Tuesday, March 14, 2017

RC RUVUMA AWATAKA VIONGOZI KUDHIBITI MATUMIZI YA POMBE AINA YA KIROBA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge.
Na Muhidin Amri,  
Songea.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge amewataka viongozi kuanzia ngazi ya vitongoji hadi wilaya, wahakikishe kwamba wanadhibiti kikamilifu matumizi ya pombe zilizofungashwa kwenye mifuko maarufu kama Kiroba ili zisiweze kuonekana mitaani zikiendelea kutumika, ikiwa ni lengo la kuokoa maisha ya Watanzania wengi hasa vijana walioathirika na matumizi ya pombe hizo.

Aidha amewataka viongozi hao pia wahakikishe kwamba kila wanapopata fursa ya kukutana na wananchi, watoe elimu kuhusiana na madhara yatokanayo na kiroba ambapo kwa kiwango kikubwa pombe hiyo imekuwa ikisababisha madhara makubwa katika jamii.

Dkt. Mahenge alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, ambapo alieleza kuwa matumzi ya viroba yamekuwa yakichochea pia ongezeko la matukio ya uhalifu na ajali barabarani, hasa kwa zile zinazotokana na waendesha pikipiki maarufu kwa jina la bodaboda na kusababisha watu wengi kuumia, kupoteza viungo vyao vya mwili kuwa walemavu huku wengine wakipoteza maisha yao.


Alisema kuwa hata baadhi ya maeneo wanafunzi wa shule za msingi na sekondari wamekuwa wakiacha kuzingatia masomo yao darasani badala yake wamekuwa vinara wakubwa wa kunywa pombe hizo, jambo ambalo linahatarisha hapo baadaye kuwa na taifa la watu goigoi ambao watashindwa kumudu kufanya kazi za kujiletea maendeleo.


Mkuu huyo wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Mahenge alifafanua kuwa matumzi ya kiroba yamekuwa yakisababisha athari mbalimbali hasa kwa vijana ambao hununua pombe hiyo kutokana na urahisi wa bei yake, hivyo ameliagiza Jeshi la Polisi na vyombo vyote vya ulinzi na usalama mkoani humo kufanya doria mara kwa mara hasa maeneo ya mipakani na sehemu za starehe ili kuweza kudhibiti kabisa matumzi ya pombe hiyo na kwa yule atakayekamatwa akiuza achukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

No comments: