Thursday, January 1, 2015

MAKAHABA WATIKISA MANISPAA YA SONGEA, WAITAKA SERIKALI KUCHUKUA HATUA



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WANANCHI wa Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wameshtushwa na kuwepo kwa wimbi la wasichana kutoka nje ya wilaya hiyo, wanaofika na kufanya vitendo vya ukahaba katika mitaa mbalimbali  nyakati za usiku huku wengine  wakicheza muziki wakiwa nusu uchi kwenye nyumba za starehe maarufu  kwa jina la Kangamoko, jambo linalohofiwa kuongezeka kwa maambukizi mapya ya ugonjwa wa Ukimwi.

Ilielezwa kuwa kundi hilo la makahaba linadaiwa kutoka mikoa ya Mbeya, Tanga, Dar es Salaam na miji mingine mikubwa wamekuja Songea kwa ajili ya kufanya biashara hiyo ya ukahaba, ambapo ikifika majira ya saa tatu usiku wamekuwa wakijipanga katika mitaa mbalimbali kutafuta wanaume.

Makahaba hao ambao wanalalamikiwa wanakadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 18 hadi 30 ambao wamekuwa wakifanya shughuli hiyo isiyo rasmi hasa katika mitaa maarufu ya Delux, Serengeti, Majimaji na barabara ya Sokoine, huvaa nguo fupi na nyingine zinazoonesha maumbile ya miili yao kwa lengo la kutaka kuwavutia wanaume, ambao hujikuta wakiingia mtegoni bila kutarajia kutokana na ushawishi unaofanywa na wasichana hao.

WAHITIMU MAFUNZO YA JKT WATAKIWA KULINDA AMANI


Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama kushoto, akisalimiana na Mkuu wa  utumishi wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) makao makuu, Kanal Thomas Mbele, kabla ya kufunga mafunzo ya miezi mitatu ya kijeshi kwa vijana 985 operesheni miaka 50 ya muungano kwa mujibu wa sheria awamu ya pili mwak 2014 katika kikosi cha 842 KJ Mlale JKT, katikati ni kaimu mkuu wa Brigedi ya 410 Songea Kanal JJ Fulla.

Na Dustan Ndunguru,

Songea.

WAHITIMU wa mafunzo ya Jeshi la kujenga Taifa (JKT) nchini, wametakiwa kuwa mstari wa mbele katika kulinda na kudumisha amani tuliyonayo badala ya wao kuwa chanzo cha vurugu hususani, katika kipindi hiki ambapo taifa lipo katika mchakato wa kupata katiba mpya.

Naibu Waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi, Jenista Mhagama alitoa rai hiyo mwishoni mwa wiki iliyopita, wakatialipokuwa akifunga mafunzo ya miezi mitatu  ya kijeshi kwa wahitimu 985 wa kozi ya ualimu   Operesheni miaka 50 ya Muungano, kwa mujibu wa sheria awamu ya pili mwaka 2014 katika kikosi cha 842 KJ Mlale JKT  wilaya ya Songea mkoani Ruvuma.

Alisema serikali haikukosea kurudisha mafunzo ya JKT kwa vijana wanaomaliza vyuo,  kwani dhamira yake kubwa ni kutaka kuwaandaa na kuwajenga vijana hao kuwa viongozi bora, na wenye ari kubwa na  moyo wenye uzalendo kwa nchi yao.

Jenista pia aliwataka kukataa kutumika vibaya na watu wenye nia mbaya katika nchi, kwa kuwatumia kama ngazi ya wao kufanikisha mambo yao binafsi jambo ambalo litaweza kuhatarisha amani na utulivu uliodumu tangu nchi ipate uhuru mwaka 1961.

SCCULT YAINGIA KATIKA KASHFA MPYA, YADAIWA KUKUMBATIA FEDHA ZA WAKULIMA



Kassian Nyandindi,
Songea.

OFISI ya Chama Kikuu Cha Akiba na Mikopo Tanzania (SCCULT) mkoani Ruvuma, imeingia katika kashfa mpya baada ya uongozi wa chama cha kuweka na kukopa, Kihulila juu SACCOS wilaya ya Mbinga mkoani humo, kuishushia lawama kwamba imeshindwa kushughulikia lalamiko lao kwa muda mrefu la kurejeshewa, shilingi milioni 3,122,000 baada ya kujitoa uanachama miaka mingi iliyopita.

Walisema licha ya ofisi hiyo kuwa na taarifa kamili juu ya jambo hilo na ufuatiliaji wa madai hayo, kuanza kufanyika tokea Februari 16 mwaka 2010 na SACCOS hiyo ilipojitoa uanachama kwa hiari, Desemba 30 mwaka 2008 hakuna jitihada zilizozaa matunda mpaka sasa.

Akizungumza kwa niaba ya viongozi wenzake Katibu wa idara ya mikopo Kihulila juu SACCOS, Kelvin Ndunguru alisema kawaida tokea siku walipojitoa uanachama, baada ya siku 90 ilibidi SCCULT warejeshe mafao yao yaliyotokana na michango mbalimbali waliyokuwa wakichangia.

Ndunguru alifafanua kuwa tatizo hilo lipo hata mezani kwa Mrajisi msaidizi wa vyama vya ushirika mkoani humo, na viongozi wengine wa wilaya ya Mbinga, lakini hakuna majibu sahihi wanayopewa juu ya madai hayo huku siku zikiendelea kupita.

WAKULIMA WALIA NA MVUA, MAZAO YAO YAKAUKA SHAMBANI

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

KUCHELEWA kunyesha kwa mvua katika maeneo mbalimbali mkoani Ruvuma, kumesababisha wakulima kupatwa na wasiwasi juu ya hali ya uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara, katika msimu huu wa kilimo hasa ikizingatiwa kuwa misimu iliyopita mvua ilikuwa ikianza kunyesha mkoani humo katika mwezi Novemba tofauti na ilivyo sasa.

Katika maelezo yao kwa waandishi wa habari kwa nyakati tofauti, wakulima wa wilaya za Namtumbo na Songea mkoani humo walisema, hali hiyo ya mvua kuchelewa kunyesha imeshaanza kuwatia hofu kubwa kwani tayari walishafanya maandalizi yote ya kilimo, ikiwemo kupanda mazao mashambani lakini hadi sasa mvua imekuwa ikinyesha kwa kusuasua.

Walisema hadi sasa mazao waliyopanda yameanza kuota lakini yanakauka kutokana na kukosekana kwa mvua za kutosha na kwamba hata wadudu wamekuwa wakijitokeza na kushambulia mimea iliyoota. 

Tuesday, December 30, 2014

MKURUGENZI MTENDAJI MBINGA AMDANGANYA RAIS KIKWETE, ADAIWA KUPANGIA MATUMIZI FEDHA ZA WAKULIMA WA KAHAWA KINYUME NA TARATIBU ZA USHIRIKA

Rais Jakaya Kikwete.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MALALAMIKO yaliyotolewa juu ya shilingi bilioni 2 ambazo baadhi ya vyama vya ushirika (AMCOS) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, vilikopeshwa na shirika la hifadhi ya jamii (NSSF) na kuleta gumzo kuwa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Hussein Ngaga, hakuzipeleka kwenye vyama hivyo badala yake alidaiwa kuziingiza kwenye akaunti ya halmashauri ya wilaya hiyo tumebaini kwamba, fedha hizo ziliingizwa kwenye akaunti husika za vyama hivyo huku akitoa masharti kwa uongozi wa AMCOS hizo kuwa, hawana ruhusa ya kuzifanyia matumizi ya kukopeshana mpaka idhini itoke kwake.

Aidha mkurugenzi huyo analalamikiwa kuwa viongozi hao wa vyama vya ushirika, alikuwa akiwapangia matumizi ya fedha hizo baada ya yeye kujiridhisha kwanza wameandaa mpango kazi wa mahesabu husika na kiasi cha kahawa walichonacho ambayo itaingizwa kiwandani, ndipo alikuwa akiwaruhusu kwenda kutoa fedha benki huku akihakikisha hundi walizoandika zina kiwango halisi anachokifahamu.

Na wakati mwingine analalamikiwa kuwa, alikuwa hawapatii fedha kwa kiwango walichoomba katika mahesabu hayo ambayo walikuwa wakimpelekea ofisini kwake kwa ajili ya kuyakagua na kujiridhisha, badala yake alikuwa anapunguza kwa kiwango anachokitaka yeye.

Tumebaini pia baada ya mauzo ya kahawa kufanyika mnadani Moshi, hivi sasa mkurugenzi Ngaga amekuwa akikwepa kutoa Fomu ya mauzo ya kahawa kwa dola (Account Sale) kwa wanaushirika hao, licha ya wao kumfuata mara kwa mara wakimtaka awapatie.

Katika fomu hiyo huonyesha kahawa ambazo zimeuzwa kwa dola na ubadilishaji wa fedha za mauzo ya kahawa kutoka kiwango cha dola kuwa shilingi, hivyo inadaiwa huenda zimeuzwa kwa bei ya juu huku wanaAMCOS hao wakimlalamikia kuwalipa bei ndogo, ndio maana hataki kutoa fomu hizo na kuweka mchakato huo wa mauzo kuwa bayana ili wakulima waweze kufahamu juu ya mauzo ya kahawa yao ulivyofanyika.

Hali hiyo imeelezwa na wakulima hao kuwa huenda anaficha ukweli halisi usiweze kujulikana juu ya mwenendo mzima wa mauzo ya kahawa yao ulivyofanyika huko mnadani kwa kila mkulima (vikundi).

Sunday, December 28, 2014

TAMISEMI MKURUGENZI WENU WA MBINGA ANA MATATIZO CHUKUENI HATUA SASA KABLA KIDONDA HAKIJAWA SUGU

Hawa Ghasia, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI)
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MAPYA yanaendelea kuibuka katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, ambapo baadhi ya Wafanyakazi wenye mikataba ya ajira ya muda wamemlalamikia Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo Hussein Ngaga, kwamba amekuwa ni mtu wa kuwatolea lugha zenye kukatisha tamaa ya kufanya kazi na kutowalipa mishahara yao kwa wakati. 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti huku wakiomba majina yao yasitajwe kwa kuhofia usalama wa kazi zao wakidai kufukuzwa kazi, walisema Mkurugenzi huyo amekuwa akiwatolea lugha zenye ukali hasa pale wanapokuwa wakidai madai yao ya msingi, kama vile fedha za malipo ya kazi walizofanya.

Wengine walifafanua kuwa hata mishahara yao ambayo inabidi walipwe tarehe husika za mwisho wa mwezi, kwa mujibu wa taratibu na sheria zilizowekwa na serikali, Ngaga amekuwa hafanyi hivyo badala yake amekuwa akiwalipa kwa kuchelewesha.

KWA MABOMU HAYA YA SONGEA, TUNAPASWA KUJIULIZA VYOMBO VYA ULINZI NA USALAMA VIPO WAPI?

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.
Na Kassian Nyandindi,

MATUKIO ya mabomu mjini Songea hapa mkoani Ruvuma, umekuwa sasa ni mchezo mchafu ambao unahatarisha usalama wa raia, hivyo kuna kila sababu kwa serikali kuchukua hatua madhubuti juu ya kudhibiti hali hii.

Tunasema kuna kila sababu sasa ya kufanya hivyo, kutokana na kile tunachoweza kusema kwamba tumechoka kusikia kauli za viongozi wa ngazi ya juu hususani hapa mkoani, wakisema kwamba watahakikisha hali hii itadhibitiwa kwa kuwakamata wahusika ili matukio kama haya yasiweze kuendelea kutokea.

Ni muhimu sasa kuona namna gani tunashirikisha jamii kwa karibu zaidi, ili waweze kutoa ushirikiano wa kutosha ambao baadaye utaweza kuleta tija katika kukomesha genge la watu hawa, ambao wanahusika kutengeneza mabomu haya.

Hili ni tukio la tatu sasa kutokea hapa songea, mara ya kwanza askari polisi walirushiwa bomu, mara ya pili lilitegwa karibu na kituo cha kurusha matangazo (TBC) mjini Songea na leo askari hawa hawa wanarushiwa tena, tunapenda kuhoji vyombo vya ulinzi na usalama vipo wapi au vimeenda likizo? 

Tunahoji hivyo sio kwa nia mbaya, kwa sababu mara kwa mara tumekuwa tukiwanukuu baadhi ya vigogo wakisisitiza na kuahidi kukomesha hali hii isiweze kuendelea kutokea, lakini inashangaza kuona matukio haya yanajirudia na kuwafanya watu waishi kwa wasiwasi.

Saturday, December 27, 2014

JESHI LA POLISI NCHINI LAUNDA TIMU KUCHUNGUZA TUKIO LA BOMU SONGEA

Askari aliyejeruhiwa na bomu mjini Songea mkoa wa Ruvuma, WP Mariamu Lukindo akiwa amelazwa katika hospitali ya mkoa huo iliyopo mjini hapa.
Na Mwandishi wetu,
Songea.

TIMU ya makachero kutoka makao makuu ya Jeshi la polisi nchini, wakishirikiana na wa mkoa wa Ruvuma, kwa ajili ya kufanya uchunguzi kuhusiana na matukio ya mabomu yanayoendelea kujitokeza mara kwa mara mkoani humo.

Makachero hao wanatoka Jijini Dar es salaam, kufanya uchunguzi kuhusiana na tukio la mtu mmoja aliyelipukiwa na bomu maeneo ya majengo mjini songea  na kujeruhi askari polisi wawili, wakati akijiandaa kuwarushia  askari waliokuwa doria na kisha bomu hilo kumuua mwenyewe.

Hayo yalisemwa na kaimu mkurugenzi wa makosa ya jinai nchini, Naibu Kamishna wa Jeshi la Polisi Diwani Athumani aliyewasili mjini  Songea kwa helkopta kwa ajili ya tukio hilo ambalo mtu ambaye hajatambulika,   amelipukiwa na bomu hilo na kufariki dunia  papo hapo wakati akijaribu kuwarushia askari waliokuwa doria na kujeruhi askari wawili.

Aliwataja askari waliojeruhiwa kuwa ni PC Mselemu na WP Mariamu Lukindo  ambaye bado amelazwa katika hospitali ya mkoa iliyopo mjini Songea.

WAENDESHA PIKIPIKI TUNDURU WACHOMA MOTO VIBANDA NA KULETA FUJO KITUO KIKUU CHA POLISI


Kamanda wa Polisi mkoani Ruvuma, ACP Mihayo Msikhela.
Na Waandishi wetu,
Tunduru.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida waendesha pikipiki maarufu kwa jina la yeboyebo, wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma walifanya maandamano makubwa kwa lengo la kupinga vitendo vya unyanyasaji ambavyo wanafanyiwa na askari polisi wa wilaya hiyo, ikiwemo kuwakamata hovyo bila kufuata taratibu.

Madereva hao waliandamana na kufanya fujo katika kituo kikuu cha polisi cha wilaya ya Tunduru, pia waandamanaji hao walichoma moto vibanda vinne ambavyo hutumiwa na kampuni ya State business center na kusababisha hasara ya mamilioni ya fedha.

Kwa nyakati tofauti madereva hao walisema wamechukua maamuzi hayo magumu, baada ya kuchoshwa na vitendo viovu ikiwemo kuombwa rushwa mara kwa mara, ambavyo hufanyiwa na askari hao hasa wa kitengo cha usalama barabarani.

AFARIKI DUNIA BAADA YA KUUMWA NA NYOKA MWENYE SUMU KALI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

BINTI wa miaka mitano Mwanahamis Omary, mkazi wa kijiji cha Kalulu wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, amekutwa akiwa amefariki dunia baada ya kuumwa na nyoka mwenye sumu kali.

Akizungumzia tukio hilo baba wa mtoto huyo Omary Bakari alisema mkasa huo ulimpata mtoto huyo, wakati akiwa anavuka mto Kalulu kuelekea shambani na kwamba wakati anakumbwa na tatizo hilo alikuwa amefuatana na mama yake mzazi Zainabu Ally.

Baada ya tukio hilo mama yake huyo alipiga kelele za kuomba msaada wa kumpeleka mtoto wao katika zahanati ya kijiji hicho  kwa matibabu zaidi, lakini ilishindikana kwani mtoto huyo alifariki dunia wakiwa njiani kuelekea katika zahanati hiyo.

Hata hivyo nyoka huyo hakuweza kutambuliwa ni wa aina gani, wakati anamuuma mtoto huyo.

UVCCM RUVUMA YAITAKA JAMII KUFARIJI WAGONJWA



Steven Augustino na Abbas Mlanya,
Tunduru.

UMOJA wa Vijana Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) mkoani Ruvuma, umewataka wadau mbalimbali kujenga tabia ya kuwatembelea wagonjwa ambao wamelazwa hospitalini, kwa lengo la kuwafariji na kuwapatia zawadi hasa katika kipindi cha sikukuu za kitaifa.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa umoja huo mkoani hapa, Alex Nchimbi wakati alipowatembelea wagonjwa waliolazwa katika hospitali ya wilaya ya Tunduru.

Aidha Nchimbi ambaye aliongozana na viongozi wenzake wa chama cha mapinduzi wilayani humo, wakiwemo wakiwemo katibu wa CCM wilaya Mohammed Lawa, Abdakah Zubery Mmala (Mwenyekiti wa UVCCM wilaya), Jumma Khatibu (Katibu UVCCM wilaya) wakiwemo pia makada na wakereketwa wa chama hicho.

Monday, December 22, 2014

SAKATA LA ESCROW: RAIS KIKWETE AZUNGUMZA NA WAZEE

Na Mwandishi wetu,
Dar.

RAIS Jakaya Kikwete hatimaye leo ametengua nafasi ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka kupitia hotuba aliyotoa kuzungumzia kashfa ya upotevu wa fedha kutoka akaunti ya Tegeta Escrow.

Hatua hiyo imechukuliwa na Rais Kikwete mbele ya wazee wa Dar es Salaam, aliokuwa akiongea nao na matangazo kurushwa moja kwa moja kupitia televisheni ya taifa na vyombo vingine.

Uchunguzi uliofanywa na kamati ya hesabu za umma ya Tanzania (PAC) ilidai kuwa Profesa Tibaijuka ni mmoja wa watu walionufaika kinyume cha sheria, kwa kujipatia fedha zilizotoka katika akauti hiyo iliyofunguliwa kutunza fedha kusubiri ufumbuzi wa mgogoro wa kibiashara kati ya kampuni ya kusambaza umeme TANESCO na kampuni binafsi ya kuzalisha umeme ya IPTL.

Siku chache zilizopita Profesa Tibaijuka aliitisha mkutano na waandishi wa habari Jijini Dar Es Salaam, kubainisha kuwa hakuwa akikusudia kujiuzulu kutokana na tuhuma zilizokuwa zikimkabili.

Aidha Rais Kikwete hakutangaza kuwachukulia hatua watumishi wengine waliodaiwa kuhusika na tuhuma hiyo, kwa maelezo kuwa uchunguzi zaidi unatakiwa kwa kila mtuhumiwa.

Kumekuwa na ubishi mkubwa kujadili endapo fedha ambazo ni mabilioni zilizochukuliwa zilikuwa za umma au la. 

Hata hivyo Rais Kikwete alisema maelezo aliyopewa na wataalamu yanaonyesha hazikuwa mali ya TANESCO.

KAYOMBO ALALAMIKIWA NA WAPIGA KURA WAKE KWA KUMTETEA MKURUGENZI MTENDAJI NA MKUU WA WILAYA YA MBINGA, WASEMA MWAROBAINI WAKE UCHAGUZI MKUU MWAKANI

Gaudence Kayombo.
Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

BAADHI ya Wakazi wa mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wamemtaka Mbunge wa jimbo la Mbinga, Gaudence Kayombo kufuta kauli zake anapokuwa akihutubia wananchi katika majukwaa ya kisiasa na kujenga hoja za kuwatetea Mkurugenzi mtendaji Hussein Ngaga na Mkuu wa wilaya hiyo, Senyi Ngaga kwamba ni viongozi wazuri na wameleta maendeleo makubwa wilayani humo.

Sambamba na hilo wananchi hao ambao ni wapiga kura wake, wamesema kuwa kauli za Kayombo kuwatetea viongozi hao ni sawa na kujichimbia kaburi kwa kupoteza nafasi aliyonayo, katika uchaguzi mkuu ujao ambao unatarajiwa kufanyika mwakani kwa nafasi ya kumchagua Rais, Wabunge na Madiwani.

Walifafanua kuwa wanamshangaa Mbunge huyo amekuwa akiwasafisha viongozi hao wawili kwamba wanafanya vizuri, wakati maendeleo mengi yaliyofanywa wilayani humo yamefanywa na viongozi wenzao waliowatangulia na sio wao ambao wamefika hapa wilayani wanamuda mfupi na hakuna jambo jipya la maendeleo walilobuni na  kuweza kujivunia   kwa wananchi wakati mengi yaliyopo wanayoyaendeleza ni yale ambayo yalifanyiwa ubunifu na viongozi wenzao waliowatangulia.

Hayo yalisemwa jana na wakazi wa mji wa Mbinga kwa nyakati tofauti, mara baada ya Mbunge Kayombo kumaliza kuhutubia katika viwanja vya soko kuu mjini hapa, kwenye mkutano wa hadhara ambao uliandaliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani humo kwa ajili ya kushukuru wapiga kura wake kukipatia viti vingi vya nafasi ya Wenyeviti wa vitongoji, katika chaguzi za serikali za mitaa zilizofanyika hivi karibuni. 

Saturday, December 20, 2014

WAPOTEZA MAISHA KWA MAMBO YA KIMAPENZI NA USHIRIKINA



Steven Augustino na Abbas Mlanya,
Ruvuma.

WATU wawili wamefariki dunia mkoani Ruvuma, katika matukio mawili tofauti yaliyotokea wilayani Tunduru na Namtumbo mkoani humo, ambapo la kwanza linasababishwa na wivu wa kimapenzi na lingine linahusishwa na mambo ya ushirikina.

Baadhi ya mashuhuda wa tukio lililotokea wilayani Tunduru, walisema kuwa marahemu aliyetambuliwa kwa jina la Yusuph Jafari ambaye amehamia wilayani humo, akitokea wilaya ya Masasi alikuwa kinara wa kutembea na wake za watu na baadaye kuuawa na watu wasiojulikana.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, ASP Mihayo Msikhela alisema kuwa tukio la kwanza lilitokea  Disemba 16 mwaka huu katika kitongoji cha Naunditi kijiji cha Majimaji, kilichopo kata ya Muhuwesi wilayani humo.

MKURUGENZI MTENDAJI MBINGA AMDANGANYA RAIS KIKWETE, ADAIWA KUCHOTA FEDHA ZA WAKULIMA WA KAHAWA NA KUZIPANGIA MATUMIZI KINYUME NA TARATIBU ZA USHIRIKA

Rais Jakaya Kikwete.

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

SHILINGI bilioni 2 ambazo baadhi ya vyama vya ushirika wa kahawa wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, vilikopeshwa hivi karibuni na shirika la hifadhi ya jamii (NSSF) zimezua malalamiko kwamba, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Hussein Ngaga hakuzipeleka kwenye vyama hivyo badala yake anadaiwa kuziingiza kwenye akaunti ya halmashauri ya wilaya hiyo na kuanza kukopesha vikundi husika.

Imeelezwa kuwa kitendo kilichofanywa na mkurugenzi huyo, ni ukiukwaji wa sheria na taratibu za ushirika, hivyo alitakiwa fedha hizo azifikishe kwanza kwenye ushirika kwa kufuata mgawo husika na sio yeye kuzipangia matumizi na kwamba kwa kufanya hivyo, amemdanganya Rais Jakaya Kikwete kwa kauli yake aliyoitoa hivi karibuni mbele yake kwamba fedha hizo watakabidhiwa walengwa wa vyama vya ushirika.

Rais Kikwete mnamo Julai 19 mwaka huu, alikabidhi mfano wa hundi kwa viongozi wa vyama vya ushirika ambavyo vilikopeshwa fedha hizo alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo, kwa vyama vinne ambavyo vilipewa mkopo huo na shirika hilo.

Friday, December 19, 2014

WAANDIKISHAJI NA WASIMAMIZI UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA WILAYANI MBINGA WALALAMIKIA POSHO ZAO

Waziri wa TAMISEMI Hawa Ghasia (kulia) pamoja na Katibu mkuu TAMISEMI Jumanne Sagini. (kushoto)
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KASORO za uchaguzi zilizojitokeza katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika hivi karibuni hapa nchini, pia hali ya hewa imechafuka wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma kufuatia baadhi ya Waandikishaji na Wasimamizi wa uchaguzi huo, kumlalamikia Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo Hussein Ngaga, kwamba malipo ya posho walizolipwa katika zoezi hilo amewalipa kidogo, tofauti na maeneo mengine nje ya wilaya hiyo.
Aidha kufuatia hali hiyo Waandikishaji na Wasimamizi hao wamemuomba Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Hawa Ghasia, kuingilia kati na kuweza kulifanyia kazi jambo hilo ili waweze kupata haki yao ya msingi kwa kazi waliyofanya.
Malalamiko hayo yalitolewa kwa nyakati tofauti walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, kwa kuomba majina yao yasitajwe gazetini ambapo walisema kuwa hata wakati wanafanyiwa semina na kupewa miongozo juu ya utekelezaji wa zoezi hilo, hawakulipwa posho badala yake waliambiwa kwamba watalipwa mara baada ya uchaguzi kufanyika.

Thursday, December 18, 2014

UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA: WACHOMEWA NYUMBA MOTO KUTOKANA NA MALUMBANO YA KISIASA



Na Steven Augustino,
Tunduru.

UCHAGUZI wa Serikali za Mitaa ambao umefanyika hivi karibuni Disemba 14 mwaka huu, umeacha makovu wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma kwa baadhi ya viongozi na wakereketwa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kuchomewa moto nyumba zao na watu wasiojulikana, na kusababisha hasara kubwa ya kuunguliwa mali zilizomo ndani ya nyumba hizo pamoja na kukosa makazi. 

Taarifa za tukio hilo zinaeleza kuwa Diwani wa kata ya Ngapa Rashid Issaya na mwanachama wake Hassan Liugu nyumba zao zilichomwa moto, baada ya kuzuka malumbano ya kisiasa na kuwasababishia hasara kubwa ya kuungua nyumba zao pamoja na mali zilizokuwemo ndani yake.

Sambamba na tukio hilo, mfuasi mmoja wa Chama Cha Wananchi (CUF) Yashua Kawisa (21) ambaye ni mkazi wa kijiji cha Mbesa wilayani humo, naye amejeruhiwa vibaya kwa kukatwa mapanga, wakati akiwa katika kampeni za uchaguzi huo.

AFARIKI DUNIA BAADA YA KUKANYAGWA NA LORI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

KIJANA mwenye umri wa miaka 15 aliyefahamika  kwa jina la Khasim Mohammed, mkazi wa kijiji cha Mtangashari wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma amefariki dunia baada ya kupata ajali katika gari, ambalo alikuwa ameomba msaada ili aweze kusafiri.

Mihayo Msikhela kamanda wa polisi wa mkoa huo, alisema kuwa marahemu huyo alifariki dunia papo hapo baada ya kuanguka katika gari hilo.

Alisema ajali hiyo ilitokana na gari lenye namba za usajiri T699 BCX mali ya kampuni ya China Civil Engineering Construction Co.Ltd (CCECC) inayojenga kipande cha barabara kilometa 58.7 kutoka Tunduru mjini hadi Matemanga. 

Tuesday, December 16, 2014

MADIWANI MBINGA KUMSHTAKI MKURUGENZI KWA WAZIRI MKUU

Waziri mkuu, Mizengo Pinda.

Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

BAADHI ya Madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wanampango wa kwenda kumuona Waziri mkuu wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda kwa lengo la kufikisha kilio chao juu ya mgogoro ambao unaendelea kati ya mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo na Afisa elimu wa msingi wa wilaya hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wa habari hizi, Madiwani hao walisema kuwa wamechoshwa na mambo ambayo yanafanywa na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Mbinga, Hussein Ngaga kwa kuendekeza migogoro na mambo yasiyokuwa na tija katika jamii.

Aidha walifafanua kuwa Ngaga ameshindwa kuiongoza wilaya hiyo, kutokana na kuendekeza migogoro na afisa elimu msingi wa wilaya hiyo, Mathias Mkali na kuchukua hatua ya kumsimamisha kazi kinyume na taratibu za utumishi wa umma wakati hana makosa.

SAFARI YA MWISHO YA MARAHEMU MENAS ANDOYA MBUNDA, ASKOFU NDIMBO AWATAKA WAKRISTO KUTENDA MEMA KATIKA MAISHA YAO

Mzee Asteri Ndunguru, upande wa kulia akisoma taarifa fupi ya marahemu Menas Mbunda Andoya nyumbani kwa marahemu mjini hapa.

Mwili wa marahemu Menas Mbunda Andoya ukiombewa katika kanisa la Mtakatifu Killian lililopo mjini Mbinga.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma naye alishiriki katika ibada ya mazishi hayo, kwenye kanisa la Mtakatifu Killian Mbinga mjini.

Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

WAKRISTO wametakiwa kuacha matendo ya kumpuuza mwenyezi Mungu, badala yake wametakiwa kutenda mema katika maisha yao ya kikristo kwani hakuna binadamu aliyefunga mkataba na Mungu juu ya kuishi.

Hayo yalisemwa na Askofu mkuu wa jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, John Ndimbo alipokuwa akihutubia katika misa takatifu ya mazishi ya marahemu Menas Andoya kwenye kanisa la mtakatifu Kiliani lililopo mjini hapa.

“Miili yetu ni hekalu la bwana na maskani ya mpito hapa duniani, inatupasa kufanya kila jitihada kwa mambo ambayo yanampendeza Mungu, hakuna binadamu asiyekuwa na utashi juu ya kifo”, alisema Ndimbo.