Wednesday, November 5, 2014

WANAFUNZI WAANDAMANA KUTOKANA NA CHOO WANACHOKITUMIA KUJAA NA KUSABABISHA HARUFU KALI

Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

WANAFUNZI wanaosoma katika Chuo cha Maendeleo ya Jamii (FDC) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameandamana kwenda katika ofisi ya Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, kutokana na choo wanachokitumia kujaa na kusababisha harufu kali katika eneo la chuo hicho.

Tukio hilo lilitokea Novemba 3 mwaka huu majira ya asubuhi, ambapo walieleza kwa nyakati tofauti kuwa walifikia hatua ya kufanya hivyo kutokana na uongozi husika wa chuo hicho, kutochukua hatua za haraka katika kunusuru hali hiyo.

Walisema baada ya kuona tatizo hilo halifanyiwi kazi kwa muda mrefu, waliona ni vyema wapeleke kilio chao kwa Mkurugenzi mtendaji wa wilaya ya Mbinga Hussein Ngaga, ili tatizo hilo la choo kufurika lifanyiwe kazi haraka.


Aidha walipofika katika eneo la ofisi za Mkurugenzi huyo, wanafunzi hao walielezwa kwamba wasiwe na jazba hivyo warejee katika eneo la chuo ambapo baada ya kufanya hivyo, baadhi ya viongozi wa kata ya Mbinga mjini akiwemo Ofisa tarafa wa Mbinga mjini, walikwenda huko kuzungumza na wanafunzi hao na uongozi wa chuo cha FDC ili kuweza kumaliza kero hiyo.

Akihojiwa na waandishi wa habari, Mkuu wa chuo hicho cha maendeleo ya jamii wilayani hapa Aidan Mchawa alisema hasira za wanachuo hao kuandamana zilitokana na uongozi husika wa chuo, kuchelewa kufanyia matengenezo ya choo hicho ambacho kimejaa.

Mchawa alisema tatizo hilo la kuchelewa lilitokana na chuo kukosa fedha za kuweza kufanya kazi hiyo, hivyo jitihada zitafanyika za kuweza kumaliza kero hiyo mapema iwezekanavyo.


“Chuo hiki kina wanafunzi 150 wote hawa waliandamana kupinga tatizo hili ambalo lipo mbele yetu, tulijaribu kuwatuliza wasifanye hivi lakini ilishindikana kutokana na wengi wao kuwa na hasira kali”, alisema Mchawa.

No comments: