Saturday, December 6, 2014

WAFANYABIASHARA TUNDURU WALIA NA SERIKALI


Na Steven Augustino,

Tunduru.

WAFANYABIASHARA na walipa kodi wanaotakiwa kutumia mashine za kielektroniki (EFD'S) wilayani Tunduru mkoani hapa, wameiomba serikali inunue mashine hizo na kuzigawa bure kwa wafayabiashara hao, ili ziweze kusaidia serikali kukusanya kodi husika.

Ombi hilo limetolewa na wafanyabiashara hao wakati walipokuwa wakizungumza na maafisa waandamizi wanaosimamia ukusanyaji wa kodi, katika mkutano uliofanyika kwenye Ukumbi wa New generation uliopo mjini hapa.

Mfanyabiashara aliyejitambulisha kwa jina la Kazembe Said ndiye aliyeanza kufanya uchokonozi wa kupenyeza ombi hilo, na kuongeza kuwa pamoja na mambo mengine wao hawapingani na taratibu za ulipaji wa kodi, isipokuwa kinacho wakwaza ni kutokuwa na mitaji ya kutosheleza kununua mashine hizo.

Wakati wafanyabiashara hao wakionekana kuunga mkono ombi hilo naye Leonsi Kimario akaja na hoja ya kuisihi serikali, kuandaa utaratibu mzuri wa matumizi na mapato ambayo yamekuwa yakitokana na kodi za wananchi tofauti na sasa, ambapo kumekuwa kukitokea kashfa za matumizi mabaya ya fedha yakiwa yanazungumzwa mara kwa mara Bungeni.


Kimario aliendelea kufafanua kuwa endapo utaratibu huo utaachiliwa uendelee kulitafuna taifa hili, ipo hatari ya walipa kodi kuanza kugomea ulipaji wake hali ambayo itasababisha serikali kukosa mapato na kusababisha jamii yenye kipato duni, kuteseka kutokana na hata kukosa huduma za matibabu na mahitaji mengine muhimu ya kibinadamu ambayo serikali inapaswa kutoa huduma.

Awali akitoa maelekezo ya taratibu za ulipaji wa kodi hiyo kwa kutumia mashine za kielektroniki Afisa elimu kwa umma (TRA) mkoani Ruvuma, Justine Kititi pamoja na mambo mengine aliwataka walipa kodi wilayani humo, kuzingatia maelekezo ya ulipaji wa kodi ikiwa ni juhudi a kuinua pato la taifa.

Alifafanua kuwa faida za wafanyabiashara hao kutumia mashine hizo ni pamoja na kuwasaidia kutunza kumbukumbu katika biashara zao.

Akizungumzia upande wa hasara ambazo wanaweza kuzipata endapo watashindwa kuzitumia alieleza kuwa watapata hasara kwa kulipa kodi kubwa, pale watakapofanyiwa makadirio.

Hata hivyo  Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wilaya ya Tunduru Joshua Mwakatumbula alisema kwa sasa serikali haifanyi biashara, isipokuwa imetafuta wadau wa kushirikiana nao na mamlaka hiyo, kwa kutengeneza na kuuza mashine hizo kisha kuzisambaza kwa walengwa yaani wafanyabiashara.  

No comments: