Monday, July 22, 2013

WANACHAMA WA CWT MBINGA WAUJIA JUU UONGOZI WA WILAYA, WATISHIA KUJITOA UANACHAMA

Katibu wa CWT wilayani Mbinga, Samwel Mhaiki.




















Na Mwandishi wetu,

Mbinga.

KATIKA hali inayoonesha kuwa ni matumizi mabaya ya madaraka na ukiukaji wa taratibu na sheria za utumishi wa umma, Katibu wa Chama Cha Walimu Tanzania(CWT) tawi la Mbinga mkoani Ruvuma, Samwel Mhaiki ananyoshewa kidole na wanachama wa chama hicho wilayani humo, akidaiwa kutowalipa baadhi ya wanachama fedha zao  zinazotokana na asilimia 15 ya makato yatokanayo na mishahara yao ya kila mwezi.

Wamezungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti wilayani hapa, wakisema Katibu huyo amekuwa akifanya kitendo hicho, kwa kushirikiana na Mwenyekiti wake wa wilaya hiyo Batson Mpogolo.

Pia wanachama hao wengi wao wametishia kujiondoa uanachama katika umoja huo na kusema wakisha kamilisha mchakato huo wa kujitoa, wapo tayari kwenda kufungua kesi Mahakamani dhidi ya Katibu wao wa wilaya hiyo na Mwenyekiti, ili waweze kulipwa fedha zao wanazodai.

Vilevile viongozi hao wa CWT wamekuwa wakilalamikiwa kwamba, ni zaidi ya miezi 20 sasa walimu wengi waliopo wilayani Mbinga hawajalipwa fedha hizo.

Kadhalika muda mwingi wamekuwa wakionekana wakiwa safarini kuelekea Manispaa ya Songea hususani kwa siku za mapumziko yaani Jumamosi na Jumapili kwa kutumia wakati mwingine gari la chama la wilaya hiyo.

Kitendo hicho cha kusafiri mara kwa mara katika siku za kazi na kwenda huko, walieleza wakidai kuwa wanamashaka na safari zao wanazozifanya na huenda wakawa wanafuja fedha hizo kwa kufanya starehe au kwa manufaa mengine binafsi.

“Hizi safari za mara kwa mara zinatutia mashaka, huenda huko wanakula bata kwa kutumia fedha zetu hizi za makato ya kila mwaka lakini viongozi wetu wa CWT mkoa na taifa wapo kimya wameziba masikio hakuna hatua iliyochukuliwa licha ya sisi wanachama kulalamika kwa muda mrefu”, walisema.


Aidha walimu hao walifafanua kuwa viongozi hao wamekuwa muda mwingi wakipita katika matawi yao mashuleni huko vijijini, na kufanya usanii wa danganyatoto kwa kuonyesha wanawapenda wanachama   wao matawini pale wanapowatembelea.

Wakati mwingine wanapopita huko matawini wanadaiwa kupita kuhamasisha migomo isiyokuwa na msingi wowote, ambayo hujenga ugombanishi kati ya serikali na mwajiri wao.

Pamoja na mambo mengine walieleza kuwa wamechoshwa na vitendo hivyo na kuahidi kwamba wanachohitaji ni kuona makato yao yanarejeshwa kwa mujibu wa taratibu za chama zinavyosema na sio vinginevyo.

Hata hivyo Mwandishi wetu hivi karibuni, alipomuuliza Katibu wa CWT wa wilaya ya Mbinga Samwel Mhaiki ili aweze kutolea ufafanuzi juu ya tuhuma hizo alisema, yeye hakuna mwalimu anayemdai na malipo kwa wanachama wake yamekwisha lipwa lakini pia alipotafutwa Mwenyekiti wake Batson Mpogolo, hakuweza kupatikana na simu yake muda mwingi ilikuwa imefungwa.

No comments: