Monday, January 19, 2015

MBUNGE GAUDENCE KAYOMBO AENDELEA KUKALIA KUTI KAVU MBINGA



Gaudence Kayombo.
Na Mwandishi wetu,

Ruvuma.

WAFANYABIASHARA wa wilaya ya Mbinga mkoa wa Ruvuma, wametishia kutomchagua tena Mbunge wa Jimbo la Mbinga, Gaudence Kayombo kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenye uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu, kwa kile walichodai kwamba ameshindwa kuwatetea Bungeni na badala yake ameunga mkono ongezeko la kodi la asilimia 100. 

Aidha walisema Mbunge huyo mara kwa mara wanapomtaka azungumze na wafanyabiashara hao kupitia vikao mbalimbali, kwa lengo la kusikiliza kero zao amekuwa hajitokezi huku wakidai amekuwa akitoa sababu nyingi kwamba amebanwa na majukumu.

Hayo yalijiri walipokuwa wakizungumza kwenye kikao cha wafanyabiashara hao kilichoketi kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii (FDC) mjini hapa, na baadhi ya maofisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutoka makao makuu ya mamlaka hiyo na mkoa huo, mmoja wa wafanyabiashara hao, Benedict Luena alisema wameumizwa na Mbunge wao kushindwa kuwatetea kuhusu suala hilo. 


“Hatukumtuma bungeni kwenda kulala, bali kutuwakilisha kutokana na kutugeuka nasi tumejipanga kumwajibisha kwa namna yoyote ile, ikiwemo hata kumwangusha katika uchaguzi ujao kwani hatuwezi kuwa na mbunge asiyejali kero za wananchi wake,” alisema Luena.

Mfanyabiashara mwingine, Ally Mbunda alisema kwa muda mrefu wamekuwa wakiomba kukutana na mbunge huyo ili waweze kuzungumzia kero zao zinazowasumbua, lakini amekuwa akisema amebanwa na majukumu mengine.

Kayombo alipohojiwa kwa njia ya simu, alikiri kusikia malalamiko hayo lakini akashangazwa na taarifa hizo akisema, tangu kikao kilipomalizika hakuna viongozi wala wafanyabiashara waliomfuata kumweleza hatua zilizofikiwa juu ya kikao hicho.

Alisema anashangaa kwa nini malalamiko hayo yanatokea kipindi hiki cha kampeni, “siyo wafanyabiashara peke yao wanaopiga kura, kwanza sheria inapitishwa na wabunge wote na inatumika nchi nzima hivyo sioni haja ya wao kuniadhibu”, alisema Kayombo.

No comments: