Wednesday, July 17, 2013

WAZIRI MKUU AENDELEA NA ZIARA YAKE MKOANI RUVUMA, SASA YUPO WILAYANI NYASA

Waziri Mkuu Mizengo Pinda, akiwa katika kazi za ujasiriamali.

















Na Kassian Nyandindi,

Nyasa.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda leo anaendelea na ziara yake mkoani Ruvuma, ambapo kwa sasa yupo wilaya ya Nyasa na atapokea taarifa ya maendeleo ya wilaya hiyo, katika kata ya Lituhi wilayani humo.

Mkuu wa wilaya hiyo Ernest Kahindi akizungumza na mwandishi wa habari hizi, alisema baada ya Waziri huyo kusomewa taarifa hiyo, ataelekea katika kata ya Kihagara na kuweka jiwe la msingi kituo cha afya Kihagara, kilichopo wilayani humo.

Vilevile Pinda baada ya hapo atafungua skimu ya mradi wa umwagiliaji Lundo na jengo la Karakana lililopo katika mji wa Mbamba bay wilayani Nyasa, ambalo linatumika kwa ajili ya kutengenezea boti za kisasa.

Kadhalika Kahindi alisema akitokea hapo ataelekea katika eneo maalum ambalo limeandaliwa katika mji huo, kwa ajili ya kufanya uzinduzi wa wilaya ya Nyasa ambapo uzinduzi utaenda sambamba na kuzindua boti moja kubwa, ambalo litatumika kwa ajili ya shughuli za uvuvi.


Pamoja na mambo mengine Waziri Pinda baada ya kumaliza ziara yake ya kikazi katika wilaya ya Nyasa, ataelekea wilaya ya Mbinga ambako ameandaliwa kwa ajili ya mapumziko.

Siku inayofuata kiongozi huyo ataelekea mkoani Mtwara kwa ajili ya shughuli ya kikazi, na atarejea tena wilayani Mbinga.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, alisema Waziri Pinda ataendelea na ziara yake wilayani Mbinga ifikapo siku ya Jumapili, Julai 21 mwaka huu kuanzia majira ya saa nne asubuhi.

Atakapokuwa wilayani humo atasomewa taarifa ya maendeleo ya wilaya na kuendelea na ziara yake, atatembelea na kwenda kuweka jiwe la msingi katika kituo cha kuzalisha umeme wa maji,  ambacho kinamilikiwa na mzawa ambaye ni mkazi mmoja wilayani humo, aitwaye Menas Andoya.

Pia ataweka jiwe la msingi katika ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi ambayo inaendelea kujengwa mjini hapa, na baadaye kutembelea eneo la kituo cha kufua umeme(TANESCO Power House) na hatimaye atahutubia  wananchi.

No comments: