Monday, December 15, 2014

KABROTHER KUINGIA SOKONI NA MKUKI KWA NGURUWE

Msanii Gidion Kabrother akisisitiza jambo, wakati alipokuwa akizungumza na Mkurugenzi wa mtandao huu, Kassian Nyandindi Mbinga mjini mkoa wa Ruvuma.

Hii ni moja kati ya Filamu yake ambayo aliitoa mara ya mwisho, ikitamba kwa jina la Ni Shida, ambayo ipo sokoni.
Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

MUIGIZAJI wa filamu nchini, Gidion Simon maarufu kwa jina la Kabrother anatarajia kutoa filamu yake mpya yenye picha kali, ambayo itatamba hivi karibuni kwa jina la Mkuki kwa Nguruwe hivyo wadau mbalimbali amewataka kukaa mkao wa kula na kuipokea albamu hiyo, kwa kuendelea kumuunga mkono kwa kazi zake.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Kabrother anasema filamu hiyo inazalishwa na kusambazwa na kampuni ya Pamoja Film, iliyopo Jijini Dar es Salaam.

Anafafanua kuwa filamu hiyo imebeba maudhui mazuri yenye kulenga kuelimisha jamii, ikiwemo inakemea vitendo vinavyofanywa na baadhi ya wafanyakazi mahospitalini wenye tabia ya kutibu wagonjwa, kwa kutumia madawa ambayo yamepitwa muda wake wa matumizi na kusababisha madhara kwa mtumiaji.

“Ndugu mwandishi katika matumizi ya madawa haya feki ni hatari sana, hata mkurugenzi husika mwenye hospitali hujikuta siku ya mwisho hata ndugu yake akiathirika na madawa hayo kwa sababu tu ya uzembe huu na kusababisha nguvu kazi ya taifa hili kupotea”, anasema Kabrother.

Pia filamu hiyo inaiasa jamii hasa kwa wale wenye kipato, kuacha tabia au matendo ya kuumiza wenzao kwa namna moja au nyingine kutokana tu, na hali ya uchumi mzuri walionao.


Kabrother uzoefu wake katika fani ya uigizaji wa filamu hapa nchini, amepitia kwenye vikundi vya sanaa vya Tamacaefo sunlight (Manyoni), Emima (Morogoro) na Best tallent (Shinyanga).

Kwa sasa anafanya kazi zake za usanii kwa kushirikiana na wasanii wakongwe hapa nchini Senga, Pembe, Kinyambe na Matumaini na kwamba Kabrother anatamba na filamu zake tatu ambazo tayari zipo sokoni zenye kufahamika kwa majina ya Exccident, Nimeshindwa na ile iitwayo Ni shida.

Pamoja na mambo mengine Gidion Kabrother licha ya kuwa msanii, pia ni mwalimu wa shule za msingi ambaye amebobea kwenye masomo ya Hisabati, Kingereza na Tekinolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT).

Kadhalika ni mtaalamu wa michezo ya mpira wa mikono (Hand ball) na mpira wa wavu (Volley ball), na kwamba kwa mtu yeyote yule ambaye anahitaji kupata filamu zake anaweza kufanya mawasiliano kwa kupiga simu ya kiganjani namba; 0757 947301.

No comments: