Thursday, December 18, 2014

UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA: WACHOMEWA NYUMBA MOTO KUTOKANA NA MALUMBANO YA KISIASA



Na Steven Augustino,
Tunduru.

UCHAGUZI wa Serikali za Mitaa ambao umefanyika hivi karibuni Disemba 14 mwaka huu, umeacha makovu wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma kwa baadhi ya viongozi na wakereketwa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kuchomewa moto nyumba zao na watu wasiojulikana, na kusababisha hasara kubwa ya kuunguliwa mali zilizomo ndani ya nyumba hizo pamoja na kukosa makazi. 

Taarifa za tukio hilo zinaeleza kuwa Diwani wa kata ya Ngapa Rashid Issaya na mwanachama wake Hassan Liugu nyumba zao zilichomwa moto, baada ya kuzuka malumbano ya kisiasa na kuwasababishia hasara kubwa ya kuungua nyumba zao pamoja na mali zilizokuwemo ndani yake.

Sambamba na tukio hilo, mfuasi mmoja wa Chama Cha Wananchi (CUF) Yashua Kawisa (21) ambaye ni mkazi wa kijiji cha Mbesa wilayani humo, naye amejeruhiwa vibaya kwa kukatwa mapanga, wakati akiwa katika kampeni za uchaguzi huo.


Taarifa za tukio hilo zinaeleza kuwa majeruhi huyo alikatwa panga, katika paji la uso na kukimbizwa katika hospitali ya Misheni Mbesa kwa matibabu zaidi. 

Akizungumzia mkasa huo ofisa mtendaji wa kata ya Mbesa Rasso Kundete, alisema kuwa majeruhi Kawisa alijeruhiwa na mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa serikali kitongoji cha Luwawa, anayefahamika kwa jina la Alex Mchopa wakati wakiwa katika mchakato wa kampeni za mwisho usiku wa kuamkia Disemba 14 mwaka huu.

Naye Mtendaji wa kata ya Ngapa, Zuberi Ngoma alisema kuwa chanzo cha matukio hayo kilisababishwa na vijana na wafuasi wa Chama Cha Wananchi (CUF) wilayani Tunduru, kukataa kupokea matokeo ya uchaguzi huo baada ya kuonekana kuwa mgombea wa CCM alikuwa ameibuka na ushindi baada ya kupata kura 350 huku wao wakiwa na kura 290.

Kamanda wa Polisi mkoani Ruvuma, Mihayo Msikhela amethibitisha kuwepo kwa matukio hayo na kueleza kuwa Polisi wanaendelea kufanya uchunguzi ili kuweza kuwapata watuhumiwa na chanzo cha matukio hayo.

Msikhela aliendelea kufafanua kuwa nyumba ya diwani Isaya ilichomwa moto mchana wa Desember 14 mwaka huu majira ya saa 8:30 mchana, na kwamba tukio la kuchomwa kwa nyumba ya Liugu lilitokea majira ya saa 2:00 usiku siku ulipofanyika uchaguzi huo.

Kuhusu tukio la majeruhi Alex Mchopa ambaye amelazwa katika hospitali ya Misheni Mbesa, alisema polisi wanaendelea kumtafuta mtuhumiwa kwa kushirikiana na askari wan chi jirani ya Msumbiji, ambako inadaiwa kuwa mtuhumiwa amekimbilia huko.

No comments: