Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
BAADHI ya wananchi wanaoishi katika kijiji cha Ntunduaro kata
ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamempongeza Mkurugenzi mtendaji wa
Halmashauri ya wilaya hiyo Venance Mwamengo kwa kuchukua hatua ya kufunga
mashine ya kukusanyia ushuru katika eneo la Amani Makolo, ambalo husafirishwa
mkaa wa mawe kwenda nje ya wilaya hiyo kitendo ambacho kwa kiasi kikubwa
kimesaidia kudhibiti mapato ya fedha yatokanayo na mkaa huo.
 |
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa. |
Walisema kuwa hapo awali kabla ya kufungwa kwa mashine hiyo
ya Electronic (EFD’S) mapato mengi yalikuwa yakipotea kutokana na kukusanywa
kwa njia ya vitabu vya risiti, ambapo watendaji waliokuwa wakipewa dhamana ya
ukusanyaji wa fedha hizo za ushuru walikuwa hawawajibiki ipasavyo.
Theodosia Mahundi mkazi wa kijiji hicho aliwaeleza waandishi
wa habari kuwa udhibiti huo wa mapato unapaswa kufanywa kwa kutumia mashine
hiyo, katika kila eneo ambalo serikali inakusanya mapato ili kuweza kudhibiti
mianya ya wajanja wachache, ambao wamekuwa wakitafuta njia za ufujaji wa fedha
za serikali.
Mahundi alisema kuwa ni faraja kwao kuona mapato hayo jinsi
yanavyodhibitiwa na kwamba wanaimani kuwa hata serikali, itaweza kuwahudumia
wananchi wake kwa kuwapelekea huduma muhimu kama vile madawa kwenye zahanati na
vituo vya afya kwa wakati.
Naye Renatus Mapunda mkazi wa kijiji cha Amani Makolo kata ya
Amani Makolo alisema kuwa hapo awali madereva wengi wanaosafirisha mkaa wa mawe
kwenda nje ya wilaya hiyo, ameshuhudia wakiwa wanakwepa kulipa ushuru huo
ambapo alitoa ushauri kwa kuitaka serikali kuendelea kuongeza nguvu ya udhibiti
wa mapato yatokanayo na mkaa huo, ili jamii iweze kunufaika nayo kwa njia ya
kuwaletea maendeleo katika nyanja mbalimbali.