Monday, July 22, 2013

BREAKING NEWS: PADRE WA KANISA KATOLIKI PERAMIHO SEMINARI JIMBO LA SONGEA, ABURUTWA MAHAKAMANI KWA KUMPATIA HONGO MKUU WA WILAYA YA MBINGA

Padre Xavery Kazimoto Komba  wa Peramiho Seminari jimbo la Songea, akiwa amegeuza mgongo kwa lengo la kuficha sura yake, wakati Waandishi wa habari wakimpiga picha alipokuwa eneo la Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, akisubiri kusomewa mashtaka yake.(Picha na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

MAPYA yameibuka juu ya sakata la Padre mmoja wa Kanisa Katoliki hapa nchini, Peramiho Seminari jimbo la Songea mkoani Ruvuma, Xavery Kazimoto Komba ambaye alikamatwa na kuwekwa mahabusu, leo amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani humo, kwa tuhuma ya kutoa hongo ya shilingi milioni 1 kwa Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga, kwa lengo la kumshawishi asichukuliwe hatua kwa makosa aliyofanya ya kuwatapeli baadhi ya wakulima wa kahawa wilayani humo.

Padre huyo anatuhumiwa kufanya utapeli huo kwa kutumia kampuni yake ambayo hujishughulisha na kununua kahawa, inayofahamika kwa jina la Songea network Company Limited ambayo yeye ndiye Mkurugenzi wa kampuni hiyo.

Inadaiwa kuwa Kasisi huyo wa kanisa Katoliki alikamatwa na kuswekwa mahabusu katika Kituo kikuu cha Polisi wilayani humo, mapema Julai 19 mwaka huu majira ya mchana, kufuatia kutoa hongo ya fedha hizo kwa kutumia utaratibu wa M – pesa kwenda namba ya simu ya Mkuu wa wilaya hiyo ambazo mahakamani hapo hazikutajwa.

Ilidaiwa Mahakamani hapo na Mwendesha mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU) mkoani Ruvuma, Bi. Maria Mwakatobe mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wa wilaya ya Mbinga, Geofrey Mhini kuwa Xavery Kazimoto Komba anadaiwa kufanya kosa hilo Mei 20 mwaka huu na Mei 26 mwaka huu katika majira tofauti.

Mwakatobe aliendelea kudai kwamba Padre huyo anatuhumiwa mnamo Mei 20 mwaka huu alituma kiasi cha shilingi 400,000 na Mei 26 mwaka huu alituma tena shilingi 600,000 kwenda namba ya simu ya Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, akiwa na lengo la kumshawishi mkuu wa wilaya hiyo asimchukulie hatua kufuatia shauri ambalo lilikuwa kisheria katika ofisi yake.


Mwendesha mashtaka huyo wa TAKUKURU aliieleza mahakama kwamba upelelezi wa shauri hili umekamilika, hivyo dhamana kwa mshtakiwa ipo wazi na kuitaka mahakama ifuate mkondo wake wa kisheria.

Kabla ya Hakimu mkazi wa mahakama hiyo kutoa masharti ya dhamana upande wa utetezi wa mshtakiwa uliomba kupewa nafuu ya dhamana ambapo, hakimu mkazi mfawidhi, Mhini alisema dhamana kwa mshtakiwa Xavery Kazimoto Komba ipo wazi kwa masharti ya mdhamini mmoja mwaminifu mwenye uwezo wa kuweka “bondi” ya shilingi milioni 3.

Ambapo baada ya tukio hilo mdhamini aliyeandaliwa na ndugu wa mshtakiwa kwa ajili ya kumdhamini, alijitokeza Mahakamani hapo na kujitambulisha kwa jina la Prosper Mahay, akiwa na barua za utambulisho kutoka kwa Mwenyekiti wa mtaa anaoishi hapa Mbinga mjini na vielelezo vingine vya umiliki wa nyumba yake moja, iliyopo kitongoji cha Manzese hapa Mbinga mjini.

Mdhamini huyo baada ya kutoa vielelezo hivyo, mahakama iliriridhia na kutoa dhamana kwa mshtakiwa, na kupanga tena siku ya shauri hilo ambalo litakuja kwa ajili ya kusomwa maelezo ya awali mahakamani hapo Agosti 12 mwaka huu.

No comments: