Tuesday, December 16, 2014

MADIWANI MBINGA KUMSHTAKI MKURUGENZI KWA WAZIRI MKUU

Waziri mkuu, Mizengo Pinda.

Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

BAADHI ya Madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wanampango wa kwenda kumuona Waziri mkuu wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda kwa lengo la kufikisha kilio chao juu ya mgogoro ambao unaendelea kati ya mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo na Afisa elimu wa msingi wa wilaya hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wa habari hizi, Madiwani hao walisema kuwa wamechoshwa na mambo ambayo yanafanywa na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Mbinga, Hussein Ngaga kwa kuendekeza migogoro na mambo yasiyokuwa na tija katika jamii.

Aidha walifafanua kuwa Ngaga ameshindwa kuiongoza wilaya hiyo, kutokana na kuendekeza migogoro na afisa elimu msingi wa wilaya hiyo, Mathias Mkali na kuchukua hatua ya kumsimamisha kazi kinyume na taratibu za utumishi wa umma wakati hana makosa.


“Hata kama serikali imeunda tume na kuileta hapa kwetu kwa lengo la kuchunguza mgogoro huu, ni lazima tujipange tukamuone Waziri mkuu, huyu mkurugenzi hatumtaki kwa sababu hana nia njema ya kutuletea maendeleo sisi wanambinga, muda mwingi yeye ni mtu wa kupenda kujenga makundi ambayo hayana maelewano na wenzake”, walisema.

Aidha Madiwani hao walisema wilaya hiyo ambayo sasa ilionekana kufanya vizuri katika sekta ya elimu msingi, hivi sasa wana wasiwasi huenda ikashuka kielimu kutokana na mkurugenzi Ngaga kuendeleza malumbano hata na walimu mashuleni wakiwemo Waratibu elimu kata ambao muda mwingi walikuwa wakisimamia maendeleo ya watoto mashuleni.

Kufuatia hali hiyo walieleza kwamba, umefika wakati kwa serikali kuona umuhimu wa kumhamisha mkurugenzi huyo, ili kuweza kunusuru maendeleo ya wilaya ya Mbinga hususani katika sekta ya elimu ambayo inaonekana sasa kuanza kuyumba.

“Hivi sasa amefikia hatua ya kuhamisha walimu na waratibu elimu kata, katika vituo vyao vya kazi na kuwapeleka maeneo mengine, kwa nini hizi fedha anazotumia kuhamisha hawa watu asifanyie maendeleo mengine ya wanambinga”? walihoji.

Pamoja na mambo mengine waliongeza kuwa wamefikia mahali wamechoshwa na matendo yake, hivyo hawaoni sababu ya kuendelea kukaa na mkurugenzi ambaye muda mwingi anapenda kugombana na watendaji wake wa chini ambao wanasimamia maendeleo ya wananchi.

No comments: