Monday, April 1, 2013

UZINDUZI WA ALBAMU YA INJILI WAFANA, MKUU WA WILAYA YA MBINGA AWATAKA WANANCHI KUJENGA USHIRIKIANO

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga (Aliyeinama katikati) akiingiza DVD yenye nyimbo za Injili zilizotungwa na Rose Mahenge kwenye radio, ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa albamu ya Waweza zeeka mapema, uliofanyika kwenye ukumbi wa Uvikambi mjini Mbinga. (Picha na Kassian Nyandindi)





Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

WANANCHI wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kujenga ushirikiano na sio kujengeana ubaguzi, ikiwa ni lengo la kuwafanya waweze kusukuma mbele gurudumu la kimaendeleo kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.

Sambamba na hilo wametakiwa kushiriki kikamilifu katika suala zima la ulinzi na usalama, ili wilaya hiyo iweze kuwa na amani na utulivu na hatimaye wananchi wilayani humo, waweze kuishi kwa raha mustarehe bila kuwepo vikwazo vya hapa na pale.

Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga aliyasema hayo jana wakati wa uzinduzi wa albamu ya nyimbo za injili, ‘Waweza zeeka mapema’ iliyotungwa na mwimbaji maarufu wa nyimbo za injili wilayani humo Rose Mahenge, uzinduzi ambao ulifanyika kwenye ukumbi wa Uvikambi uliopo Mbinga mjini.


Senyi Ngaga alikuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa albamu hiyo ambayo imesheheni nyimbo hizo, zenye kufunza wanadamu waishi kwa upendo na amani, sio kupenda mambo ambayo hayampendezi mwenyezi Mungu.

Kadhalika uzinduzi huo ulishirikisha wasanii maarufu nchini, Senga na Pembe wa kutoka Jijini Dar es salaam, ambao nao walikuwa wakitumbuiza na kutoa burudani za aina mbalimbali.

Albamu hiyo imebeba nyimbo lukuki za kumsifu  Mungu ambazo ni  Waweza zeeka mapema, Mbinguni tutaimba, Maajabu ya wanadamu, Leleno tuhine, Nasubiri zamu yangu, Mungu nikupe nini, Uumbaji wa Mungu, Makabila yote, Rimix(Mbinguni tutaimba) na Mwanaume ni Yesu.

Hiki ni kibao cha pili kutolewa na msanii huyo maarufu wa nyimbo za injili hapa wilayani Mbinga, ambapo awali aliweza kutoa kibao kingine ambacho kilitamba kwa jina la ‘Mbinguni ndiko nyumbani kwetu’.

Kwa mujibu wa maelezo ya msanii huyo alimweleza mwandishi wa habari hizi kuwa, nyimbo hizo zimebeba maudhui yanayolenga na kumtaka binadamu kumcha Mungu na kuacha starehe na anasa mbalimbali ambazo zimekuwa zikisababisha ongezeko la dhambi duniani.

Awali Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, aliwasisitiza wakazi wa wilaya hiyo kuzingatia suala la elimu, ikiwemo kwanza kupeleka watoto wao shule, ndipo mambo mengine ya kimaendeleo yafuate na kuacha tabia ya kuendekeza kuchangia kwenye harusi au sherehe za aina mbalimbali.

No comments: