Tuesday, December 2, 2014

SONGEA WALALAMIKIA UBOVU WA DALADALA WAZITAKA MAMLAKA HUSIKA KUCHUKUA HATUA



Na Gideon Mwakanosya,
Songea.

BAADHI ya wakazi wa halmashauri ya Manispaa ya songea mkoa wa Ruvuma, wamezilalamikia  mamlaka husika zikiwemo kikosi cha usalama barabarani mkoani humo na  Sumatra kwa kushindwa kudhibiti daladala mbovu, zinazofanya kazi ya kubeba abiria katika manispaa hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakazi hao wameeleza kuwa kwa muda mrefu sasa, daladala ambazo zinaonyesha kuwa ni mbovu lakini zimekuwa zikiendela kubeba abiria zimekuwa zikihatarisha maisha ya abiria wanaotumia daladala hizo.

Felix Komba mkazi wa Mahenge alisema kuwa daladala zinazotoka Songea mjini mtaa wa Delux, kwenda Matogoro na Songea Boys zinaonekana hata kwa macho kuwa ni mbovu.


Said Athumani mkazi wa eneo la Matarawe amesema kuwa kwa muda mrefu wakazi wa maeneo hayo, na Mjimwema wamekuwa wakitumia daladala ambazo  ni mbovu na kwamba zimekuwa zikisheheni abiria, na wakati mwingine zikiwa kwenye eneo la mlima zinashindwa kupanda.

Ameziomba mamlaka zinazohusika kusimamia shughuli mbalimbali za vyombo vya moto mkoani humo, kuona umuhimu wa kuchukua hatua madhubuti na kuzisitisha daladala zote ambazo zinaonekana hazifahi kubeba abiria.

Kwa upande wake Afisa mfawidhi wa mamlaka ya udhibiti wa nchi kavu na majini (SUMATRA) mkoani Ruvuma, Sebastian Rohai alisema kuwa ofisi yake ilishapokea malalamiko kutoka kwa abiria na tayari zoezi la kukamata daladala mbovu zinazofanya kazi Manispaa ya songea, zimeshaanza tangu wiki iliyopita.

Kamanda wa polisi mkoa wa Ruvuma Mihayo Msikhela alisema kuwa tangu abiria  walipoanza kulalamikia ubovu wa daladala hizo, tayari kikosi cha usalama barabarani mkoani humo kimeshaanza kazi ya kukamata daladala zote ambazo inadaiwa kuwa ni mbovu.

Hata hivyo Mwenyekiti wa chama cha usafirishaji mkoa wa Ruvuma Golden Sanga, alipohojiwa kuhusiana na malalamiko ya baadhi ya daladala zinazotoa huduma katika maeneo ya njia za kutoka soko kuu kwenda Mjimwema, Soko kuu kwenda mkuzo, Delux kwenda Songea Boys na Delux kwenda Matogoro alisema kuwa ofisi yake kwa kushirikiana na mamlaka husika inayafanyia kazi malalamiko hayo.

No comments: