Sunday, March 19, 2017

RC RUVUMA AGEUKA MBOGO MHANDISI MSHAURI ANUSURIKA KUMWEKA MAHABUSU

Gari la halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma lenye namba STK 7456 likipita kwa shida katika barabara ambayo alipewa kujenga kwa kiwango cha lami kutoka kijiji cha Longa, Kipololo hadi Litoho wilayani humo Mkandarasi wa Kampuni ya Canopies International Tanzania Limited ya Jijini Dar es Salaam na G'S Contractors Company Limited ya kutoka mkoani Iringa tangu mwaka 2015 ambapo ilitakiwa kukamilika ujenzi wake mwaka jana lakini hadi sasa bado haijakamilika na kusababisha kero kubwa kwa watumiaji wa barabara hiyo.

Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida Salum Mjema ambaye ni Mhandisi mshauri na mkaguzi mkuu wa kazi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kijiji cha Longa, Kipololo na Litoho wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma ambayo imefadhiliwa na Jumuiya ya nchi za Ulaya (EU) amenusurika kuwekwa mahabusu na Mkuu wa mkoa huo, Dkt. Binilith Mahenge kwa madai kwamba ameshindwa kusimamia ipasavyo na kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo kwa wakati uliopangwa.

Mkuu huyo wa mkoa aligeuka na kuwa kama mbogo wakati alipokuwa akikagua barabara hiyo juzi kufuatia taarifa iliyomfikia ofisini kwake kwamba mradi huo umekuwa ukisuasua ujenzi wake, licha ya kazi hiyo kupewa wakandarasi wawili wa Kampuni ya Canopies International Tanzania Limited na G’S Contractors Company Limited kushindwa kujenga kwa tabaka la lami barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 24.954 katika kipindi cha kuanzia Septemba 30 mwaka 2015 hadi Desemba 30 mwaka 2016.

Dkt. Mahenge alionekana kuwa mkali na kusikitishwa na hali hiyo huku akishangazwa na wakandarasi hao kulipwa fedha kwa baadhi ya kazi walizofanya huku hatua ya utekelezaji ikiwa bado haijakamilika kwa viwango vinavyotakiwa.

“Hivi sasa naweza nikawaweka ndani tokea barabara hii ianze kujengwa hadi sasa haijakamilika, naagiza viongozi ngazi ya mkoa na wilaya ya Mbinga kwa kushirikiana na Katibu tawala wa mkoa huu fanyeni uchunguzi wa kina juu ya kazi hii ikiwemo na malipo yaliyofanyika, kwani inaonesha ni uchakachuaji mtupu umefanyika na tukibaini haya maovu mliyoyafanya tutawaweka ndani wote watakaokuwa wamehusika kuhujumu mradi huu na kuwafikisha kwenye vyombo vya kisheria”, alisema Dkt. Mahenge.

Saturday, March 18, 2017

BUNDI ATUA KWA OFISA USHIRIKA MBINGA MKUU WA WILAYA ASEMA ANACHUNGUZWA ATACHUKULIWA HATUA KALI ZA KINIDHAMU

Na Kassian Nyandindi,        
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye amesema kwamba serikali wilayani humo inaendelea kufanya uchunguzi juu ya malalamiko anayolalamikiwa Kaimu Ofisa ushirika wa wilaya hiyo, Kanisius Komba ambayo yanatoka kwa wakulima wa vyama vya ushirika wilayani hapa na pale itakapobainika kuna ukweli juu ya tuhuma anazonyoshewa kidole na wakulima hao hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yake.
Cosmas Nshenye.

Aidha Nshenye alifafanua kuwa wakulima wengi wamekuwa wakimtuhumu kwamba amekuwa hatimizi majukumu yake ya kazi za ukaguzi wa vyama hivyo ipasavyo, badala yake anadaiwa kushirikiana na viongozi wa vyama vya ushirika kuhujumu vyama hivyo visiweze kusonga mbele kimaendeleo.

Kadhalika alidai kuwa wanaushirika hao wamekuwa wakimtuhumu kwamba ni mtu ambaye anapenda kushiriki katika vitendo vya rushwa na kupotosha ukweli wa ripoti za ukaguzi wa vyama hivyo.

Hayo yalisemwa na Mkuu huyo wa wilaya ya Mbinga, Nshenye alipokuwa akizungumza juzi na waandishi wa habari ofisini kwake ambapo aliongeza kuwa amekuwa akitoa taarifa hizo za ukaguzi ambazo wakati mwingine hazina viambatanisho vyenye kuonesha uhalisia wa ukaguzi uliofanyika.

“Hamna pasipo na ushirika Mbinga hii asipolalamikiwa, suala hili lipo tunaendelea kulichunguza taarifa za ukaguzi amekuwa akizifanyia ujanja ujanja na amekuwa sio mtu mkweli katika masuala ya ukaguzi analalamikiwa na watu wengi”, alisema Nshenye.

MRADI WA MAJI KIGONSERA WAHARIBIWA NA MAFURIKO YA MVUA


Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa mafuriko ya mvua yaliyosababisha kuzolewa kwa mradi wa maji Kigonsera uliopo katika kata ya Kigonsera wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, uharibifu uliotokea umesababisha hasara ya shilingi milioni 15,000,000 ikiwa ni gharama sasa inayotakiwa kufidia ujenzi wa miundombinu ya maji ambayo imeharibika.

Kaimu Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Yohanes Nyoni alisema hayo alipokuwa akitoa taarifa kwa waandishi wa habari juu ya tukio hilo ambapo alieleza kuwa lilitokea Machi 6 mwaka huu katika kata hiyo.

Nyoni alifafanua kuwa sababu kubwa iliyosababisha mradi huo kuharibiwa na mafuriko hayo inatokana na uchafuzi wa mazingira katika chanzo hicho cha maji kwani baadhi ya wananchi wameweka makazi ya kudumu karibu na chanzo na kuendesha shughuli za kilimo.

Alisema kuwa hali hiyo husababisha nyakati za masika udongo kumomonyoka hatimaye matope hujaa kwenye chanzo na mawe makubwa yaliyobebwa na mafuriko kuvunja miundombinu husika ya mtego wa maji kutokana na kukosekana kwa uimara wa ardhi.

Wednesday, March 15, 2017

BREAKING NEWS: OFISA USHIRIKA HALMASHAURI WILAYA YA MBINGA ABURUTWA MAHAKAMANI AKIDAIWA PEMBEJEO ZA WAKULIMA

Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

KAIMU Ofisa ushirika wa Halmashauri wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Kanisius Komba (36) leo amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya mwanzo Mbinga mjini wilayani humo, kwa tuhuma ya madai ya pembejeo za kilimo zenye thamani ya shilingi milioni 3,000,000.

Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Beatrice Mbafu alidai Mahakamani hapo kuwa mshtakiwa Komba alitenda kosa hilo katika kipindi cha mwezi Januari mwaka huu baada ya kushindwa kuwafikishia mifuko 100 ya mbolea aina ya UREA na SA wakulima wa vikundi vya VICOBA vilivyopo wilayani humo.

Ilidaiwa kuwa Ofisa ushirika huyo aliwaambia wakulima hao waingize fedha hizo kwenye akaunti namba 70810002597 benki ya NMB kwenda kwa Kampuni ya IWAWA Agrovet and General Supply iliyopo Jijini Dar es Salaam, ili waweze kupatiwa pembejeo hizo lakini mpaka sasa hawakuweza kupewa mbejeo zenye thamani ya fedha hizo.

MKANDARASI UJENZI WA BARABARA YA NAMTUMBO HADI TUNDURU ALIFUKUZWA NA SERIKALI KUTOKANA NA KUSHINDWA KUTEKELEZA MAJUKUMU ALIYOPEWA

Na Muhidin Amri,      
Songea.

WAKALA wa Barabara (TANROAD) mkoani Ruvuma amesema kwamba kuanzia mwezi Januari mwaka 2013 hadi kufikia Januari mwaka huu, ametumia jumla ya shilingi bilioni 2,011,195,000 ikiwa ni gharama ya ulinzi wa mitambo iliyoachwa na Mkandarasi wa Kampuni ya Progressive Higleig ya kutoka nchini India.

Imeelezwa kuwa gharama hizo zimetokana na kuwalipa askari Polisi waliokuwa wakilinda mitambo ya kampuni hiyo katika maeneo mbalimbali ya mradi kwa kipindi cha miaka minne, baada ya serikali kumfukuza mkandarasi huyo kutokana na kushindwa kujenga barabara ya kutoka wilaya ya Namtumbo hadi Tunduru mkoani hapa kwa kiwango cha lami.

Meneja wa TANROAD wa mkoa huo, Razack Alinanuswe alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake na kuongeza kuwa serikali imeingiza shilingi bilioni 4,319,452,900 baada ya kuuza mitambo hiyo kwa njia ya mnada kwa watu binafsi na taasisi mbalimbali.

Alisema kuwa baada ya serikali kumfukuza mkandarasi huyo kutokana na kushindwa kwake kufanya kazi hiyo aliyopewa, ililazimika kushikilia mitambo yake na Wakala huyo wa barabara mkoani hapa na kubeba jukumu la kuilinda kwa muda wote kwa kutumia Jeshi la Polisi ambalo lilifanya kazi kwa uadilifu mkubwa licha ya kuwepo kwa baadhi ya changamoto mbalimbali.

Tuesday, March 14, 2017

RC RUVUMA AWATAKA VIONGOZI KUDHIBITI MATUMIZI YA POMBE AINA YA KIROBA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge.
Na Muhidin Amri,  
Songea.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge amewataka viongozi kuanzia ngazi ya vitongoji hadi wilaya, wahakikishe kwamba wanadhibiti kikamilifu matumizi ya pombe zilizofungashwa kwenye mifuko maarufu kama Kiroba ili zisiweze kuonekana mitaani zikiendelea kutumika, ikiwa ni lengo la kuokoa maisha ya Watanzania wengi hasa vijana walioathirika na matumizi ya pombe hizo.

Aidha amewataka viongozi hao pia wahakikishe kwamba kila wanapopata fursa ya kukutana na wananchi, watoe elimu kuhusiana na madhara yatokanayo na kiroba ambapo kwa kiwango kikubwa pombe hiyo imekuwa ikisababisha madhara makubwa katika jamii.

Dkt. Mahenge alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, ambapo alieleza kuwa matumzi ya viroba yamekuwa yakichochea pia ongezeko la matukio ya uhalifu na ajali barabarani, hasa kwa zile zinazotokana na waendesha pikipiki maarufu kwa jina la bodaboda na kusababisha watu wengi kuumia, kupoteza viungo vyao vya mwili kuwa walemavu huku wengine wakipoteza maisha yao.

SERIKALI MKOANI RUVUMA YATENGA MILIONI 335.6 KWA VIKUNDI VYA VIJANA

Na Kassian Nyandindi,    
Songea.

KATIKA kuhakikisha kwamba serikali inaendelea kuviwezesha vikundi vya vijana na wanawake hapa nchini, mkoa wa Ruvuma kupitia halmashauri zake nane zilizopo mkoani humo imetenga shilingi milioni 335.6 kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017 ili vikundi hivyo viweze kujiinua kiuchumi na kusonga mbele kimaendeleo.

Katika fedha hizo tayari mikopo ya shilingi milioni 90.5 imetolewa kwa vikundi vya vijana 2,619 vyenye wanachama 1,292 ambao wamenufaika na mikopo ya fedha za mfuko wa maendeleo ya vijana pamoja na fedha za mapato ya ndani ya halmashauri husika ndani ya mkoa huo.

Mkoa wa Ruvuma unakadiriwa kuwa na vijana 672,540 sawa na asilimia 48 ya wakazi wa mkoa huo wapatao milioni 1,376,891 kulingana na sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 na wastani wa ongezeko la watu kila mwaka.

Hayo yalisemwa na Kaimu Katibu tawala wa mkoa huo, Bwai Biseko alipokuwa akitoa taarifa ya shughuli za maendeleo ya vijana mkoani hapa kwenye mafunzo elekezi ambayo yalijumuisha vijana hao kutoka mikoa mitatu ya Ruvuma, Lindi na Mtwara yaliyofanyika katika Manispaa ya Songea mjini hapa.

Sunday, March 12, 2017

KAMPUNI YA OVANS YAPONGEZWA KWA KUUNGA MKONO JITIHADA ZINAZOFANYWA NA SERIKALI

Mitambo ya Kampuni ya Ovans Construction Limited,  ikiendelea na kazi ya ujenzi uwanja wa michezo shule ya msingi Kiwanjani uliopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

KATIKA kuhakikisha kwamba jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali ya awamu ya tano hapa nchini zinaendelea kuungwa mkono, Kampuni ya Ovans Construction Limited iliyopo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma imejitokeza na kutoa mchango wake wa kukarabati uwanja wa michezo wa shule ya msingi Kiwanjani uliopo mjini hapa kwa manufaa ya jamii.

Aidha imefafanuliwa kuwa lengo la kuukarabati uwanja huo ni kuufanya uweze kuwa wa kisasa zaidi ambapo utaendana na zoezi la uoteshaji nyasi kwa mfumo wa kisasa, ili wanafunzi wa shule hiyo na vijana wa kutoka Mbinga mjini waweze kucheza mpira wa miguu na kufanya mazoezi mbalimbali ya viungo vya mwili.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Vallence Urio akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake amesema kuwa kampuni yake imetoa mchango wa vifaa kama vile Caterpiller, Roller, Dumper truck na Exacavator ambavyo vinatumika kwa ajili ya kuchimba udongo na kusawazisha uwanja huo.

Vallence aliongeza kuwa baada ya kumaliza kusawazisha pia wataushindilia vizuri na kuupanda nyasi ambazo zitapandwa kitaalamu na kwamba zikisha kua na kufikia kiwango bora kinachofaa zitakatwa kwa mashine maalumu tayari kwa uwanja huo kuuweka katika maandalizi ya kuanza kutumika kucheza michezo mbalimbali.

Saturday, March 11, 2017

MSONGOZI APONGEZA UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI AKIDAI KUWA WANAWAKE WAMEANZA KUNUFAIKA

Jackline Msongozi akizungumza juzi siku ya sherehe za maadhimisho ya wanawake duniani mjini Songea.
Na Julius Konala,      
Songea.

MBUNGE wa Viti maalum Wanawake mkoani Ruvuma, Jackline Msongozi kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ameipongeza serikali ya awamu ya tano kupitia Wakala wake wa barabara Tanroads mkoani hapa, kwa kusimamia na kukamilisha ujenzi wa barabara kiwango cha lami inayounganisha upande wa Mangaka mkoani Mtwara hadi Namtumbo mkoani Ruvuma kwa madai kuwa baadhi ya wanawake wameanza kunufaika na mradi huo kiuchumi kutokana na kuuza bidhaa mbalimbali.

Msongozi alisema hayo juzi wakati alipokuwa akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya Wanawake duniani ambapo kiwilaya yalifanyika katika viwanja vya soko la Mjimwema lililopo mjini Songea.

Alisema kuwa kukamilika kwa mradi huo kumechochea kasi ya maendeleo kwa akina mama wajasiriamali kujiinua kiuchumi kutokana na kuanzisha biashara ndogo ndogo pembezoni mwa barabara hiyo pamoja na kusafirisha mazao yao kwa urahisi.

CWT YASAIDIA WATOTO WALEMAVU SONGEA

Na Julius Konala,        
Songea.

KATIKA kuadhimisha siku ya Wanawake duniani, Chama Cha Walimu (CWT) kitengo cha wanawake Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma kimetoa msaada wa vitu mbalimbali kwa watoto wenye ulemavu ambao wana matatizo ya kusikia (Viziwi) katika shule ya msingi maalum ya Mtakatifu Vincent Ruhuwiko iliyopo mjini hapa.

Msaada huo ulitolewa jana shuleni hapo na Mwenyekiti wa CWT kitengo cha wanawake Manispaa ya Songea, Zabiuna Nchimbi ambapo alidai kuwa wameamua kufanya hivyo baada ya kuguswa na tatizo hilo linalowakabili watoto hao wenye ulemavu wa kusikia.

Nchimbi alitaja msaada uliotolewa kwa ajili ya watoto hao kuwa ni viatu, nguo, mafuta ya kupaka, chumvi pamoja na sabuni za kufulia huku akidai kuwa kufanikiwa kwa zoezi hilo kumetokana na kuchangishana walimu wenyewe.

SERIKALI YATAKIWA KUENDELEA KUBORESHA MIUNDOMBINU RAFIKI KWA WATU WENYE ULEMAVU

Martin Mbawala, ambaye ni Mratibu wa mafunzo ya sheria ya watu wenye ulemavu wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma akiwasisitiza jambo washiriki wa mafunzo hayo katika kata ya Mpepai wilayani hapa.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

BAADHI ya Watu wenye ulemavu wanaoishi katika kata ya Mpepai Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali izingatie suala la uboreshaji wa miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu hasa kwenye majengo ya umma yanayoendelea kujengwa hapa nchini kwa ajili ya kutolea huduma mbalimbali.

Washiriki wa mafunzo.
Vilevile wamesisitiza jamii kuacha tabia ya kuwafungia ndani watoto wenye ulemavu na kwamba wametakiwa kujenga mazoea ya kuwafichua watu wenye tabia ya kuwaficha watoto hao, ili wahusika wanaofanya hivyo wachukuliwe hatua kali za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

Hayo yalisemwa juzi na Walemavu hao kwa nyakati tofauti wakati walipokuwa wakichangia hoja mbalimbali katika mafunzo ya siku mbili ya sheria ya watu wenye ulemavu, yaliyofanyika katika kata ya Mpepai halmashauri ya mji huo ambayo yalifadhiliwa na shirika lisilokuwa la kiserikali la Foundation for Civil Society.

Wednesday, March 8, 2017

SIKU YA WANAWAKE DUNIANI: ANAHITAJI MSAADA WAKO ILI AWEZE KUTEMBEA VIZURI


Beatrice Ndomba, akiwa bado hajapata tatizo la ulemavu wa miguu.
Na Albano Midelo,
Songea.

HUJAFA hujaumbika, Beatrice Ndomba (24) pichani, alizaliwa akiwa na miguu yake yote miwili hadi alipomaliza kidato cha nne na kuanza kusoma Stashahada ya uhasibu mwaka wa kwanza mkoani Mbeya 2014.

Aidha akiwa huko ndipo alipatwa na ulemavu wa viungo baada ya kukatwa miguu yake yote miwili.

Beatrice hivi sasa anaishi mtaa wa Ruhuwiko kanisani, katika Manispaa ya Songea mkoa wa Ruvuma na ndoto zake za kuwa Mhasibu zimefifia.

Mwaka jana alipata mafunzo ya ufundi kushona, kwa hiyo amejiajiri kama fundi cherehani na kwamba hivi sasa anahitaji msaada wa miguu bandia, ili aweze kutembea na kuendesha shughuli zake za kujitafutia ridhiki kama Watanzania wengine.

Beatrice ni mtoto yatima, anaishi na wadogo zake wawili, ukiguswa na tatizo hili unaombwa kumchangia kiasi chochote kile ili aweze kununua viungo bandia vyenye ubora kwa kuwa alivyonavyo sasa vinamuumiza miguu na hawezi kutembea vizuri.

CCM RUVUMA WAITAKA SERIKALI KUSIMAMIA KIKAMILIFU UJENZI WA DARAJA MTO RUHUHU

Na Kassian Nyandindi,    
Nyasa.

KAMATI ya siasa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Ruvuma, imeitaka serikali kupitia Wakala wake wa barabara (TANROADS) mkoani humo kusimamia kikamilifu ujenzi wa daraja la mto Ruhuhu, lililopo wilayani Nyasa mkoani hapa na kumuhimiza mkandarasi anayejenga daraja hilo akamilishe ujenzi wake kwa wakati na viwango vinavyokubalika.

Aidha kampuni ya ujenzi Lukolo Construction Limited ndiyo inayofanya kazi ya ujenzi wa daraja hilo, ambapo Wajumbe wa Kamati hiyo walitembelea juzi kuona maendeleo ya mradi huo, ambao upo katika kata ya Lituhi wilayani humo mpakani mwa mkoa wa Ruvuma na wilaya ya Ludewa mkoa wa Njombe.

Mjumbe mmoja ambaye ni Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Ruvuma, Oddo Mwisho alisema kuwa serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania imejipanga kikamilifu kwa kuhakikisha kwamba, inaondoa kero zilizopo kwa wananchi wake wanaoishi katika maeneo hayo ndio maana inajenga daraja hilo hivyo mkandarasi huyo anapaswa kufanya jitihada kuhakikisha ujenzi huo unakamilika ndani ya mkataba husika.

Napegwa Kiseko ambaye ni Mhandisi mshauri ujenzi wa daraja hilo aliiambia Kamati hiyo ya siasa ya Chama Cha Mapinduzi kwamba mradi huo ujenzi wake unafadhiliwa kwa asilimia mia moja na serikali ya Tanzania.

“Daraja hili linalojengwa hapa, lipo umbali wa kilometa 84 kutoka kijiji cha Kitai wilaya ya Mbinga ambako kuna barabara kuu ya kiwango cha lami, tutahakikisha tunasimamia na kushauri kwa umakini mkubwa ili liweze kukamilika kwa viwango vinavyokubalika na wananchi waweze kuanza kulitumia”, alisema Kiseko.

Sunday, March 5, 2017

MBUNGE ATAKA KUREJESHWA KICHWA CHA NDUNA SONGEA MBANO

Waziri wa maliasili na utalii Profesa, Jumanne Magembe akiangalia juzi picha mbalimbali za marehemu mzee Rashid Kawawa (Simba wa vita) mara baada ya kuzindua rasmi makumbusho ya Kawawa eneo la Bombambili kata ya Bombambili katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.
Na Waandishi wetu,  
Songea.

MBUNGE wa viti maalum wanawake kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Ruvuma, Jaqcline Msongozi ameiomba serikali kupitia Waziri wa maliasili na utalii Profesa Jumanne Maghembe kuhakikisha kwamba inafanya juhudi za kuiomba serikali ya nchi ya Ujerumani kurejesha kichwa cha Nduna Songea Mbano.

Nduna Songea Mbano alikuwa Chifu wa kabila la Wangoni mkoani hapa ambaye  alifariki katika vita vya Majimaji mwaka 1905  pamoja na  Mashujaa wengine 66 na kwamba lengo la kukiomba kichwa hicho, ili kiweze kuoneshwa kwenye maadhimisho ya kumbukumbu ya vita hivyo kila mwaka hatua ambayo itasaidia hata vizazi vya sasa na vijavyo kuwa na uelewa juu ya tukio hilo.

Msongozi alitoa ombi hilo hivi karibuni mbele ya Waziri huyo ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya kumbukizi ya miaka 110 ya Mashujaa wa vita hivyo yaliyofanyika katika eneo la Mahenge Manispaa ya Songea ambako wamezikwa Mashujaa hao.

Alisema kuwa wananchi na wazee wa mkoa wa Ruvuma, kwa muda mrefu wamekuwa wakiomba kurejeshwa kwa kichwa cha Nduna Songea Mbano ili kiweze kuoneshwa kwa vizazi vya sasa na vijavyo na kuwa kivutio halisi kwa Watalii kutoka maeneo mbalimbali, kwa madai kwamba hakuna sababu ya kichwa chake kuendelea kukaa Ujerumani wakati yeye ni Mtanzania.

WAFANYABIASHARA SONGEA WANYOSHEANA KIDOLE

Na Mwandishi wetu,        
Songea.

KWA nyakati tofauti Wakazi wa Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wamelaani kitendo cha baadhi ya Wafanyabiashara wa Soko kuu Songea kukosa uzalendo na kushindwa kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano, katika kufanikisha suala la ukusanyaji wa mapato yake.

Aidha walisema kuwa badala yake wafanyabiashara hao wamekuwa wakihusika moja kwa moja kushinikiza watu wengine kukataa ongezeko la kodi mpya ya vibanda katika Soko hilo, kwa ajili ya maslahi yao binafsi huku wapangaji wengine wakijinufaisha kutokana na pango wanalopokea jambo ambalo linaisababishia serikali hasara kubwa.

Walisema kuwa kitendo cha wapangaji hao kugomea ongezeko hilo jipya la pango katika vibanda  hivyo linaonesha ni jinsi gani baadhi ya watu wanavyotaka kujinufaisha kupitia migongo ya watu wengine, kwani haiwezekani  Manispaa ya Songea ikapata fedha kidogo  na watu walioingia mikataba kwa kuwatumia madalali wakiendelea kunufaika kuwapangisha watu wengine kwa fedha nyingi.

Hivi karibuni wafanyabiashara wa Soko kuu la Manispaa hiyo walijikuta katika mgogoro mkubwa na uongozi husika wa Manispaa baada ya kugomea bei mpya ya pango inayotakiwa kulipwa kwa Manispaa badala ya madalali ambao wamekuwa wakijinufaisha kupitia mgongo wa nyuma.

RC RUVUMA ATAKA MAPAMBANO DHIDI YA MADAWA YA KULEVYA YAIMARISHWE


Mkulima wa mahindi kijiji cha Liweta halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma Sam Sanga katikati akiwa na bangi mara baada ya kukamatwa nayo na kikosi maalum cha kupambana na madawa ya kulevya shambani mwake juzi wilayani humo.
Na Kassian Nyandindi,
Songea.
MKUU wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge amelitaka Jeshi la Polisi mkoani humo, kuhakikisha kwamba linasimama imara na kuongeza nguvu hasa katika maeneo ya mipakani ili kuweza kuwabaini na kuwachukulia hatua kali za kisheria watu wanaoingiza madawa ya kulevya kupitia mipaka ya mkoa huo.

Aidha Dkt. Mahenge ameviagiza vyombo vyote vya ulinzi na usalama mkoani hapa kuhakikisha vinashirikiana na Polisi kufanya msako mkali utakaoweza kufanikisha kuwakamata baadhi ya watu wanaotumia, kuuza na kusafirisha madawa hayo kutoka ndani na nje ya nchi.

Mkuu huyo wa mkoa wa Ruvuma, alitoa agizo hilo juzi wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake mjini Songea na kusisitiza kwamba vita dhidi ya madawa ya kulevya ni ya kufa na kupona hadi pale watu wote wanaojihusisha na biashara hiyo watakapoiacha.

NAMTUMBO WALIA NA TATIZO LA UPUNGUFU WA DAWA VITUO VYA KUTOLEA HUDUMA ZA AFYA

Na Yeremias Ngerangera,      
Namtumbo.

KUFUATIA kuwepo kwa tatizo kubwa la upungufu wa dawa katika vituo vya kutolea huduma ya afya wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, Mbunge wa Jimbo la Namtumbo mkoani humo, Injinia Edwin Ngonyani amesikitishwa na hali hiyo na kuwaahidi wananchi wake kwamba tatizo hilo litapatiwa ufumbuzi wa kudumu ili lisiendelee kuumiza wananchi.

Ngonyani ambaye pia ni Naibu  Waziri  wa  ujenzi, uchukuzi  na mawasiliano alipokea malalamiko hayo juzi kutoka kwa wananchi wake kwamba vituo vya afya vilivyopo katika Jimbo hilo imekuwa ni kero kubwa juu ya upatikanaji wa dawa pamoja na huduma zingine muhimu za matibabu.

“Hapa katika jimbo letu kero kubwa pia huduma za bima ya afya pia ni tatizo, maji pamoja na upungufu wa waganga katika vituo vya kutolea huduma ya afya tunaiomba serikali itatue tatizo hili”, walisema.

Friday, March 3, 2017

MUHONGO AKUTANA NA KAMPUNI ZA UTAFUTAJI NA UCHIMBAJI MAFUTA NA GESI ASILIA NCHINI

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (mbele katikati) akiongoza mkutano na wawakilishi wa Kampuni za utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia nchini mkoani Mtwara hivi karibuni.

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo upande wa kulia akizungumza wakati wa mkutano na Kampuni zinazojihusisha na utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia nchini uliofanyika Madimba, mkoani Mtwara hivi karibuni. Kushoto ni Kaimu Kamishna msaidizi wa nishati sehemu ya Petroli, Mwanamani Kidaya.

Mwakilishi kutoka Kampuni ya Ophir Energy, Halfan Halfan (katikati) akielezea maendeleo ya shughuli zinazofanywa na kampuni yake wakati wa mkutano wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) na Kampuni za utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia nchini.
Na Mwandishi wetu,
Mtwara.

WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesema kwamba mikutano ya kila baada ya miezi mitatu na kampuni zinazojihusisha na utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia hapa nchini, itakuwa ikifanyika maeneo mbalimbali nchini hususan kwenye rasilimali husika.

Waziri Muhongo aliyasema hayo hivi karibuni mkoani Mtwara wakati wa mkutano wake na wawakilishi wa kampuni hizo, uliofanyika kwenye Kituo cha kuchakata gesi asilia cha Madimba mkoani humo.

Alisema kuwa mikutano hiyo mara zote ilikuwa ikifanyika Jijini Dar es Salaam hivyo ili kuweza kuleta tija zaidi ni vyema ikafanyikia kwenye maeneo yenye gesi asilia na baadaye siku za usoni itafanyika kwenye maeneo yatakayogundulika kuwa na mafuta.

TUKIO KATIKA PICHA: MBUNGE WA TUNDURU KUSINI AWATAKA WANANCHI WAKE KUZINGATIA MAAGIZO YA SERIKALI

Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kusini wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, Daimu Mpakate (katikati) akizungumza wakati wa ziara ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) ya kutembelea mto Muhuwesi uliopo wilayani humo ambapo aliwataka wananchi wa jimbo hilo kuzingatia maagizo yaliyotolewa na serikali juu ya zuio la kuacha shughuli za uchimbaji wa madini, katika mto huo hadi hapo maelekezo mengine yatakapotolewa na serikali.

SERIKALI YAZUIA UCHIMBAJI MADINI KWENYE MTO MUHUWESI TUNDURU

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akimsikiliza Ofisa Madini Mkazi wilaya ya Tunduru mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Fredrick Mwanjisi akielezea kuhusiana na shughuli za uchimbaji wa madini ya vito zilizokuwa zikifanyika kwenye mto Muhuwesi wilayani humo.

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akizungumza na baadhi ya wachimbaji wadogo wa madini ya vito wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma wakati alipotembelea eneo la mto Muhuwesi wilayani humo.
Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

SERIKALI hapa nchini imezuia shughuli za uchimbaji wa madini ya vito katika mto Muhuwesi wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, hadi hapo taarifa za kitaalamu zitakapotolewa mara baada ya kukamilika kwa zoezi la tathimini na ukaguzi husika.

Agizo hilo la kuzuia kazi hiyo kufanyika katika mto huo limetolewa hivi karibuni wilayani humo na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alipofanya ziara yake kwenye mto huo ili kujionea hali ya eneo hilo kufuatia ajali iliyosababisha kifo cha mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Kanje Ally na majeruhi mmoja ambao waliingia na kuanza kuchimba ndani ya mto huo.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ofisa madini mkazi wa wilaya ya Tunduru, Mhandisi Fredrick Mwanjisi alisema kuwa zaidi ya watu sita walivamia eneo hilo la mto kufanya shughuli za uchimbaji wa madini kinyume cha taratibu, kutokana na kutokuwa na vibali vilivyowaruhusu kufanya shughuli hiyo ya uchimbaji katika eneo hilo.