Monday, April 29, 2013

BREAKING NEWS: MWANAFUNZI AKATWA MKONO, AUGUZA JERAHA HOSPITALINI


Na Steven Augustino,
Tunduru.

MWANAFUNZI anayesoma darasa la pili katika shule ya msingi Mwongozo kata ya Ligoma tarafa ya Namasakata wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma,  ameumizwa vibaya katika mkono wake wa kulia baada ya kukatwa na upanga na mwanafunzi mwenzake.
Ikra Said mwenye umri wa miaka saba ndiye aliyekatwa mkono wake, na amelazwa katika hospitali ya wilaya ya Tunduru akiendelea na matibabu.

Mwandishi wa habari hizi amezungumza na majeruhi huyo ambapo alisema  kuwa mkasa huo ulimpata wakati akiwa na wanafunzi wenzake ambao walikuwa wametumwa na mwalimu waliye mtaja kwa jina moja la Komba ili wakamtafutie kuni msitu uliojirani na shule hiyo.

Akifafanua taarifa hiyo mwanafunzi huyo alisema kuwa wakati wakiwa katika harakati hizo za kutafuta kuni, ghafla alijikuta akishambuliwa kwa kukatwa na panga katika mkono wake wa kulia, na mwanafunzi mwenzake Ashraki Said anayesoma darasa la tatu shuleni hapo.   

Katika taarifa hiyo mwanafunzi huyo baada ya kufanya tukio hilo, alikimbia na kumtelekeza katika eneo la tukio kabla ya kuokolewa na wanafunzi wengine ambao walimpeleka nyumbani kwao, na kuwaeleza wazazi wake juu ya mkasa huo.

Baba mzazi wa majeruhi huyo Said Izulu alisema kuwa baada ya kumpokea mwanaye aliyeumizwa alienda shuleni kwa ajili ya kutaka maelezo juu ya kilichotokea, lakini hakupewa ushirikiano na walimu hali ambayo ilimfanya achukue jukumu la kumkimbiza hospitali kwa ajili ya matibabu.

Alisema kilicho msikitisha zaidi ni kitendo cha walimu hao akiwemo mwalimu ambaye alitajwa kuwatuma watoto hao, ili wakamtafutie kuni kutoonesha ushirikiano baada ya tukio hilo baya kujitokeza.

Alipotafutwa kaimu afisa elimu shule za msingi wilayani Tunduru, Flavian Nchimbi ili kuzungumzia tukio hilo hakupatikana ofisini kwake wala katika simu yake yenye namba 0755646719 haikuweza kupatikana.

Wakizungumza kwa masharti ya kutotajwa majina yao baadhi ya maofisa wa idara ya elimu wilayani humo, kwa madai kuwa wao siyo wasemaji walisema kuwa endapo mwalimu Komba alichukua maamuzi ya kuwatumikisha  watoto  kwa manufaa yake alifanya kosa.

Walisema taratibu za kuwatuma wanafunzi kwenda kufanya kazi yoyote yenye manufaa ya shule, hutakiwa kufanya kazi hizo mbele ya usimamizi wa mwalimu na kwamba hata kama kuni hizo walizokuwa wametumwa ni kwa ajili ya kupikia chakula cha wanafunzi, ilitakiwa awepo mwalimu ili kuepusha matatizo yanayoweza kutokea baadaye.


No comments: