Friday, March 24, 2017

WASHIRIKI WA MAFUNZO JUU YA MATUMIZI BORA YA ARDHI SONGEA WALALAMIKIA KUKOSA USHIRIKIANO TOKA OFISI ZA VIJIJI

Na Julius Konala,   
Songea.

MTANDAO wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) mkoani Ruvuma, kupitia ufadhili wa shirika la Tanzania Foundation for Civil Society (FCS) umeendesha mafunzo juu ya matumizi bora ya ardhi kwa wakulima wadogo wadogo wanaotoka katika kata nne wilayani Songea mkoani humo.

Mafunzo hayo yalifanyika jana kwenye ukumbi wa mikutano wa chuo cha ushirika kilichopo katika Manispaa ya Songea ambayo yalifunguliwa na Mwenyekiti wake Asumpta Ndauka, ambapo washiriki hao wametakiwa kuzingatia sheria na taratibu husika za mafunzo hayo waliyopata kwani wao ndio waathirika wakubwa wa migogoro ya ardhi vijijini.

Aidha mafunzo hayo yalishirikisha washiriki 200 wa kutoka katika kata ya Magagura, Mpitimbi, Mpandangindo na Mbingamhalule wilayani humo na kwamba Mwenyekiti huyo amewataka pia wanawake kuwa mstari wa mbele katika kupigania haki zao juu ya umilikishwaji wa ardhi na kupata hati miliki kwa madai kuwa wao wamekuwa wakikosa fursa hiyo kutokana na uwepo wa tatizo la mfumo dume.


“Hivi sisi wanawake kwetu ni wapi, maana kwa upande wa wazazi wetu tunakosa fursa ya kumiliki ardhi na kwa waume zetu hatuna nafasi ya kumiliki ardhi jambo hili linatufanya tushindwe kuelewa nafasi yetu katika suala la umiliki wa ardhi lipo wapi”, alihoji Ndauka.

Naye Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Leonce Mutalemwa aliwataka washiriki hao wa vikundi vya wakulima kutambua kuwa suala la umiliki wa ardhi ni haki ya kila  mmoja iwe mwanaume au mwanamke, huku akiwaasa washiriki hao kuwa na hati ya pamoja kwa mali isiyogawanyika kwa madai kwamba kufanya hivyo kutasaidia kuondoa migogoro katika familia na kumlinda mjane au mgane.

Wanufaika hao wa vikundi vya wakulima kutoka katika kata hizo wameweza kujifunza mada mbalimbali ikiwemo kujua sheria za ardhi Tanzania na kutambua thamani ya ardhi.

Kwa upande wao baadhi ya washiriki hao, Pascal Kilawi kutoka kata ya Mpitimbi, Prisca Mhagama kutoka kata ya Magagura na Dionis Geo walipokuwa wakihojiwa na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti walisema kuwa mafunzo hayo yameweza kuwajengea uwezo wa ufahamu juu ya masuala ya ardhi, ambapo miongoni mwao wameanza kupata mwanga katika kupata haki zao na kwamba wanakumbana na changamoto ya kupata ushirikiano mdogo toka ofisi za vijiji na wananchi wengi kushindwa kumudu gharama za upimaji na upatikanaji wa hati miliki.

No comments: