Saturday, March 11, 2017

MSONGOZI APONGEZA UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI AKIDAI KUWA WANAWAKE WAMEANZA KUNUFAIKA

Jackline Msongozi akizungumza juzi siku ya sherehe za maadhimisho ya wanawake duniani mjini Songea.
Na Julius Konala,      
Songea.

MBUNGE wa Viti maalum Wanawake mkoani Ruvuma, Jackline Msongozi kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ameipongeza serikali ya awamu ya tano kupitia Wakala wake wa barabara Tanroads mkoani hapa, kwa kusimamia na kukamilisha ujenzi wa barabara kiwango cha lami inayounganisha upande wa Mangaka mkoani Mtwara hadi Namtumbo mkoani Ruvuma kwa madai kuwa baadhi ya wanawake wameanza kunufaika na mradi huo kiuchumi kutokana na kuuza bidhaa mbalimbali.

Msongozi alisema hayo juzi wakati alipokuwa akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya Wanawake duniani ambapo kiwilaya yalifanyika katika viwanja vya soko la Mjimwema lililopo mjini Songea.

Alisema kuwa kukamilika kwa mradi huo kumechochea kasi ya maendeleo kwa akina mama wajasiriamali kujiinua kiuchumi kutokana na kuanzisha biashara ndogo ndogo pembezoni mwa barabara hiyo pamoja na kusafirisha mazao yao kwa urahisi.


Aidha amewataka wanawake hao kutumia fursa ya kukamilika kwa miradi ya ujenzi wa barabara, kujikita kwenye shughuli za uzalishaji mali ikwemo katika nyanja ya kilimo na ufugaji kwa lengo la kujipatia kipato badala ya kuwa tegemezi.

Mbali na mambo mengine Mbunge huyo ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo, amewapongeza pia wanawake hao kwa kuonesha moyo wa ujasiri katika kugombea nafasi mbalimbali za uongozi za kisiasa mkoani humo.

Awali akisoma risala  kwa niaba ya wanawake wenzake mbele ya mgeni rasmi, Joyce Mwanja alisema kuwa kutokana na uhamasishaji wa wanawake wengi kujiunga katika vikundi vya uzalishaji mali kumesaidia kuongeza uelewa  na ari ya utendaji kazi kiuchumi ambapo jumla ya vikundi 300 vya wanawake wazalishaji mali vimeundwa mjini hapa.


Mwanja alisema kuwa katika kipindi hicho chote shughuli mbalimbali za uzalishaji mali zimefanyika ikiwemo usindikaji, kilimo, uanzishwaji wa magenge ya kuuzia biashara, ufugaji, kilimo, ufumaji na uhifadhi wa mazingira ambapo katika kipindi cha mwaka 2014/2015 hadi mwaka 2016/2017 jumla ya vikundi 172 vya wanawake wajasiriamali vimepatiwa mikopo midogomidogo yenye masharti nafuu yenye thamani ya shilingi milioni 87.1.

No comments: