Tuesday, July 23, 2013

UWANJA WA MAONI: CWT MBINGA TUMEPOTEZA MWELEKEO NA MALENGO YA CHAMA TUSIHANGAIKE KUZIBA JUA KWA UNGO

Mwenyekiti wa CWT Taifa, Grattian Mukoba.

 

















Na Kassian Nyandindi,

VIONGOZI wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Mbinga mkoani Ruvuma, wanalalamikiwa na walimu ambao ni wanachama wa chama hicho wilayani humo, kwa kutowalipa fedha za marejesho ya asilimia 15 kutoka kwenye makato ya mishahara yao.

Nionavyo kwa hakika hii ni dharau na dhuluma ni vyema sasa wahusika wachukuliwe hatua kwa kutotimiza wajibu wao ipasavyo kwa wanachama hao.

Nahoji, Katibu wa CWT na Mwenyekiti wako mnafanya nini, hizi fedha mmezipeleka wapi? tunaomba sasa tupate majibu ili tuweze kujiridhisha juu ya malalamiko haya.

Ni malalamiko ambayo sasa yamedumu kwa muda mrefu, wanachama nimezungumza nao baadhi yao kwa nyakati tofauti wanasikitika wakisema wengine ni zaidi ya miezi 24 hadi 30 fedha zao wengi wao bado hawajalipwa.

Hii ni dhambi jasho la mtu huwa halipotei bure ni vyema sasa tukawa wastaarabu kwa kuchukua hatua mapema, katika kunusuru hali hii ambayo mbele tunaweza tukatengeneza shimo la kutumaliza wenyewe.

Uongozi wa namna hii haufai katika jamii, kila kukicha wanachama wamekuwa wakikinyoshea kidole CWT Mbinga, ni dhahiri sasa tunaonesha udhaifu katika utendaji wetu wa kazi, yatupasa sasa tubadilike !

Zama za watu kudanganywa na kupigwa danadana zimepitwa na wakati, kwa hili la marejesho ya makato ya mishahara ya walimu ni vyema tukae mezani na kulifanyia kazi haraka.

Nimeambiwa na wanachama wengi kwamba endapo suala hili litaendelea kuwa sugu, wametishia kujitoa uanachama, nasema endapo itakuwa hivyo hili litakuwa ni pigo kubwa kwa uongozi wa chama cha walimu Mbinga, na jamii sasa itatucheka na kutuzomea hata tutakapokuwa tukipita barabarani.

Kumekuwa na hata tabia ya kupakana matope na kumchafua ofisa elimu wa wilaya hiyo Mathias Mkali, kuwa anahamasisha walimu wajitoe, nimefanya mahojiano na baadhi ya walimu wanasema wao ni waelewa na wana akili timamu hawawezi kuhamasishwa na mtu mmoja juu ya kujitoa katika chama hicho, bali wanachohitaji ni kulipwa madai yao ya makato ya mishahara yao kila mwezi.

Wengine walisema huyo ofisa elimu tangu amekuja hapa wilayani ameweza kuhakikisha stahili zao za msingi ikiwemo uhamisho, likizo, matibabu na masomoni wamelipwa kwa wakati; tofauti na siku za nyuma walikuwa wakipata shida.

Wengine wamefafanua kwamba Mkali amekuwa ni mtu msikivu pale    wanapokuwa na shida zao za msingi, na amekuwa akihimiza utendaji bora wa kazi mashuleni.

Wanasema leo wanashangaa kuona maneno hayo yanatoka wapi, kwa ujumla viongozi wa CWT Mbinga wamepoteza mwelekeo na malengo ya chama hicho, sasa wanahangaika kuziba jua kwa ungo, ukweli upo bayana tunachohitaji hapa walimu walipwe madai yao ya msingi.

Wahenga walisema, Cheo ni dhamana hivyo hatuna budi kuihudumia jamii iliyotuweka madarakani, kwa misingi ya utawala bora ili tuweze kuondoa malalamiko na mitafaruku isiyokuwa na tija.

Katibu wa CWT uliopo Mbinga, sote tunafahamu ndiyo mtendaji mkuu wa kuliongoza jahazi hili la chama hapa Mbinga, sasa kama matatizo haya yanaendelea kweli tutafika?.....tubadilike.

Yawezekana viongozi wa ngazi ya mkoa na taifa, mmefumbwa macho na uongozi wa CWT wilaya ya Mbinga ! ndio maana hakuna hatua zinazoonesha kuzaa matunda licha ya malalamiko haya kudumu kwa kipindi kirefu sasa. Ama kweli tunaweza kusema ufisadi upo kila kona !
  
Nashauri kilio hiki cha wanachama wa chama hicho hapa wilayani ni vyema kikafanyiwa kazi haraka, ikiwezekana hata viongozi wa ngazi ya juu serikalini ingilieni kati suala hili ili wanachama husika waweze kupata haki zao za msingi, vinginevyo tukiendelea kufumbia macho hatutawatendea haki wanakondoo hawa wa Mbinga, ambao kilio chao kimedumu kwa muda mrefu sasa…….. tuchukue hatua.

Mungu ibariki Mbinga na Tanzania kwa ujumla,   

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa simu namba 0762578960.

No comments: