Sunday, March 5, 2017

RC RUVUMA ATAKA MAPAMBANO DHIDI YA MADAWA YA KULEVYA YAIMARISHWE


Mkulima wa mahindi kijiji cha Liweta halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma Sam Sanga katikati akiwa na bangi mara baada ya kukamatwa nayo na kikosi maalum cha kupambana na madawa ya kulevya shambani mwake juzi wilayani humo.
Na Kassian Nyandindi,
Songea.
MKUU wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge amelitaka Jeshi la Polisi mkoani humo, kuhakikisha kwamba linasimama imara na kuongeza nguvu hasa katika maeneo ya mipakani ili kuweza kuwabaini na kuwachukulia hatua kali za kisheria watu wanaoingiza madawa ya kulevya kupitia mipaka ya mkoa huo.

Aidha Dkt. Mahenge ameviagiza vyombo vyote vya ulinzi na usalama mkoani hapa kuhakikisha vinashirikiana na Polisi kufanya msako mkali utakaoweza kufanikisha kuwakamata baadhi ya watu wanaotumia, kuuza na kusafirisha madawa hayo kutoka ndani na nje ya nchi.

Mkuu huyo wa mkoa wa Ruvuma, alitoa agizo hilo juzi wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake mjini Songea na kusisitiza kwamba vita dhidi ya madawa ya kulevya ni ya kufa na kupona hadi pale watu wote wanaojihusisha na biashara hiyo watakapoiacha.


Dkt. Mahenge alisema kuwa mapambano dhidi ya madawa ya kulevya ni magumu, hivyo kila mwananchi lazima ashiriki kikamilifu bila kujali wahusika wa biashara hiyo ni watu wa aina gani, cheo au mchango wao katika jamii inayotuzunguka.

Alisema kuwa madhara ya madawa ya kulevya katika jamii yetu ni makubwa mno ambapo baadhi ya familia zimepoteza vijana wao ambao ni nguvu kazi na sio kwa familia hizo tu, bali hata kwa taifa letu jambo ambalo limechangia kuendelea kuwa maskini.

Pia aliwataka wananchi wa mkoa wa Ruvuma, wakiwemo waandishi wa habari kutoa taarifa sahihi zitakazofanikisha kukamatwa kwa watu hao huku akiongeza kuwa, madawa hayo ni janga kubwa katika nchi yetu na kwamba viongozi waliopo katika ngazi ya vijiji, kata na wilaya nao wametakiwa kushiriki kikamilifu katika kupambana na vita hiyo ambayo imeanzishwa na serikali hii ya awamu ya tano.

Dkt. Mahenge amewaagiza wafanyakazi wa uwanja wa ndege wa Songea, ofisi za uhamiaji na bandari ya Mbamba bay wilayani Nyasa mkoani humo, kuongeza juhudi na umakini mkubwa wa kufanya upelelezi na upekuzi wa watu wanaoingia na  kutoka katika maeneo hayo.

Hata hivyo amewataka vijana hususan waendesha Pikipiki maarufu kwa jina la bodaboda kuwa makini pale wanapowabeba watu au mizigo ambayo hawaitambui, kwani baadhi ya wahalifu hupenda kutumia usafiri wa aina hiyo ili kufanikisha malengo yao.

No comments: