Tuesday, December 9, 2014

DED MBINGA ALALAMIKIWA WAMTAKA AZINGATIE MAKUBALIANO YALIYOFANYWA NA WAZAZI

Hussein Ngaga, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma.










Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

AGIZO lililotolewa hivi karibuni na Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Hussein Ngaga juu ya michango wanayochanga wazazi kwa ajili ya watoto wao kujisomea wakati wa likizo (Makambi) wilayani humo, na kuingizwa kwenye akaunti ya fedha za ruzuku kutoka serikalini kwa ajili ya kuendeshea mitihani mashuleni (Capitation) limezua mapya, kufuatia kamati husika zinazojishughulisha na uendeshaji wa makambi hayo kulalamika wakidai kwamba, kufanya hivyo ni ukiukaji wa taratibu na makubaliano yaliyofanywa na wazazi kupitia vikao husika.
 
Imeelezwa kuwa ni vyema mkurugenzi huyo, akazingatia mawazo na makubaliano yaliyofanywa na wazazi hao na sio vinginevyo, hivyo kutozingatia hilo ni kukosa utawala bora katika jamii na kuleta migogoro isiyokuwa ya lazima.

Kwa nyakati tofauti walipozungumza na mwandishi wa habari hizi wajumbe wa kamati hizo walieleza kuwa, michango inayokusanywa kutoka kwa kila mzazi ambaye ana mtoto anayesoma katika shule husika, hukabidhiwa mkuu wa kambi na kamati hufanya kazi ya kupanga mapato na matumizi na sio utaratibu huo ambao mkurugenzi huyo ameutoa.

Walidai kuwa michango hiyo kuingizwa kwenye akaunti ya Capitation hivi sasa kunaleta kikwazo kikubwa kwao, hasa pale wanapohitaji kufanya matumizi husika kwani wanapokwenda kwa mkurugenzi huyo ili waweze kupata fedha hizo kwa ajili ya kuendeshea shughuli za watoto hao katika kambi, hukumbana na vikwazo vingi.

Walifafanua kuwa uendeshaji wa makambi hayo ni mfumo ambao wazazi wa wilaya hiyo walijiwekea mikakati yao wenyewe na kujenga makubaliano juu ya namna ya kuinua kiwango cha taaluma, kupitia vikao vya Mabaraza ya kata (WDC) ambapo makubaliano yao yalikuwa kila mchango unapokusanywa akabidhiwe mkuu wa kambi husika, kwa ajili ya kupanga matumizi na baadaye mwisho wa kambi taarifa ya mapato na matumizi itolewe kwenye kikao hicho cha WDC kwa eneo husika.


“Hapa tunavyozungumza kuna baadhi ya wenzetu ambao wameingiza michango hii kwenye akaunti ya Capitation, wakifuatilia fedha kwa mkurugenzi huyu ili waweze kwenda vijijini kwa ajili ya kuendeshea makambi, wanashindwa kuzipata kwa muda muafaka huku wakibaki wanasumbuka hawajui cha kufanya”, walisema.

Vilevile waliongeza kuwa kutokana na ukiritimba huo wa ucheleweshaji wa kutoa fedha kwa wakati kunasababisha baadhi ya makambi mashuleni, huko vijijini watoto hulala na giza katika eneo ambalo wameweka kambi, kutokana na kukosa fedha za kununua mafuta (Petroli) kwa ajili ya kuweka kwenye genereta.

Kutotolewa fedha hizo kwa wakati na kukosekana kwa mafuta hayo, watoto hao hivi sasa huko vijijini wanashindwa hata kujisomea nyakati za usiku, jambo ambalo walimu wengi wamesema kuwa huenda utaratibu huo aliouanzisha mkurugenzi Ngaga juu ya fedha hizo kuingizwa kwenye akaunti hiyo ya fedha za ruzuku kutoka serikalini, badala ya kukabidhiwa mkuu wa kambi husika na kupanga taratibu za matumizi ya kuendeshea masomo ya watoto wakati wa likizo kama ilivyokuwa awali, ndio mwelekeo wa kufa kwa makambi hayo na wilaya ya Mbinga huenda ikawa nyuma kielimu kwa shule za msingi kutokana na walimu wengi kuanza kukata tamaa ya kujitolea kufundisha.

Pia nimezungumza na Wazazi kwa nyakati tofauti nao walisema, wanamshangaa Mkurugenzi huyo kuanzisha taratibu za kwake bila kushirikisha wazazi wenye watoto kupitia vikao husika, ambapo walifafanua kuwa makubaliano yao kupitia vikao vya WDC haikuwa hivyo huku baadhi yao wakisema ni vyema mfumo wa kujisomea watoto wakati wa likizo, taratibu husika akaziacha kama wazazi walivyokubaliana katika vikao hivyo na sio kuzibadilisha ambapo asipofanya hivyo mbele wanaona giza kwa maendeleo ya watoto wao kielimu wilayani humo.

“Kiongozi mzuri ni yule ambaye anashirikisha wenzake na sio kuamua mambo yeye binafsi, kwa jambo hili tunamtaka afuate taratibu ambazo sisi wazazi kwa kushirikiana na walimu wetu kupitia vikao husika, tulikwisha kaa na kuweka mikakati madhubuti ya kufanikisha watoto wetu wakue kielimu hivyo tunasema hatuhitaji kurudishwa nyuma na mtu yeyote ambaye hana uchungu na maendeleo ya wanambinga”, walisema.

Walieleza kuwa michango wanayochanga wazazi kwa watoto wao ili wajisomee wakati huo wa likizo, sio mpango uliowekwa na serikali bali ni makubaliano yao na walimu mashuleni ambapo kufikia hatua ya kuingiza fedha hizo kwenye akaunti ya serikali ni kuingilia matakwa yao ambayo wamejiwekea wenyewe, hivyo wamemtaka aache kufanya hivyo badala yake afuate makubaliano ya vikao husika vya mabaraza ya kata.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga Hussein Ngaga alipotafutwa ili aweze kuzungumzia malalamiko hayo, hakuweza kupatikana na simu yake ilikuwa ikiita kwa muda mrefu bila kupokelewa.


No comments: