Sunday, November 2, 2014

WAPOTEZA MAISHA BAADA YA KUNYWA POMBE KUPITA KIASI



Na Willy Sumia,
Sumbawanga.

WATU wawili wamefariki dunia kutokana na kulewa pombe na kuwa chakari wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa, kitendo ambacho kiliwasababishia kuzama katika mto wakati walipokuwa wakirejea nyumbani.

Kitendo cha kuzama mtoni, watu hao wanadaiwa kupoteza maisha baada ya kushindwa kuvuka mto walipokuwa wakirejea kutoka kunywa pombe nyakati za usiku katika tarafa ya Mtowisa wilayani humo.

Waliopoteza maisha wametajwa kuwa ni Leonard Salehe (44) mkazi wa kijiji cha Zimba na Gilbert Machimu (47) mkazi wa kijiji cha Sakalilo.


Imeelezwa kuwa hivi karibuni, Leonard Salehe alikuwa ametoka matembezini akiwa amelewa na alipofika katika mto Mkanga alishindwa kujimudu na kuyumba hadi kwenye mkondo wa maji na kuzama hadi alipokutwa na umauti.

Gilbert  Machimu alikuwa ametoka matembezini naye akiwa amelewa pombe za kienyeji alipofika katika mto Zimba, alishindwa kujimudu na kuyumba hadi mtoni ambako maji yalimzidi nguvu na kufariki dunia.

Kamanda wa polisi mkoani Rukwa, Jacob Mwaruanda alisema uchunguzi wa awali ulibaini kuwa vifo vyote hivyo vilisababishwa na ulevi uliopindukia, ambao uliwafanya marehemu hao kushindwa kujimudu na kuzama katika maji ya mito hiyo, walipokuwa wakirejea majumbani kwao.

Msimu wa kiangazi katika mkoa huo, huwa kunaibuka tabia ya kunywa pombe kupita kiasi kutokana na kukamilika kwa mavuno na kuongezeka kwa kipato baada ya kuuza mazao yao hasa mahindi.



No comments: