Wednesday, October 31, 2012

WANAOBEZA YALIYOFANYWA NA MWALIMU NYERERE WAPUUZWE

















 Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. (Picha na mtandao)



Na Dustan Ndunguru,


Songea.


PADRE wa kanisa la Roman Katoliki Bw. John Chacha  ambaye pia ni makamu mkuu wa chuo kikuu cha SAUT tawi la Songea  mkoani, ameshangazwa na baadhi ya watu ambao wanaobeza kazi  zilizofanywa na hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kwa kusema hazikuwa na tija katika Taifa hili.

Kauli hiyo aliitoa wakati wa mahubiri ya ibada ya jumapili ambayo ilikuwa ni siku ya watakatifu waliyoishi kwa uadilifu kwa kumcha Mungu, pamoja na utii mbele ya jamii ambayo iliyokuwa ikiwazunguka.

Akihubiri katika kanisa la mtakatifu Mathias Mlumba Kalemba jimbo kuu la Songea Padre Chacha alisema, kumekuwa na tabia iliyozoeleka kwa baadhi ya watu kubeza kazi zilizofanywa na waasisi wa nchi ambao walikuwa wanajituma usiku kucha kuhakikisha taifa  linakwenda sawa bila upendeleo.
               
“Ninashangazwa  sana kuona baadhi ya watu wamekuwa wakibeza kazi zilizofanywa na mwalimu Nyerere, pamoja na wenzake na kusema kuwa suala la ufisadi  lilikuwepo tangu enzi za mwalimu jambo ambalo ni ukosefu wa fikra za kichambuzi na uwiano wa kihistoria”
  
“Kwa kumbukumbu yangu mwalimu Nyerere aliwahi kugoma kujengewa nyumba akasema kwa vile napenda kusoma vitabu na maktaba yangu imechakaa naomba mnitengenezee, ili vitabu vyangu vikae sehemu nzuri, lakini kwa mtanzania wa sasa akiambiwa hivyo tu ndio wa kwanza kufuatilia ahadi hiyo bila hata kuwa na uwoga wowote”, alisema Padre huyo.


Alisema watanzania wa sasa wanatakiwa kufuata mambo mazuri yaliyofanywa na mwalimu ambapo kwa kufanya hivyo kila mtu atakuwa na uchungu na nchi yake na kuondokana na ubinafsi ambao unaonekana kutawala kila mahali.

Padre Chacha alisema kila kiongozi wa chama cha siasa na wanachama wake kwa ujumla, wanapaswa kujifunza kwa dhati yale ambayo yalionyeshwa na waasisi na kwamba waache chokochoko ambazo siku zote zinaonesha kutaka kuharibu amani na utulivu uliodumu kwa miaka mingi sasa.
                                             
               

No comments: