Thursday, January 1, 2015

WAHITIMU MAFUNZO YA JKT WATAKIWA KULINDA AMANI


Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama kushoto, akisalimiana na Mkuu wa  utumishi wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) makao makuu, Kanal Thomas Mbele, kabla ya kufunga mafunzo ya miezi mitatu ya kijeshi kwa vijana 985 operesheni miaka 50 ya muungano kwa mujibu wa sheria awamu ya pili mwak 2014 katika kikosi cha 842 KJ Mlale JKT, katikati ni kaimu mkuu wa Brigedi ya 410 Songea Kanal JJ Fulla.

Na Dustan Ndunguru,

Songea.

WAHITIMU wa mafunzo ya Jeshi la kujenga Taifa (JKT) nchini, wametakiwa kuwa mstari wa mbele katika kulinda na kudumisha amani tuliyonayo badala ya wao kuwa chanzo cha vurugu hususani, katika kipindi hiki ambapo taifa lipo katika mchakato wa kupata katiba mpya.

Naibu Waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi, Jenista Mhagama alitoa rai hiyo mwishoni mwa wiki iliyopita, wakatialipokuwa akifunga mafunzo ya miezi mitatu  ya kijeshi kwa wahitimu 985 wa kozi ya ualimu   Operesheni miaka 50 ya Muungano, kwa mujibu wa sheria awamu ya pili mwaka 2014 katika kikosi cha 842 KJ Mlale JKT  wilaya ya Songea mkoani Ruvuma.

Alisema serikali haikukosea kurudisha mafunzo ya JKT kwa vijana wanaomaliza vyuo,  kwani dhamira yake kubwa ni kutaka kuwaandaa na kuwajenga vijana hao kuwa viongozi bora, na wenye ari kubwa na  moyo wenye uzalendo kwa nchi yao.

Jenista pia aliwataka kukataa kutumika vibaya na watu wenye nia mbaya katika nchi, kwa kuwatumia kama ngazi ya wao kufanikisha mambo yao binafsi jambo ambalo litaweza kuhatarisha amani na utulivu uliodumu tangu nchi ipate uhuru mwaka 1961.


Serikali bado itaendelea kuwaandaa vijana kutoka maeneo mbalimbali hapa nchini, wanaomaliza elimu ya juu katika vyuo vikuu na vikosi vya jeshi, ili kuwa viongozi waadilifu watakaokuja kuwaongoza wengine kwa kuzingatia maadili mema ambayo hayatazua malalmiko kwa wananchi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo alifafanua kuwa, lengo lingine la mafunzo hayo ya JKT ni kumfanya kijana aweze kujitambua na kutambua majukumu yake ya kila siku katika maisha yake,  na kulitumikia taifa badala ya kuwa kijana anayetumia muda wake mwingi kukaa kijiweni bila shughuli yoyote  na kuanza kulalamika huku kukiwa na fursa nyingi za kiuchumi.

“Kwa kukosa uzalendo ndiyo maana baadhi ya vijana wengi nchini  hasa wale waliopata nafasi ya kuchaguliwa kufanya kazi katika maeneo ya vijijini, wengi  wao wamekataa kwenda huko kwa kukosa uzalendo  hivyo serikali haitarajii  tena kuona wahitimu wanaotoka katika vikosi vya jeshi la kujenga taifa, wanakuwa na tabia kama hii ya kushindwa kutumikia watanzania wenzao”, alisema.

Kadhalika aliwasihi wahitimu hao mara watakapofika katika vituo vyao vya kazi kuwa na moyo wa huruma kwa wanafunzi, pamoja na jamii itakayowazunguka  huku wakikumbuka kuwa serikali imetumia gharama kubwa  wakati wote wa mafunzo yao ya kijeshi, hivyo ni lazima waonyeshe uzalendo katika kulitumikia taifa lao.

Awali  wahitimu hao kupitia risala yao iliyosomwa na Julieth Soza, walisema kutokana na umoja na ushirikiano mzuri baina ya vijana, wakufunzi na viongozi kwa ujumla wamepata mafanikio  katika sekta ya ujanja wa porini, matumizi ya silaha na ramani, utimamu wa mwili, sheria za kijeshi, usalama na utambuzi wa usalama wa ndani, mafanikio mengine ni kuchimba mahandaki, uokoaji, elimu ya ukimwi, kupiga shabaha, kwata, uraia, uzalishaji mali, michezo na mbinu za kivita.

Naye mwakilishi Mkuu wa Jeshi la kujenga taifa ambaye pia ni Mkuu wa utumishi katika jeshi hilo, Kanal Thomas Mbele aliwapongeza  wahitimu hao kwa kuonyesha uvumilivu katika muda wote waliokuwa katika mafunzo hayo na kwamba jeshi hilo linatambua kuwa vijana hao wanakabiliwa na changamoto nyingi wanapokuwa mafunzoni.

No comments: