagizo yanayotolewa na serikali kuacha kufanya shughuli yoyote mita sitini kutoka kwenye maeneo yenye vyanzo vya maji.

TANESCO MBINGA KUENDELEA KUBORESHA HUDUMA YA UMEME KWA WANANCHI WAKE

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (kushoto) akisikiliza maelezo kutoka kwa Kanuti Punguti ambaye ni Meneja wa kituo cha kufua umeme wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, alipotembelea hivi karibuni akiwa katika ziara yake ya kikazi kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme katika wilaya hiyo.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa Ofisi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, inaendelea na mikakati yake ya kufikisha huduma ya nishati ya umeme kwa wananchi wa mjini na vijijini wilayani humo, ambao bado hawajafikiwa na huduma hiyo ili waweze kuwa na maendeleo.

Aidha serikali kupitia mpango wake wa usambazaji umeme vijijini (REA) awamu ya tatu, shirika hilo linatarajia kuwafikia wananchi wa vijiji 146 vilivyopo wilayani hapa na kwamba wametakiwa kuacha kuzuia maeneo yao kupitisha nguzo za umeme kwa malengo ya kudai fidia, wakati miradi hiyo haina fidia ya aina yoyote ile.

Hayo yamesemwa na Meneja wa TANESCO tawi la Mbinga, Kanuti Punguti wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ambapo alieleza kuwa hadi sasa shirika hilo limewafikia wateja 5,612 wanaopata huduma ya umeme wilayani humo.

MARTIN MSUHA NA MTAZAMO WA KUIJENGA UPYA MBINGA VIJIJINI

Mbunge wa jimbo la Mbinga vijijini mkoani Ruvuma, Martin Msuha akizungumza na wananchi wa kata ya Maguu na Mbuji juu ya mpango wa serikali unaowataka wakubali kupima maeneo yao ili waweze kuwa na hati miliki na kuweza kuondoa migogoro isiyokuwa ya lazima katika jamii, Msuha alikuwa katika ziara yake ya kikazi ya kuwatembelea wananchi wa jimbo hilo kwa lengo la kuhamasisha shughuli mbalimbali za kimaendeleo.  (Picha na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,

NOVEMBA 5 mwaka jana Rais Dkt. John Magufuli ametimiza mwaka mmoja tangu aingie madarakani, alipochaguliwa kushika wadhifa huo baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka 2015 ambao pia ulivishirikisha vyama mbalimbali vya upinzani.

Kama inavyofahamika wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita Rais huyo aliahidi masuala ambayo angeyatekeleza mara tu baada ya Watanzania kukipatia ridhaa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuongoza nchi, ambapo mpaka anatimiza mwaka mmoja baada ya kuingia madarakani amefanikiwa kutimiza ahadi zake kwa asilimia kubwa na hivyo kuwafanya wananchi kuendelea kujenga imani kwa kiongozi huyo.

Wakati Watanzania hao wakishuhudia utendaji kazi wa kizalendo ambao umekuwa ukiendelea kutekelezwa na Dkt. Magufuli, Wabunge nao kwa upande wao wanapaswa kujitathimini na kueleza nini hasa wamewafanyia wananchi wao  waliowachagua tangu walipoingia madarakani mara baada ya uchaguzi mkuu kufanyika Oktoba 25 mwaka 2015.

Ikumbukwe kwamba ushindi huo wa CCM ulitokana na Watanzania hawa kuwa na imani kubwa na chama hicho, hivyo kinachotakiwa sasa kwa viongozi wake ni kuendelea kutekeleza kwa vitendo yale yote ambayo yameainishwa ndani ya Ilani ya uchaguzi huo sambamba na yale ambayo waliahidi wao binafsi.

Katika uchaguzi huo mkuu ambao wabunge, madiwani na Rais walichaguliwa zipo pia ahadi mbalimbali zilitolewa kwa madai kwamba wangezitekeleza mara tu wakichaguliwa na kuingia madarakani, sasa ni vyema kila baada ya kipindi fulani viongozi hao ni muhimu wakayatafakari yale yote ambayo wameyafanya ili wananchi waweze kuyafahamu.

Katika makala haya, mmoja kati ya Wabunge ambao walitoa ahadi kwa wananchi wakati wa kuomba ridhaa ya kushika nafasi hiyo ya uwakilishi wa kuongoza wananchi, Mbunge wa jimbo la Mbinga vijijini mkoani Ruvuma, Martin Msuha ambaye alipeperusha bendera ya CCM na kuonekana kuwa mshindi katika kinyang’anyiro hicho mara baada ya uchaguzi huo kufanyika.

WAFANYABIASHARA SONGEA WAIOMBA SERIKALI KUWEKA UTARATIBU WA MAKAMPUNI YA TANCOAL ENERGY NA MANTRA KULIPIA KODI RUVUMA

Kamishna wa kodi za ndani wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Elijah Mwandumbya akizungumza na wafanyabiashara wa Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kwenye ukumbi wa mikutano wa Songea Club uliopo mjini hapa, upande wa kushoto kwake ni Naibu Kamishna mkuu wa TRA Charles Kichele.
Na Mwandishi wetu,      
Songea.

WAFANYABIASHARA katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wameiomba serikali kuweka utaratibu kwa makampuni mawili yanayojishughulisha na uchimbaji madini mkoani hapa, kulipia kodi mkoani humo badala ya Dar es salaam ili yaweze kusaidia kupunguza makali ya shilingi bilioni 12 ambazo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Ruvuma imepangiwa kukusanya mwaka huu toka kwa wafanyabiashara hao.

Ombi hilo lilitolewa jana na wafanyabiashara hao kwenye mkutano uliofanyika baina yao na uongozi wa TRA makao makuu jiji Dar es Salaam, uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Songea Club uliopo mjini hapa.

Akichangia hoja kwenye mkutano huo mmoja wa wafanyabiashara hao Jaribu Mangoma alisema kuwa kutokana na kitendo cha serikali kuyaachia makampuni ya TANCOAL Eenergy inayojishughulisha na uchimbaji wa makaa ya mawe katika mgodi wa Ngaka uliopo kijiji cha Ntunduaro wilayani Mbinga na kampuni ya MANTRA inayofanya utafiti wa upatikanaji wa madini aina ya Urani, eneo la mto Mkuju wilayani Namtumbo ndiyo yanayochangia wafanyabiashara kukadiriwa kodi kubwa ambayo inawafanya baadhi yao wafilisike na wengine kufunga maduka yao.

Tuesday, January 17, 2017

MADUDU YA TASAF MBINGA YAITIA HASARA SERIKALI MAMILIONI YA FEDHA

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye.
Na Kassian Nyandindi,        
Mbinga.

SERIKALI wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma imesema kuwa tokea ulipoanza mfumo wa kuziwezesha kaya maskini wilayani humo kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) awamu ya tatu imepata hasara ya shilingi milioni 59,936,000 ambazo walikuwa wakilipwa walengwa hewa wasiokuwa na sifa.

Aidha kufuatia hali hiyo imefanikiwa kuokoa kiasi cha shilingi milioni 26,474,000 katika kila awamu ya uhaulishaji fedha kwa kaya hizo maskini na wilaya imeweza kurejesha shilingi milioni 4,784,000 kutokana na walengwa hao kukosa sifa.

Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa wilaya hiyo, Cosmas Nshenye alisema kuwa kufuatia kuwepo kwa tatizo hilo serikali imechukua hatua ya kumsimamisha kazi Mratibu wa TASAF wilaya, Ahsante Luambano ambaye anadaiwa kuzembea katika kusimamia majukumu yake ya kazi ipasavyo ili kupisha uchunguzi.

CHAWATASO YALIA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA YAITAKA SERIKALI KUDHIBITI WANAOCHOMA MISITU

Na Mwandishi wetu,    
Songea.

CHAMA cha Waganga wa jadi, wakunga na mangariba wa tiba asilia mkoani Ruvuma (CHAWATASO) kimetoa rai kwa serikali kuweka sheria kali itakayoweza kuwadhibiti watu wanaochoma misitu na kukata miti hovyo.

Mwenyekiti wa chama hicho, Mustafa Kafimbo amesema kuwa endapo hatua zisipochukuliwa za kudhibiti vitendo hivyo vya uharibifu wa misitu hali hiyo itasababisha miti mingi iliyokuwa ikitumika kutengenezea dawa kupotea na kuwa kero katika jamii.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti huyo wa CHAWATASO alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wao uliofanyika mjini hapa huku akiongeza kuwa dawa nyingi ambazo hutumika katika jamii, zinatokana na majani ya miti asilia na mizizi hivyo vitendo vya ukataji wa miti na kuchoma misitu havipaswi kuendelea kufumbiwa macho.

Kafimbo ameiomba pia serikali kukitambua chama chao ambacho kilisajiliwa mwaka 2008 na kupewa namba ya usajili 17NGO/0441 kikiwa na jumla ya wanachama waanzilishi 13 mkoani hapa ambapo hivi sasa chama hicho kina wanachama 348.

Sunday, January 15, 2017

WAZIRI WA ARDHI ASISITIZA WANAOKAIDI MBINGA KULIPA KODI YA ARDHI WAFIKISHWE MAHAKAMANI

Dkt. Angelina Mabula, Naibu Waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi.
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

NAIBU Waziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi Dkt. Angelina Mabula ameuagiza uongozi wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, uhakikishe kwamba unatoa notisi kwa watu wote katika wilaya hiyo ambao hawajalipa kodi ya ardhi, ili waweze kulipa kwa wakati uliopangwa na kwa wale ambao watakaidi kulipa wapelekwe mahakamani.

Aidha alifafanua kuwa suala la kulipa kodi ya serikali ni lazima na sio hiari na kwamba katika wilaya hiyo kuna jumla ya shilingi milioni 500 zipo nje kwa wadaiwa wa kodi ya ardhi ambao wamemilikishwa viwanja kisheria na hawataki kulipa kodi husika kwa wakati.

Agizo hilo lilitolewa jana na Dkt. Mabula wakati alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani hapa, akizungumza na wananchi wa Mbinga na viongozi wa wilaya kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.

Dkt. Mabula alisisitiza pia katika kupunguza kero na migogoro ya ardhi ni vyema sasa viongozi husika ambao wamepewa dhamana ya kushughulikia masuala ya ardhi, wawafikie wananchi mara kwa mara kwenye maeneo yao na kutatua matatizo hayo yaliyopo kwa wakati.

HALMASHAURI MAFIA YAJIWEKEA MIKAKATI YA KUONGEZA UZALISHAJI WA MAZAO



Na Julius Konala,  
Mafia.

HALMASHAURI ya wilaya ya Mafia mkoani Pwani, imejiwekea mikakati mbalimbali ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya biashara wilayani humo kutoka zao moja la nazi linalozalishwa sasa, hadi kufikia matatu ikiwemo zao la korosho kwa lengo la kuinua pato la halmashauri hiyo.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Erick Mapunda alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na gazeti hili ofisini kwake wilayani Mafia kwa lengo la kuelezea shughuli mbalimbali za maendeleo zinazofanywa na halmashauri hiyo.

Aidha Mapunda alisema kuwa mpaka sasa tayari wamekwisha tenga kiasi cha fedha kwa ajili ya kununulia kilo 200 za mbegu ya korosho, ambapo zitaweza kuzalisha  miche 1000 ambayo itagawiwa bure kwa wananchi na taasisi za shule.

Monday, January 9, 2017

SERIKALI KUICHUKULIA HATUA KAMPUNI YA TANCOAL ENERGY

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiagana na Mkuu wa mafunzo na utendaji kivita wa brigedi ya Tembo Songea mkoani Ruvuma, Kanali Samwel Makabala katika uwanja wa ndege wa Songea jana mara baada ya Waziri Mkuu kuhitimisha ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani hapa.
Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameitaka kampuni inayojishughulisha na uchimbaji wa madini ya makaa ya mawe Tancoal Energy, kwenye mgodi wa Ngaka wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kutekeleza makubaliano ambayo yapo kwenye mikataba kabla serikali haijachukua hatua zaidi.

Agizo hilo lilitolewa na Waziri Mkuu Majaliwa jana alipokuwa akizungumza na viongozi mbalimbali wa mkoa huo kwenye kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku nne ya kikazi mkoani hapa, ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo ambapo alisisitiza kuwa endapo kampuni hiyo haitatekeleza makubaliano husika ya mikataba iliyoingia na serikali, italazimika kuizuia isiendelee na kazi ya uchimbaji wa makaa hayo na kuitafuta kampuni nyingine ambayo itaridhia makubaliano ambayo yataleta manufaa kwa Watanzania juu ya uendeshaji wa mgodi huo.

“Nilipata fursa ya kukagua shughuli mbalimbali za mgodi wa makaa ya mawe wa Ngaka nimejionea mwenyewe shughuli za uchimbaji wa makaa haya na uzalishaji wa umeme unaotekelezwa na kampuni ya Tancoal Energy, ambayo ni kampuni ya ubia kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) na kampuni ya Pacific Coparation East Africa ya Australia”, alisema Majaliwa.

Pia alieleza kuwa pamoja na kazi nzuri inayofanyika kwenye mgodi huo, amebaini kuwepo kwa mapungufu mengi yakiwemo Shirika hilo la maendeleo la taifa kutolipwa gawio lake (Dividend) tangu ulipoanza uzalishaji wa makaa hayo mwaka 2011.

Sunday, January 8, 2017

MAJALIWA: VIONGOZI BODI YA KOROSHO WAKAMATWE

Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameuagiza uongozi wa serikali ya mkoa wa Mtwara kuwakamata mara moja viongozi wanne wa Bodi ya zao la korosho Tanzania, akiwemo Kaimu Meneja mkuu wa Chama cha ushirika wilaya ya Masasi (MAMCU) mkoani humo Kelvin Rajab baada ya kubaini kuwepo mapungufu makubwa ya wizi wa korosho za wakulima.

Aidha aliwataja viongozi wengine watatu ambao Waziri Mkuu huyo alisema kuwa wameshiriki kwa namna moja au nyingine kuhujumu korosho hizo za wakulima na wanapaswa kukamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya dola kuwa ni Lawrence Njozi ambaye ni Meneja wa tawi chama kikuu cha ushirika MAMCU, Yusuph Namkukula ambaye ni Mkurugenzi na Ramadhan Namakweto wa kampuni ya YURAP ambayo ilikuwa ikishiriki kwenye minada ya manunuzi ya zao hilo.

Majaliwa alitoa agizo hilo leo alipokuwa kwenye kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku nne ya kikazi mkoani Ruvuma, kwenye ukumbi wa mikutano Ikulu ndogo mjini Songea.

Saturday, January 7, 2017

MKURUGENZI NDC AKALIA KUTI KAVU WAZIRI MKUU ABAINI MADUDU MGODI MAKAA YA MAWE MBINGA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiangalia makaa ya mawe katika mgodi wa Ngaka yanayochimbwa na kampuni ya Tancoal Energy, kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga jana alipotembelea mgodi huo kwa ajili ya kujiridhisha kama kamapuni hiyo inalipa kodi kwa serikali ipasavyo na kubaini kwamba tangu mwaka 2011 mgodi huo ulipoanza ulipaji wake wa kodi umekuwa ni tatizo.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

MKURUGENZI Mtendaji wa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) Mlingi Mkucha amejikuta akiwa katika wakati mgumu baada ya kushindwa kutolea ufafanuzi mbele ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa juu ya kodi ya gawio la serikali inayopatikana katika mgodi wa makaa ya mawe Ngaka uliopo katika kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma.

Aidha kufuatia hali hiyo, serikali hapa nchini imesema kuwa itamtuma Gavana wake wa Benki kuu pamoja na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwenda kufuatilia mwenendo mzima wa fedha za kodi ya serikali katika mgodi huo, ili kuweza kujiridhisha kama kodi hiyo ilikuwa inalipwa serikalini ipasavyo au la.

Hayo yalijitokeza jana mbele ya Waziri Mkuu, Majaliwa alipokuwa katika ziara yake ya kikazi mkoani hapa, baada ya kutembelea mgodi huo kwa lengo la kujionea maendeleo yake na changamoto mbalimbali zilizopo ambapo alisema kuwa endapo ukweli ukibainika baada ya ukaguzi kufanyika, wahusika walioshiriki kukwepa kulipa kodi hiyo watawajibika kulipa tangu mgodi huo ulipoanza.

Thursday, January 5, 2017

MAJALIWA AZIAGIZA HALMASHAURI NCHINI KUTAMBUA VYANZO VYA MAJI NA KUHIFADHI VISIHARIBIWE

Wananchi wa kijiji cha Magingo na Mkongotema wakimlaki Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa baada ya kuwasili katika kijiji hicho kufungua mradi mkubwa wa maji uliogharimu shilingi bilioni 1.9 ambao utahudumia wananchi wa vijiji hivyo viwili.
Na Kassian Nyandindi,          
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameagiza Halmashauri zote za wilaya hapa nchini zitambue vyanzo vyote vya maji na hatimaye vitunzwe na kuhifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na baadaye.

Aidha Majaliwa amesema kuwa nia ya serikali ya awamu ya tano ni kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata maji safi na salama, hivyo hawana budi kuwa na tabia ya kutunza vyanzo hivyo kwa manufaa ya jamii.

Majaliwa alisema hayo leo wakati alipokuwa akifungua mradi wa maji wa vijiji vya Mkongotema na Magingo wilaya ya Songea vijijini mkoani Ruvuma, ambao ujenzi wake umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 1.9 na wenye uwezo wa kuhudumia wakazi 5,300 wanaoishi katika maeneo hayo.

SERIKALI KUJENGA KITUO CHA KUPOOZEA UMEME MAKAMBAKO HADI SONGEA

Na Kassian Nyandindi,       
Songea.

SERIKALI hapa nchini imesema kwamba inatarajia kujenga kituo cha kupoozea umeme gridi ya taifa kutoka Makambako mkoa wa Njombe hadi Songea mkoani Ruvuma, ambao utasafirishwa kwa lengo la kuondoa adha ya upatikanaji wa nishati hiyo muhimu katika mji wa Songea.

Kadhalika imeelezwa kuwa serikali imekuwa ikitambua kuwa upatikanaji wa umeme katika mkoa wa Ruvuma, umekuwa ni hafifu hivyo ili dhamira ya serikali ya uanzishwaji wa viwanda vidogo vidogo na vile vikubwa iweze kutimia ni lazima kuwepo na nishati ya umeme wa uhakika.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alisema hayo leo alipokuwa akizungumza na wananchi wa wilaya ya Songea vijijini huku akisisitiza kuwa umeme huo utasambazwa pia katika maeneo mbalimbali mkoani Ruvuma, kwa lengo la kuboresha na kuinua zaidi hali ya uchumi ya mkoa huo.

NFRA KANDA YA SONGEA YATAKIWA MAHINDI ILIYONUNUA KUYATUNZA VIZURI

Meneja wa wakala wa taifa wa hifadhi ya chakula NFRA Kanda ya Songea Majuto Chabuluma wa kwanza kushoto akimuonesha Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kiasi kidogo cha mahindi kilichonunuliwa na NFRA, ambayo msimu huu imeshindwa kufikia malengo ya  kununua tani 22,000 badala yake imenunua tani 10,335.256 tu, kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge.
Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

WAKALA wa Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) Kanda ya Songea mkoani Ruvuma, ametakiwa kuhakikisha kwamba mahindi yote yaliyonunuliwa yanatunzwa vizuri kwa umakini mkubwa, hayaharibiki katika maghala ya kuhifadhia chakula ili yaweze kusaidia pale itakapotokea tatizo la njaa hapa nchini.

Agizo hilo limetolewa jana na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa alipokuwa ametembelea kituo cha hifadhi hiyo kilichopo katika Manispaa ya Songea mjini hapa.

“Hakikisheni mahindi haya yanatunzwa vizuri ili yasiweze kuharibika, yasije yakatokea kama msimu uliopita mwaka jana mahindi mengi yaliharibika hivyo serikali hatutaki kuona tena mwaka huu tatizo hili linajirudia”, alisisitiza Majaliwa.

Alifafanua kuwa serikali kupitia kitengo chake cha kuhifadhi chakula kila mwaka kipo kwa ajili ya kununua kiasi kidogo cha ziada ya chakula na sio vinginevyo, ikiwa ni lengo la kuweka tahadhari pale yanapotokea matatizo ya njaa.

WAFANYAKAZI WA KAMPUNI WADAIWA KUTAPELI WANANCHI TANESCO YATOA TAHADHARI KWA WATEJA WAKE

Na Mwandishi wetu,        
Songea.

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) mkoani Ruvuma, limewatahadharisha Wananchi wa mkoa huo hususan kwa wale wanaoishi vijijini kuwa makini na watu wanaotumia jina la shirika hilo, kuwatapeli fedha kwa kisingizio cha kuwaingizia umeme majumbani mwao kupitia Mpango wa Umeme Vijijini (REA) katika awamu hii ya tatu.

Aidha limewataka kuwa na mazoea ya kutoa taarifa kwa shirika hilo pale wanapoona kuna watu wanaokwenda kwenye maeneo yao, kwa kujifanya  maofisa wa TANESCO na kuanza kuchangisha fedha kwa kuwa wenye mamlaka ya kufanya hivyo ni shirika hilo na sio vinginevyo.

Hatua hiyo inafuatia tukio la hivi karibuni la maofisa wa shirika hilo kikosi cha usalama kwa kushirikiana na wananchi kuwatia mbaroni vijana wanne wa Kampuni ya Syba Electrical Service and General Enterprises inayofanya kazi ya ukandarasi wa umeme, yenye makao makuu yake mkoani Mwanza baada ya vijana hao kujitambulisha kama maofisa wa TANESCO wakiwa tayari wamekusanya zaidi ya shilingi 700,000 kutoka kwa wakazi wa kijiji cha Mbinga Mhalule wilayani Songea mkoani hapa.

Wednesday, January 4, 2017

WAZIRI MKUU AWATAKA VIONGOZI KUCHUKUA HATUA DHIDI YA WATOTO WASIOPELEKWA SHULE

Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Ruvuma, Mhashamu Raphael Reuben Haulle akisalimiana na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo katika uwanja wa ndege Songea mjini mkoani hapa, mara baada ya Waziri huyo kuwasili tayari kwa kuanza ziara ya siku tano ambapo atapata fursa ya kukagua na kuhimiza shughuli za maendeleo pamoja na kuongea na wananchi pamoja na watumishi wa serikali wa mkoa huo
Na Kassian Nyandindi,       
Songea.

VIONGOZI wa serikali mkoani Ruvuma, wameagizwa wahakikishe kwamba watoto wote walioandikishwa kuanza elimu ya awali, msingi na sekondari kwa mwaka huu wa masomo wanakuwepo shuleni mara shule zitakapofunguliwa Januari 9 mwaka huu.

Kadhalika wanapaswa kuchukua hatua dhidi ya watoto wenye umri wa kwenda shule ambao hivi sasa, wamekuwa wakishinda kwenye vituo vya mabasi (Magari ya abiria) ili waweze kwenda shule na kuweza kumaliza kabisa tatizo la utoro katika mkoa huo.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, ametoa agizo hilo leo akiwa mkoani Ruvuma katika ziara yake ya siku nne mara baada ya kupokea taarifa ya maendeleo ya mkoa iliyosomwa na Mkuu wa mkoa huo, Dkt. Binilith Mahenge Ikulu ndogo mjini Songea.

Amewaonya Wakurugenzi wa halmashauri za wilaya na miji hapa nchini kutekeleza kwa kusimamia kikamilifu mpango wa utoaji wa elimu bure kwa shule za serikali, ambao unatoa nafasi kwa vijana wengi zaidi kupata fursa ya kusoma kwani serikali imeshaondoa gharama zote ambazo zilikuwa kikwazo kwa baadhi ya familia.

Pamoja na agizo hilo Waziri Mkuu, Majaliwa ameagiza  pia jamii kushiriki kikamilifu katika utunzaji wa mazingira kwenye maeneo yao ili waweze kuepuka hatari ya kutokea ukame hasa ukizingatia kuwa mkoa wa Ruvuma, unafaa kwa shughuli za kilimo na ni moja kati ya mikoa inayopata mvua za kutosha mwaka hadi mwaka.

MAJALIWA APONGEZA KUKUA KWA PATO LA MWANANCHI WA KAWAIDA RUVUMA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akipunga mkono leo katika uwanja wa ndege Songea mjini mara baada ya kuwasili kwa ajili ya kuanza ziara ya kikazi ya siku tano mkoani Ruvuma, kulia ni mkewe mama Mary Majaliwa, kulia kwake ni Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge na Mkuu wa wilaya ya Songea Palolet Mgema.
Na Kassian Nyandindi,           
Songea.

PATO la Mwananchi wa kawaida hapa nchini (Percapital income) katika mkoa wa Ruvuma limepanda kutoka shilingi milioni 2,082,167 mwaka juzi hadi kufikia shilingi milioni 2,415,485 kwa mwaka 2016, hatua ambayo imeufanya mkoa huo kushika nafasi ya tatu kitaifa ikitanguliwa na mikoa ya Dar es Salaam na Iringa.

Aidha pato hilo linaonesha kwamba ni ongezeko la asilimia 16 ikilinganishwa na pato la mtu mmoja kwa mwaka 2014  ambapo ongezeko hilo limetokana na shughuli ya kiuchumi kama vile kilimo ambacho hutegemea kwa kiasi kikubwa wakazi wa mkoa huo kuendeshea maisha yao.

Hayo yalisemwa leo na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge alipokuwa akitoa taarifa ya maendeleo ya mkoa huo kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Ikulu ndogo mjini Songea.

Dkt. Mahenge alisema kuwa wananchi wake hutegemea shughuli hizo kiuchumi ambapo zaidi ya asilimia 87 ya wakazi wake, hupata riziki yao kutokana na shughuli hiyo ambayo huchangia pia pato la taifa kwa asilimia 3.3 kwa mwaka, huku pato la mkoa likifikia wastani wa asilimia 75.

WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA AWASILI MKOANI RUVUMA ASISITIZA SERIKALI KUENDELEA KUNUNUA MAZAO YA WAKULIMA VIJIJINI

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge mara baada ya kuwasili leo katika uwanja wa ndege Songea mkoani hapa kwa ziara ya kikazi, kulia kwake ni mke wa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Mama Mahenge.
Na Mwandishi wetu,           
Songea.

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema kwamba, serikali kupitia Wakala wake wa Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) itaendelea kununua mazao ya wakulima moja kwa moja vijijini, ili waweze kunufaika na bei elekezi ambayo imekuwa ikitolewa na serikali.

Majaliwa alisema hayo leo mara baada ya kupokea taarifa ya maendeleo ya mkoa wa Ruvuma, Ikulu ndogo mjini hapa ambapo yupo mkoani humo kwa ziara ya kikazi ya siku tano hadi Januari 8 mwaka huu.

Alisema kuwa pamoja na serikali kutoa bei elekezi ya ununuzi wa mazao ya wakulima ambao ndio hasa wavuja jasho walikuwa hawanufaiki na bei hiyo nzuri, badala yake wafanyabiashara walanguzi ndio waliokuwa wakitajirika jambo ambalo kamwe haliwezi kupewa nafasi tena kwa sasa.

“Wananchi wanapaswa kuelekezwa juu ya umuhimu wa kutunza chakula walichokwishazalisha msimu uliopita, kutokana na uwepo wa kiwango cha mvua kisichoridhisha mwaka huu na maofisa kilimo katika halmashauri wawaelimishe wakulima hawa, namna ya kujikita zaidi katika uzalishaji wa mazao yanayostahimili ukame ili kukabiliana na uwezekano wa kutokea kwa njaa msimu ujao”, alisema Majaliwa.

WANANCHI WALALAMIKIA UJENZI WA BARABARA

Na Kassian Nyandindi,         
Nyasa.

BAADHI ya Wananchi wanaoishi katika wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma wamelalamikia ujenzi wa barabara ya kutoka Mbinga mjini hadi Mbamba bay wilayani humo, iliyopo chini ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kwa kutofuatilia kwa karibu ujenzi unaoendelea sasa, hali ambayo inasababisha barabara hiyo kufanyiwa matengenezo ya mara kwa mara.

Aidha walisema kuwa wanashangaa kuona ikifanyiwa matengenezo kwa mara ya pili na mkandarasi mwingine, wakati ni miezi michache tu imepita kulikuwa na mkandarasi ambaye alikuwa akiitengeneza.

Wameiomba serikali kupitia Wakala huyo wa TANROADS kuwabana wakandarasi wazembe wanaopewa kazi ya kujenga barabara wilayani hapa, ili kuepuka barabara hizo kufanyiwa matengenezo ya mara kwa mara jambo ambalo linaisababishia serikali hasara kubwa juu ya upotevu wa fedha za wananchi.

Tuesday, January 3, 2017

WAZIRI MKUU KUANZA ZIARA YAKE YA KIKAZI KESHO MKOANI RUVUMA

Na Mwandishi wetu,      
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa kesho anatarajia kuanza ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani Ruvuma ambapo atapata fursa ya kutembelea na kukagua shughuli za maendeleo ya wananchi, katika wilaya ya Mbinga na Songea mkoani hapa.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mkuu wa mkoa huo, Dkt. Binilith Mahenge alisema kwamba Majaliwa atawasili katika uwanja wa ndege Songea majira ya saa 9.00 alasiri na kupokelewa na viongozi wa serikali na chama.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Aliwataka wananchi wote kwenye maeneo ambayo Waziri huyo atafanya mikutano, wahudhurie kwa wingi ili kumsikiliza na hatimaye kutekeleza maagizo yake ambayo atayatoa kwa viongozi, watendaji na wananchi kupitia mikutano hiyo.

Dkt. Mahenge alisema kuwa mara baada ya kuwasili ataelekea Ikulu ndogo iliyopo mjini hapa, ambako atapokea taarifa ya maendeleo ya mkoa na kwamba baada ya hapo atazungumza na watumishi wa umma.

Alisema kuwa Januari 5 mwaka huu Waziri mkuu atatembelea katika halmashauri ya Songea vijijini Madaba ambapo atazungumza pia na watumishi wa serikali, kukagua na kuzindua mradi wa maji katika kijiji cha Magingo na baadaye atahutubia mkutano wa hadhara wananchi wa Madaba.

ASKOFU MKUU WA JIMBO KUU LA SONGEA AWATAKA VIONGOZI KUTUMIA HEKIMA NA BUSARA KATIKA KULIONGOZA TAIFA

Na Kassian Nyandindi,    
Songea.

ASKOFU Mkuu wa Kanisa katoliki Jimbo kuu la Songea mkoani Ruvuma, Damian Dallu amewataka viongozi hapa nchini kutumia hekima na busara katika kuliongoza taifa, kwa lengo la kuwatendea haki wananchi wanaowaongoza kwa ajili ya kudumisha amani na mshikamano.

Dallu aliyasema hayo juzi alipokuwa akihubiri katika ibada ya misa takatifu ya mkesha wa kuuaga mwaka 2016 na kuukaribisha mwaka mpya wa 2017 iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la kiaskofu la mtakatifu Mathias Kalemba mjini Songea.

Askofu Mkuu wa Jimbo kuu la Songea, Damian Dallu.
Alisema kuwa baadhi ya mataifa yameingia katika machafuko kutokana na viongozi wake kushindwa kutumia hekima na busara, katika kutatua changamoto na migogoro mbalimbali inayowakabili wananchi wake wanaowaongoza.

Kadhalika Askofu huyo amewataka viongozi hao kutumia mwaka mpya wa 2017 katika kutatua changamoto mbalimbali zinazolikabili taifa hili, ikiwemo migogoro ya mapigano baina ya wakulima na wafugaji ambayo inasababisha umwagaji wa damu katika baadhi ya maeneo pale inapotokea.

Monday, January 2, 2017

TAMASHA LA UZINDUZI VIVUTIO VYA UTALII NYASA LAFANA WADAU WASHAURIWA KUWEKEZA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge akizungumza na wananchi, watendaji wa serikali na wageni kutoka nje ya mkoa huo (hawapo pichani) walipofika kwenye uzinduzi wa tamasha la kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo katika wilaya ya Nyasa mkoani hapa, upande wa kulia ni Mkuu wa wilaya hiyo Esabela Chilumba na kushoto Mbunge wa Jimbo la Nyasa, Stella Manyanya ambaye pia ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Injinia Stella Manyanya.
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge katikati akikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa tamasha la kutangaza vivutio vya utalii katika wilaya ya Nyasa mkoani humo, upande wa kulia Mkuu wa wilaya ya Mbinga Cosmas Nshenye wa pili yake ni Mkuu wa wilaya ya Nyasa, Esabela Chilumba na kushoto ni Mbunge wa jimbo la Nyasa, Injinia Stella Manyanya.
Na Kassian Nyandindi,         
Nyasa.

TIMU ya viongozi wa serikali mkoa wa Ruvuma imewasili wilaya ya Nyasa mkoani humo kwa lengo la kushiriki tamasha la uzinduzi wa fursa za utalii huku serikali ikiwataka wadau kutoka maeneo mbalimbali ya ndani na nje ya mkoa huo kuwekeza wilayani humo kwenye shughuli za uvuvi, ujenzi wa hoteli za kisasa pamoja na viwanda vidogo vidogo.

Aidha imeelezwa kuwa ujenzi wa viwanda hivyo utasaidia kuifanya wilaya hiyo ipige haraka hatua mbele za kimaendeleo katika kuongeza thamani ya mazao yanayozalishwa, kukuza uchumi na kuleta ajira kwa vijana.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge alisema hayo juzi alipokuwa mgeni rasmi kwenye tamasha la uzinduzi wa fursa za utalii na kuinua uchumi wilayani Nyasa lililofanyika katika kituo cha udhibiti wa rasilimali za uvuvi wilayani humo.

Sunday, January 1, 2017

WATU 21,000 WABAINIKA KUISHI NA VIRUSI VYA UKIMWI SONGEA

Na Mwandishi wetu,       
Songea.

ZAIDI ya watu 21,000 katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wamebainika kuishi na Virusi Vya Ukimwi (VVU) hivyo wananchi wamesisitizwa kutunza afya zao ili kuweza kuepukana na maambukizi mapya ya ugonjwa wa Ukimwi, utakanao na virusi hivyo.  

Ofisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo alisema kuwa takwimu hizo zimetolewa na kitengo cha uratibu wa Ukimwi na tiba katika Manispaa ya Songea ambapo inaonesha kuwa kati ya watu wenye virusi hivyo, zaidi ya 10,000 ndiyo ambao wanaugua ugonjwa wa Ukimwi.

Alisema kuwa idadi hiyo ni wale wanaotumia dawa za kurefusha maisha (ARV) na kwamba maambukizi ya virusi hivyo yamefikia asilimia nne.

Midelo amezitaja kata ambazo zinaongoza kwa maambukizo ya ugonjwa huo katika Manispaa ya Songea kuwa ni Bombambili, Mateka, Ruvuma na Lilambo.

CCM YAPANIA KUCHUKUA USHINDI UCHAGUZI MDOGO KATA YA MAGUU MBINGA

Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Ruvuma kimewataka wananchi wa kata ya Maguu wilayani Mbinga mkoani hapa, kumchagua mgombea anayetokana na chama hicho katika uchaguzi wa nafasi ya udiwani unaotarajiwa kufanyika Januari 22 mwa huu.

Akizungumza juzi na wananchi wa kata hiyo katika uzinduzi wa kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani zilizofanyika katika viwanja vya michezo mji mdogo wa Maguu Mwenyekiti wa CCM wa mkoa hu, Oddo Mwisho alisema kuwa wanachama na wananchi kwa ujumla wake wanapaswa kukiamini chama hicho kwa kuwa ndicho pekee chenye nia ya dhati ya kuwaletea maendeleo wananchi wake.

Mwisho alisema kata hiyo ilikuwa mikononi mwa CCM hivyo wananchi wanakila  sababu ya kuendelea kukiamini na kwamba vyama vya upinzani havipaswi kupewa kuongoza kata hiyo kutokana na kukosa historia ya kuwatumikia wananchi ipasavyo katika kuwaletea maendeleo kwenye maeneo yao wanayoishi.


“Ndugu zangu wananchi kumbukeni jinsi ambavyo majimbo na kata ambazo vyama vya upinzani wamepata nafasi ya kuongoza wameshindwa kuwaletea maendeleo, kila kukicha wao kazi yao kubwa ni kuhamasisha maandamano ya kupinga mambo ambayo yanatekelezwa na serikali ya chama tawala”, alisema.

MANISPAA SONGEA YATOA MKOPO MILIONI 72.5 KWA VIKUNDI VYA UJASIRIAMALI

Tina Sekambo Mkurugenzi Manispaa ya Songea.
Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imetoa mkopo wa shilingi milioni 72.5 ambazo zimetokana na mapato yake ya ndani kwenda katika vikundi vya wanawake na vijana ili waweze kujikomboa kiuchumi.

Mkopo huo umetolewa katika kipindi cha mwaka jana kwa awamu mbili ambapo katika awamu ya kwanza jumla ya shilingi milioni 52.5 zilikopeshwa kwenye vikundi hivyo.

Aidha kati ya fedha hizo vikundi 73 vya wanawake vilikopeshwa zaidi ya shilingi milioni 36 na vikundi 35 vya vijana vilikopeshwa shilingi milioni 16.

WAKULIMA NAMTUMBO WALALAMIKIA KUCHELEWA KWA PEMBEJEO ZA KILIMO

Na Yeremias Ngerangera,          
Namtumbo.

MGOMO wa wakulima wanaozalisha mazao ya aina mbalimbali katika kijiji  cha Namabengo  wilayani  Namtumbo  mkoa wa Ruvuma, umepatiwa ufumbuzi na Mkuu wa wilaya hiyo Luckness Amlima baada ya kwenda kijijini hapo kusikiliza madai yao na kuyapatia majawabu.

Madai hayo yaliyopatiwa ufumbuzi yalikuwa pamoja na wakulima hao kukataa kununua mbegu za ruzuku ya serikali kwa madai kuwa mbegu hizo, zimechelewa kuwafikia ambapo wananchi katika msimu wa mwaka huu tayari wamepanda katika mashamba yao kwa kutumia mbegu za asili walizokuwa nazo.

Vilevile baada ya kufikia muafaka juu ya jambo hilo, wakulima waliachiwa baadhi ya mbegu pamoja na mbolea za kukuzia huku wakiitaka serikali msimu ujao kupeleka pembejeo mapema ili isiweze kutokea tena hali kama hiyo.