Tuesday, August 13, 2013

WATANZANIA WAASWA KUWAJALI WENYE MAHITAJI MAALUM

Na Anna Nkinda – Maelezo
 
Watanzania wametakiwa kujenga tabia ya kuwajali watu wenye mahitaji maalum ikiwa ni pamoja na watoto yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi ili nao wajione kana kwamba wana wazazi ingawa baadhi yao wamefiwa na wazazi wao.
 
Wito huo umetolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Montage Tanzania Teddy Mapunda  wakati wa sherehe za sikuku ya Eid Mubarak zilizofanyika katika Shule ya Sekondari ya watoto wa kike  ambao ni yatima na wanaoishi  katika mazingira hatarishi ya WAMA-Nakayama iliyopo kijiji cha Nyamisati wilaya ya Rufiji mkoani Pwani.
 
Mapunda alisema ingawa watoto hao hawana wazazi lakini kama jamii itawajali na kuwaonyesha upendo hawatahisi tofauti ya kutokuwepo kwa wazazi wao kwani kutakuwa na watu wanaowajali kama vile wazazi wao wako hai.
 
Mkurugenzi huyo pia aliipongeza shule hiyo kwa kuzisaidia shule za  jirani za Sekondari za  Mahege na Nyamisati ingawa nao wanapata msaada kutoka kwa wafadhili kwa kuimarisha miundombinu ikiwa ni pamoja na kujenga majengo, kutoa vitabu, kuweka umeme wa jua na kuwapatia walimu wa mazoezi ambao wakimaliza vipindi vya kufundisha katika shule ya WAMA-Nakayama wanaenda kufundisha katika shule hizo.
 
Naye  Kaimu Mkuu wa Shule hiyo Mwalimu Suma Mensah  alisema kuwa  shule yake inawanafunzi  322 wa kidato cha kwanza hadi cha nne kutoka mikoa yote ya Tanzania ambao ni watoto yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi.
 
Kwa upande  wa michezo alisema kuwa wanashiriki michezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mpira wa miguu kwa wanawake na mpira wa mikono kwa wanawake, drama na riadha.
 
Aliongeza  kuwa eneo la viwanja wanalo kubwa na la kutosha lakini  hawana viwanja rasmi pia wanakabiliwa na upungufu wa vifaa vya michezo kama vile jezi, viatu na mipira. 
 
“Kwa mara ya kwanza shule yetu ilishiriki mashindano ya UMISETA mwaka 2012 na kufikia ngazi ya mkoa hali ambayo imetutia  moyo na tunaamini kuwa ipo siku wanafunzi wetu watafika ngazi ya Taifa”, alisema Mwalimu Mensah .
 
Wafanyakazi wa kampuni ya Montage Tanzania waliamua kusherehekea sikukuu ya Eid Mubarak na wanafunzi hao ili kuonyesha kuwa wanawajali na kuwathamini. Pia waliwapatia zawadi za  jezi nne za michezo mbili za mpira wa miguu na mbili za mpira wa mikono na mipira 10, mitano ya mpira wa miguu na mitano ya mpira wa mikono. (Kwa hisani ya Jukwaa Huru)

No comments: