Friday, September 19, 2014

JESHI LA POLISI NCHINI LANYOSHEWA KIDOLE LATAKIWA KUACHA KUNYANYASA WAANDISHI WA HABARI

Rais Jakaya Kikwete wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

















Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

JESHI la Polisi nchini limetakiwa kuacha vitendo vya  kuwanyanyasa waandishi wa habari na kuwafanya wasitekeleze wajibu wao ipasavyo, kufanya hivyo ni kutowatendea haki na kudhalilisha taaluma ya habari.

Sambamba na hilo Jeshi hilo limenyoshewa kidole kwamba limekuwa na historia ya kupiga na kuwafukuza waandishi wa habari, hasa pale wanapotafuta ukweli juu ya matukio mbalimbali ambayo yamekuwa yakitokea miongoni mwa jamii.

Rai hiyo imetolewa na baadhi ya Wananchi wa mkoa wa Ruvuma, walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti kufuatia tukio lililotokea jana makao makuu ya jeshi hilo baada ya waandishi kupigwa, kukimbizwa na mbwa ili wasichukue taarifa za kuhojiwa kwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe.


Walisema tukio la kupigwa na kudhalilishwa kwa waandishi wa habari ni ishara tosha ya polisi waliofanya kitendo hicho kutoheshimu taaluma ya habari, huku wakivitaka vyombo mbalimbali vya kutetea haki za binadamu kuchukua hatua za kisheria dhidi ya askari polisi waliofanya kitendo hicho.

Richard Haulle mkazi wa Mpandangindo wilaya ya Songea vijijini mkoani humo, alisema Waandishi wa habari ni mhimili pekee ambao unategemewa hapa duniani kwa kutoa taarifa mbalimbali, juu ya nini kinachoendelea katika ulimwengu wa sasa hivyo jamii inapaswa kuendelea kuwaheshimu hasa pale wanapokuwa wakitimiza majukumu yao ya kazi za kila siku.

Alieleza kuwa Tanzania ni nchi yenye amani, hivyo kufikia hatua ya muendelezo wa kupiga waandishi ni kujenga tabaka la kuharibu amani tuliyonayo kama alivyosema hivi karibuni Makamu wa Rais Dokta Mohamed Gharib Bilal, kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama nchini kushirikiana na waandishi wa habari katika kufanya kazi kwa ajili ya kulinda amani ya nchi.

David Ndunguru mkazi wa kata ya Litembo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma alisema,  “ni kitendo cha ajabu sana kuona polisi wanawapiga mabomu ya machozi waandishi, wanawafukuzwa na mbwa utafikiri kama ni wahalifu ni vizuri sasa hata kama kuna amri inatoka kwa kiongozi wa juu wajirekebishe huu sio utawala bora”.

Ndunguru alisema kuwa Paul Chagonja ambaye ni Kamishna wa Operesheni na Mafunzo anapaswa kushushiwa lawama nzito, kutokana na muda mwingi alikuwa akionekana akiwaagiza askari wake wawaondoe waandishi wasitekeleze majukumu yao na hata kuwasakizia mbwa.

Kadhalika Hashimu Rashid mkazi wa Songea mjini naye alilaani juu ya vitendo hivyo, ambapo alifafanua kuwa hali hiyo ni kuminya uhuru wa utendaji kazi wa waandishi katika kuuhabarisha umma wa watanzania juu ya mambo yaliyokuwa yakitokea.

“Jeshi la Polisi limekuwa na kawaida ya kuwanyanyasa, kuwapiga na hata kuwaua waandishi wa habari pale wanapotekeleza wajibu wao wa kukusanya habari, ni vizuri sasa serikali yetu ijirekebishe ione inakosea wapi”, alisema Rashid.

Hata hivyo ukatili wa askari wa jeshi hilo kwa waandishi wa habari inakumbukwa zaidi pale walipofanya mauaji ya Mwandishi wa kituo cha Televisheni ya Chanel ten mkoani Iringa, Daud Mwangosi yaliyotokea Septemba 2 mwaka juzi, katika kijiji cha Nyololo Mufindi mkoani humo wakati mwandishi huyo akiwajibika katika majukumu yake ya kazi za kila siku.


No comments: