Saturday, November 22, 2014

KATIBU MKUU UVCCM TAIFA AENDELEA NA ZIARA YAKE WILAYANI MBINGA, SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA VIONGOZI WENYE MATENDO YA HOVYO

Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana Taifa (UVCCM) Sixtus Mapunda, akipokelewa na Vijana wakiwemo pia wanachama wa Chama Cha Mapinduzi leo asubuhi, katika eneo la Tanki la maji mjini hapa wakati anawasili wilayani Mbinga akitokea wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma.

Katibu Mkuu UVCCM Taifa, Sixtus Mapunda akiwasili katika ofisi kuu ya CCM wilayani Mbinga.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana Taifa (UVCCM) Sixtus Mapunda akizungumza na wananchi wa kata ya Mpepai wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KATIBU wa Umoja wa Vijana Taifa (UVCCM) Sixtus Mapunda amesema, serikali nchini ipo tayari kumchukulia hatua za kinidhamu kiongozi yeyote aliyekuwa madarakani, ambaye anaonesha kuwa na matendo ya hovyo kwa wananchi wake na yenye  kurudisha nyuma maendeleo husika.

“Ndugu zangu wananchi hatupo tayari mahali popote pale, kumvumilia Mkuu wa wilaya au Mkurugenzi mtendaji mwenye matendo ya hovyo na yenye kukatisha tama wananchi, tukisikia tunamwondoa haraka tunahitaji kiongozi mwenye kujali maisha na maendeleo ya watu wake”, alisema.

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu huyo leo, alipokuwa akihutubia wananchi wa kata ya Mpepai wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kwenye mkutano wa hadhara, uliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Mpepai wilayani humo.   

Mapunda alisema kuwa itakuwa ni ajabu kwa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kumkalia kimya bila kumwajibisha kiongozi ambaye hana nia njema na taifa hili, huku akiwaacha wananchi wakiteseka kutokana na mambo yake binafsi ambayo hayana tija katika jamii.


Pamoja na mambo mengine, Mapunda alizungumzia tatizo la mlundikano wa mahindi yaliyopo hapa wilayani Mbinga, ambayo serikali haija ya nunua, hivyo alieleza kuwa atakwenda kuzungumza na Rais Jakaya Kikwete ili kuona namna ya kunusuru hali hiyo.

Aliongeza kuwa wilaya hiyo hivi sasa ina mahindi mengi, ambapo inahitajika nguvu ya ziada kuona namna gani yananunuliwa ili wakulima waweze kupata hata fedha za kuendeshea maisha yao, ikiwemo kupeleka watoto wao shule.

Vilevile alifafanua kwamba atakapokutana na Rais Kikwete, atamuomba wazungumze na balozi wa nchi ya Kenya ambaye yupo hapa nchini, ili mahindi hayo yanunuliwe na kusafirishwa mpaka huko, kutokana na nchi hiyo hivi sasa inakabiliwa na tatizo la njaa.

“Tunachangamoto kubwa ya mlundikano wa mahindi hapa Mbinga, taarifa ninazo lakini napenda kuwaambia tutaona namna ya kumaliza kero hii, ili ndugu zangu wakulima nanyi muweze kupata fedha za kusukuma mbele maendeleo yenu”, alisema Mapunda.

Kadhalika alifafanua kuwa serikali itaendelea kufanya jitihada ya kutatua matatizo ya wananchi, hivyo amewataka waendelee kuwa na moyo wa kushiriki kikamilifu katika kuendeleza kauli mbiu ya kilimo kwanza ili taifa lisipatwe na baa la njaa.

Katibu wa UVCCM taifa, Bw. Mapunda yupo katika ziara yake ya kikazi ya siku tatu hapa mkoani Ruvuma.




No comments: