Tuesday, September 9, 2014

MKUU WA WILAYA MBINGA AWA MBOGO, AWASHUKIA WAFANYABIASHARA WA KAHAWA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amewashukia wafanyabishara wenye tabia ya kutorosha kahawa wilayani humo kwa lengo la kukwepa kulipa ushuru na kuwataka kuacha tabia hiyo mara moja, na atakaye endelea kufanya hivyo pale atakapobainika atachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo kunyang’anywa kibali cha ununuzi wa zao hilo wilayani humo.

Alitoa onyo hilo wakati alipokuwa akifunga kikao cha wadau wa kahawa kanda ya Ruvuma, kilichofanyika katika ukumbi wa Jimbo Katoliki mjini hapa.


Ngaga alisema haiwezekani kwa watu wachache hupenda kujinufaisha wao pekee kwa njia zisizo halali kwa kutotaka kufuata taratibu zilizowekwa, ambapo dhamira ya serikali ni kuona wananchi wake wananufaika kwa pamoja hivyo wilaya itaendelea kusimamia hilo kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba hakuna mtu anayeweza kuhujumu biashara ya zao hilo.

Alifafanua kuwa usambazaji wa mitambo ya kukoboa kahawa mbivu itaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali yanayozalisha kahawa wilayani Mbinga, ikiwa ni lengo la kuona wakulima wanafanikiwa kuzalisha kahawa yenye ubora na ambayo itapata bei nzuri sokoni.

Alisema kila mfanyabiashara anapaswa kufuata taratibu zilizowekwa katika ununuzi wa kahawa kutoka kwa wakulima, ikiwemo matumizi ya vipimo sahihi ambavyo haviwaibii wakulima.

Katika hatua nyingine mkuu huyo wa wilaya, aliwataka wakulima na wafanyabiashara kuacha tabia ya kuanika kahawa chini badala yake watumie vichanja ili kuweza kutunza ubora wake usiharibike.

No comments: