Sunday, March 26, 2017

SAMANDITO: UPIMAJI ARDHI MBINGA UTALETA MANUFAA MAKUBWA KWA WANANCHI

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Gombo Samandito alipokuwa akizungumza hivi karibuni na wakazi wa tarafa ya Mbuji wilayani humo kuhusiana na mpango wa halmashauri hiyo, kuanza mchakato wa upimaji ardhi na kuanzishwa kwa miji midogo sambamba na uendelezaji wa miji hiyo ambapo baadhi ya maeneo yatachukuliwa na serikali kwa ajili ya kupisha huduma mbalimbali za kijamii kama vile ujenzi wa shule, zahanati, miundo mbinu ya maji na barabara.
Wataalamu wa masuala ya ardhi katika halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wakiendelea na zoezi la utengenezaji wa Hati za hakimiliki za kimila kwa ajili ya kuwakabidhi wananchi ambao wamepimiwa mashamba yao wilayani humo. 
Na Kassian Nyandindi,   

SIKU zote jamii imekuwa ikitambua kwamba ardhi ni rasilimali muhimu katika kujiletea maendeleo kwa kuitumia kuendeshea shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo, ujenzi wa makazi, ufugaji na shughuli nyingine ambapo kutokana na umuhimu wake baadhi ya viongozi kwenye vitongoji na vijiji wamekuwa wakitumia umuhimu wa mahitaji ya ardhi kujinufaisha kwa kuigawa bila kuzingatia sheria, sera na kanuni zilizopo za ugawaji ardhi.

Kutokana na uwepo wa hali hiyo, sasa imekuwa ikisababisha hata kuibuka kwa migogoro ya ardhi katika baadhi ya maeneo hapa nchini na haya yote yanasababishwa na viongozi hao kutaka kuingia madarakani kwa kujinufaisha matumbo yao.

Miaka ya 1990 serikali ya Tanzania ilijihusisha katika mchakato wa kutengeneza sera na mfumo wa sheria ambayo ilipelekea uundaji wa sera ya Taifa ya ardhi ya mwaka 1995 na kutungwa kwa sheria ya ardhi ya mwaka 1999 ambazo ni sheria ya ardhi ya vijiji namba tano ya mwaka 1999 na sheria ya ardhi namba nne ya mwaka 1999 ambapo hizo zote, zimekuwa zikieleza mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji lakini licha ya kuwepo kwa sheria hizo bado changamoto ya migogoro ya ardhi imekuwa ikiendelea kujitokeza katika baadhi ya maeneo.

Aidha juhudi hizo  bado zinahitajika katika kukuza uelewa wa wanakijiji juu ya mifumo ya kisheria katika masuala ya haki za ardhi, uwezo wa uwekezaji mkubwa wa kilimo na uhusiano na ustawi wa wakulima wadogo, kilimo endelevu na maendeleo endelevu ya nchi kwa ujumla.

Hivyo katika kuliona hilo kuwa na umuhimu huo wa kipekee, Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma imeweza kuwaelimisha wananchi wake wilayani humo juu ya masuala ya upimaji wa ardhi yao ikiwemo viwanja, mashamba na miji midogo ili kuweza kuondoa migogoro isiyokuwa ya lazima. 
Gombo Samandito akiwa ameshika moja kati ya Hati ya hakimiliki ya kimila.

Migogoro hiyo ya ardhi mingi imekuwa ikijitokeza baina ya wakulima na wafugaji, wakulima na wawekezaji, mtu kwa mtu na kijiji kwa kijiji ambayo wakati mwingine imekuwa ikisababisha watu kupoteza maisha, kupata ulemavu na upotevu wa hata mali zao.

Wengi tumekuwa tukishuhudia kwamba kushamiri kwa migogoro hiyo imekuwa pia ikisababisha kudumaa kwa uchumi wa wananchi kwani wakati mwingine wakulima wamekuwa wakishindwa kuzalisha mazao, wafugaji mifugo yao kujeruhiwa, wawekezaji nao mali zao kuharibiwa na wananchi kutokana na kugombea ardhi kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo kilimo, makazi na ufugaji.

Mwandishi wa Makala haya amefanya mahojiano na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Gombo Samandito ambaye ameeleza kwamba hadi kufikia sasa mashamba yenye zaidi ya ukubwa wa ekari 78,149.065 sawa na hekta 31,259.626 yameingizwa na kupimwa katika mpango wa upimaji ardhi wa wilaya hiyo.


Samandito anasema kuwa halmashauri hiyo inaendelea kutekeleza sheria za ardhi pamoja na kutimiza agizo la serikali la kupima kila kipande cha ardhi na kukimilikisha kwa walengwa husika, huku ikiendelea kuhamasisha wamiliki wa viwanja na mashamba kulipia kodi za ardhi pamoja na kuviendeleza viwanja vyao kwa mujibu wa sheria, ikiwa pamoja na kusambaza hati za madai ya kodi kwa wadaiwa sugu na wale wanaoshindwa kulipa hufikishwa Mahakamani.

Anabainisha kuwa jumla ya hati ya hakimiliki za kimila 20,000 zinatarajiwa kutolewa kwa wananchi wa vijiji 121 vilivyopo katika kata 29 za halmashauri hiyo na kwamba mpaka sasa zaidi ya hati ya hakimiliki za kimila 3,000 zipo tayari na wananchi wanatakiwa kukabidhiwa kwa utaratibu husika ulioandaliwa.

“Lengo kubwa hapa la kufanya hivi ni kuepuka migogoro ya ardhi katika upangaji, upimaji na ugawaji wa viwanja baina ya wamiliki wa ardhi na serikali yetu hivyo mpaka sasa tumeweza kupima ekari 70,000 hapa wilayani kwa kutumia utaratibu wa upimaji shirikishi, bila kulipa fidia ambapo mmiliki wa ardhi huchangia gharama ya upimaji kwa kutoa asilimia 40 ya viwanja vitakavyopatikana katika ardhi yake,

“Utoaji wa asilimia hii ya viwanja huenda kwa halmashauri kwa lengo la kufidia maeneo yote yatakayoangukia kwenye maeneo ya huduma za kijamii kama vile barabara, maeneo ya wazi, ujenzi wa zahanati, masoko na shule huku asilimia 60 ya viwanja itakayopatikana katika ardhi husika hubaki kwa mmiliki wa ardhi na zoezi hili litaendelea kuwa endelevu kwa manufaa ya wananchi wetu”, anasema Samandito.

Pamoja na mambo mengine kwa upande wa utatuzi wa migogoro mbalimbali ya ardhi wilaya ya Mbinga, imekuwa ikiendelea kupambana na utatuzi wa migogoro hiyo kwa kutenga siku moja ya Ijumaa ya kila mwisho wa mwezi na kuanzisha dawati la kupokea kero za wananchi zinazohusiana na masuala ya ardhi ili yaweze kutatuliwa.

Awali Samandito akizungumzia kabla ya zoezi hilo la upimaji kuanza wilayani hapa, anafafanua kuwa miongoni mwa watu waliopatiwa mafunzo juu ya manufaa ya zoezi hilo wakiwemo watumishi wa serikali watendaji kata na vijiji, maafisa ugani, fundi sanifu ramani ambao baadaye walipita vijijini kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wake wa kutekeleza zoezi hilo kabla upimaji huo haujaanza.

Mafunzo hayo yalihusisha haki za ardhi kwa makundi mbalimbali, sera na sheria zinazosimamia ardhi, mpango wa matumizi ya ardhi vijijini, utatuzi wa migogoro ya ardhi ambayo yalilenga hasa kuwajengea uelewa wananchi katika masuala ya haki za ardhi na kuwajengea uwezo zaidi katika kuisimamia serikali katika usimamizi wa ardhi na rasilimali za nchi.

Mkurugenzi huyo wa halmashauri ya wilaya hiyo anaongeza kuwa wananchi wengi ni wakulima na wafugaji na kwamba shughuli zao kubwa zinahitaji ardhi kwa ajili ya kuendesha shughuli hizo hivyo mara nyingi wamekuwa wakiingia kwenye migogoro kutokana na uwepo wa mwingiliano usiokuwa na tija kwao baina ya pande hizo mbili.

Anasisitiza kuwa umefika wakati sasa viongozi wa vijiji waliopata elimu hiyo watumie nafasi yao katika kutatua changamoto ya migogoro ya ardhi kwenye maeneo yao kwa kuwasisitiza wananchi wapime ardhi zao ili baadaye waweze kuzimiliki kisheria na kuwa na hati ya hakimiliki ya kimila ambazo zitaweza kuzuia na kuondoa chanzo cha kushamiri kwa migogoro ya ardhi isiyokuwa ya lazima kwenye maeneo yao.

Anasema pia tatizo la wanaume kuwadharau wanawake kumiliki ardhi kwenye ardhi za ukoo kwa kuwaona kuwa wanawake hawana haki ya kumiliki ardhi kisheria licha ya sheria kueleza wazi kuwa mwanamke naye ana haki ya kumiliki ardhi sawa na mwanaume, hivyo anaomba jamii iondokane na dhana hii potofu na mtizamo huu hafifu uliopo katika jamii kulingana na mila na desturi kwa kuona kwamba mwanamke hana haki ya kumiliki mali hususani kwenye ardhi sawa kama ilivyo kwa wanaume.

Kadhalika Mratibu wa zoezi la upimaji ardhi wilayani humo, Faraja Kaluwa anaeleza kwamba baadhi ya viongozi kutojua majukumu yao kama viongozi katika kuongoza wananchi huko vijijini, hali hiyo nayo huchangia viongozi hao kutotambua wajibu wao na mipaka yao ya kiutendaji ambapo kufanya hivyo wamekuwa wakisababisha hata baadhi yao kugawa ardhi bila kuzingatia sheria.

Pamoja na mambo mengine Kaluwa anabainisha kuwa ardhi inayotolewa na kijiji haizidi ekari 50 na kwamba zaidi ya kiwango hicho muombaji anapaswa kwenda ngazi ya halmashauri lakini baadhi ya viongozi kwenye vitongoji au vijiji, kutokana na baadhi yao kuwa na uelewa mdogo hufanya hivyo kwa tamaa na kutoa ardhi zaidi ya ekari 50 kwa muombaji jambo ambalo ni kosa kwa mujibu wa sheria za nchi.

“Pia kuna tatizo wananchi kutokuwa na elimu katika suala zima la matumizi bora ya ardhi hivyo jitihada zaidi zinahitajika katika kutoa elimu kwa viongozi kwenye vijiji, vitongoji na jamii kwa ujumla na uwepo wa mawasiliano katika sekta za serikali katika kupanga mipango ya matumizi bora ya ardhi ili kuweza kushirikiana katika utekelezaji wa shughuli za kupanga mipango hiyo”, anasisitiza Kaluwa.


Hata hivyo kwa ujumla zoezi la upimaji ardhi kwa halmashauri ya wilaya Mbinga mkoani Ruvuma, wananchi wengi wamelipokea kwa mikono miwili baada ya kubaini kwamba litawaletea manufaa makubwa ya kukuza uchumi wao mara baada ya kuanza kupata hati za hakimiliki ya kimila ambazo huwawezesha sasa hata kwenda benki kukopa fedha za kufanyia shughuli zao za kimaendeleo, ikiwemo kuboresha mashamba yao ya kahawa na mazao mengine mbalimbali ili waweze kuzalisha kwa wingi na hatimaye kuondokana na umaskini.

No comments: