Tuesday, August 27, 2013

MSHAURI WA ZAO LA KAHAWA MBINGA ADAIWA KUHUSIKA NA UTOROSHAJI WA ZAO LA KAHAWA KWA LENGO LA KUKWEPA KULIPA USHURU

Mkuu wa Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma,  Senyi Ngaga.














Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KIGOGO mmoja wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, anadaiwa kuhusika katika vitendo vinavyofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wa zao la kahawa wilayani humo, la utoroshaji wa  zao hilo kwa lengo la kukwepa kulipa ushuru jambo ambalo linasababisha halmashauri hiyo kukosa mapato.

Wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti mjini hapa, wafanyabiashara hao walitoboa siri hiyo kwa kumtaja jina kuwa ni, Mshauri wa zao la kahawa wilayani humo Gotham Haulle ambaye ni mmoja kati ya maofisa kilimo amekuwa akijihusisha na biashara ya ununuzi wa kahawa vijijini kwa kuwatumia wafanyabiashara wajanja ambao huwarubuni wakulima kwa kununua zao hilo kwa bei ya chini.

Aidha walisema tukio la kukamatwa kwa mfanyabiashara Madawa Mwaijande la utoroshaji wa kahawa kavu tani 10 yenye thamani ya shilingi milioni 28 Agosti 21 mwaka huu majira ya usiku katika kijiji cha Kitai, Haulle anahusishwa katika tukio hilo kwa kile kinachodaiwa kuwa ofisa kilimo huyo amekuwa akishirikiana kufanya biashara hiyo na mfanyabiashara huyo.

Mfanyabiashara huyo alikamatwa akitorosha kahawa hiyo kuelekea Jijini Mbeya kwa lengo la kukwepa kulipa ushuru akiwa na gari lenye namba za usajili T 856 CFL mali ya Medson Ulendo mkazi wa mjini hapa.

Vilevile baadhi vigogo wa halmashauri hiyo ambao majina yao hawakutaka yatajwe katika mtandao huu, wamemnyoshea kidole mtumishi mwenzao wakisema, muda mwingi amekuwa hakai ofisini kutokana na kukabiliwa na shughuli ya biashara hiyo ya kahawa badala ya kutekeleza majukumu yake ya msingi aliyopewa na serikali.

“Hii kahawa tuliyoikamata juzi tumefanya utafiti na kubaini kwamba huyu mfanyakazi mwenzetu anahusika kwa kiasi kikubwa na biashara hii, lakini tupo katika hatua ya kuchukua maamuzi sahihi ambayo yatasaidia kudhibiti vitendo hivi viovu vinavyolenga kuikosesha halmashauri mapato yake”, alisema mmoja kati ya vigogo wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga.

Pamoja na mambo mengine Waandishi wa habari walipofanya mahojiano na Mshauri huyo wa zao la kahawa wilaya ya Mbinga Gotham Haulle juu ya kuhusishwa na tuhuma za kushirikiana na wafanyabiashara kutorosha kahawa kwa lengo la kukwepa kulipa ushuru huo, alikana huku akisema yeye anazobiashara zake zingine ambazo huzifanya na kumuingizia kipato.

“Mimi kwa kifupi nina hela nyingi sana, haya maneno yanayozungumzwa ni kutaka kumchafua mtu tu, na hii ni kawaida kwa vijana wahuni  wakitaka kumharibia mtu lazima wamhusishe na matukio maovu”, alisema Haulle.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo Hussein Issa Ngaga alipoulizwa na waandishi wa habari alithibisha kuwepo kwa tukio hilo na kusema, anazotaarifa kuwa baadhi ya watumishi wake wamekuwa wakijihusha na biashara ya ununuzi wa kahawa huku wakishirikiana na wafanyabiashara wengine wilayani humo kuhujumu mapato ya halmashauri hiyo.

Ngaga alisema katika kukabiliana na hali hiyo tayari kuna kamati husika imeundwa ambayo hufanya kazi ya kufuatilia vitendo hivyo viovu na wale watakaobainika, watachukuliwa hatua stahiki za kisheria na kwamba alikemea kitendo cha watendaji kuacha shughuli za kiutumishi na kupoteza muda mwingi kufanya shughuli zao binafsi, huku kazi za utumishi wa umma walizoajiriwa nazo zikiendelea kuzorota.


No comments: