Wednesday, January 14, 2015

TAMISEMI NAPATA SHIDA KUMUONA MKURUGENZI WENU WA MBINGA ANAPOENDELEA KUPANDIKIZA MIGOGORO NA SERIKALI KUWA KIMYA KUTOMCHUKULIA HATUA

Jumanne Sagini, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (OWM - TAMISEMI)

Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

KATIKA hali inayoonesha kwamba ni utendaji mbovu katika kuongoza sekta ya umma na kuendelea kupandikiza chuki miongoni mwa jamii, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani hapa, Hussein Ngaga ameendelea kulalamikiwa na baadhi ya Madiwani wake kwamba amekuwa akisambaza pesa (Rushwa) kwa lengo la kushinikiza madiwani hao wajenge hoja ya kumkataa Afisa elimu msingi wa wilaya hiyo, Mathias Mkali. Mtandao huu umeelezwa.

Kadhalika inadaiwa pia Gaudence Kayombo, Mbunge wa jimbo la Mbinga naye amekuwa akishiriki kwa namna moja au nyingine kushawishi baadhi ya Madiwani wamkatae afisa elimu huyo, kwenye kikao cha baraza la madiwani hao ambacho kitaketi mwishoni mwa mwezi huu.

Siri hiyo imevuja baada ya wengi wao wakishangaa na wengine kuchukizwa na kitendo hicho wakihoji kwa nini wanafanya hivyo, na kuwataka waachane na tabia hiyo ambayo huenda baadaye ikawageuka wao wenyewe na kuwaweka mahali pabaya.

Mwandishi wa habari hizi ameelezwa na vyanzo vyetu mbalimbali kuwa, kwa nyakati tofauti vikao vimekuwa vikifanyika ofisini kwa mkurugenzi huyo na hata nyumbani kwake, kupanga mikakati ya kuhakikisha jambo hilo linafanikiwa kwa njia yoyote ile.


Mwenyekiti wa Kamati ya elimu afya na maji katika baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya ya Mbinga, James Yaparama amekiri kupokea taarifa hizo kutoka kwa baadhi ya madiwani wenzake na kusema tabia hiyo wanayoifanya sio nzuri huku akidai kuwa fedha wanazotumia kuwagawia madiwani hao, huenda zikawa ni kodi za wanambinga ambazo ilibidi zikafanye shughuli nyingine za maendeleo ya wananchi. 

“Huyu Mkurugenzi sisi tunamshangaa sana, tokea muda mrefu wakati anaanzisha ugomvi huu na kufikia kumsimamisha kazi mwenzake (Afisa elimu msingi) bila kufuata taratibu, mara nyingi amekuwa akitumia nguvu kubwa ya pesa kutaka tu kumkandamiza mwenzake wakati hana kosa lolote na hivi anavyofanya mwisho wake nini”?, alihoji James.

Gaudence Kayombo alipoulizwa juu madai hayo alisema, “huna haja ya kuniuliza kwa hayo unayosema, wewe tabia yangu unaifahamu, na kuishia kukata simu”.

Kadhalika kwa nyakati tofauti mwandishi wetu amezungumza na baadhi ya wadau mbalimbali wa elimu wilayani Mbinga, wamesema kuwa Taasisi ya kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wilayani humo licha nayo kupelekewa malalamiko mengi juu ya mwenendo mbaya wa mambo mbalimbali ya utumishi wa umma, yanayoendelea kufanywa katika halmashauri hiyo hakuna hatua zilizochukuliwa na kuzaa matunda hadi sasa.

Walisema katika wilaya ya Mbinga taasisi hiyo ni sawa kama imeenda likizo, hivyo ni vyema serikali ikachukua hatua nyingine ya kushughulikia matatizo ya wananchi wilayani humo, lakini sio kwa hali hiyo ambayo inaendelea kuumiza wananchi.

Hivi karibuni waandishi wa habari walipozungumza na Kamanda wa TAKUKURU wa wilaya hiyo, Ditram Mhoma ili aweze kuzungumzia juu ya madai hayo ya wananchi kwamba taasisi hiyo imeenda likizo haishughulikii malalamiko yao ipasavyo, alisema sio kweli wao wanafanya kazi hawana mchezo na mtu.

Kwa upande wa watu kumlalamikia Mkurugenzi mtendaji wa Mbinga Bw. Ngaga, kamanda huyo wa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa alikiri kupokea malalamiko hayo na kuonekana akimtetea akisema ni kiongozi mzuri, ambaye hana matatizo katika kuwaongoza wananchi.

“Kaka naomba niwaelezeni, huyu Mkurugenzi wa Mbinga ni mzuri sana tunafanya naye kazi vizuri na anatupatia ushirikiano wa kutosha pale tunapofanya kazi zetu”, alisema Mhoma.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga Hussein Ngaga alipotafutwa ili aweze kutolea ufafanuzi juu ya malalamiko hayo, hakuweza kupatikana na simu yake ilikuwa ikiita kwa muda mrefu bila kupokelewa, na imekuwa ni tabia yake ya kutopokea simu na kukataa kuhojiwa na waandishi wa habari.

No comments: