Na Muhidin Amri,
Songea.
KAMPUNI ya Kambas Group of Companies,
inayofanya utafiti wa makaa ya mawe katika kitongoji cha Mipeta na Manyamba
kata ya Muhukuru Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, imetoa msaada
wa mifuko ya saruji 150 na bati 100 kwa ajili ya ukarabati wa vyumba vinne vya
madarasa, nyumba mbili za walimu na ofisi ya shule ya msingi Mipeta iliyopo
wilayani humo.
Mwanzoni mwa mwezi huu upepo mkali ulioambatana
na mvua uliezua paa katika baadhi ya madarasa, ofisi za walimu pamoja na nyumba
mbili za walimu hali iliyosababisha wanafunzi kuanzia darasa la kwa kwanza hadi
sita kulazimika kusomea vyumba viwili vya madarasa huku walimu walioezuliwa
nyumba zao za kuishi wakiomba hifadhi ya kulala kwa walimu wenzao na wenyeji wa
kitongoji hicho.
Akikabidhi msaada huo jana kwa Mkuu
wa wilaya ya Songea, Palolet Mgema Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Yahaya Yusuph alisema
wameamua kutoa vifaa hivyo vya ujenzi ikiwa ni mkakati wa kampuni yake kuunga
mkono mpango wa Serikali ya Rais Dokta John Pombe Magufuli ya kutoa elimu bure,
hivyo yeye kama mdau wa maendeleo ameona ni vyema kuchangia vifaa hivyo ili
watoto hao waweze kuendelea na masomo katika mazingira mazuri.




































