Friday, April 12, 2013

MATUMIZI SAHIHI YA MBOLEA ZA ASILI YATABORESHA ZAO LA KAHAWA


Upande wa kushoto mtaalamu wa mimea na udongo Kaminyoge Mhamerd wa kampuni ya Sustainable Harvest, ya kutoka wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro, akiwa katika eneo la shamba darasa la kilimo cha kahawa, kikundi cha Unango kata ya Ngima wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, akiwaelimisha wakulima wa zao hilo kuzingatia kanuni za kilimo bora.(Picha na Kassian Nyandindi)



Na Kassian Nyandindi,



KAHAWA ni moja kati ya bidhaa muhimu na maarufu inayopendwa duniani, vilevile ni chanzo cha mapato kwa nchi zinazozalisha zao hilo.
     
Uzalishaji wa zao hili si kazi rahisi bali ni kazi ngumu inayohitaji ujuzi wa hali ya juu, na kwamba  ili kuwawezesha wakulima kuzalisha zao hilo kwa viwango vyenye ubora, mara zote sekta husika zimekuwa zikiwaelimisha wakulima hao mara kwa mara namna ya uzalishaji huo.

Tanzania ni moja kati ya nchi inayozalisha kahawa, huku jitihada mbalimbali zimekuwa zikifanywa ili kuboresha uzalishaji wake kwa ushirikiano, kati ya serikali na taasisi binafsi.


     
Katika kuhamasisha wakulima kujiunga katika vikundi au ushirika ni njia moja wapo ambayo imekuwa ikisisitizwa, ikiwemo uzalishaji wa mazao mbalimbali kwa pamoja ili kuongeza ufanisi, na muungano huo inakuwa rahisi kwa wataalamu wa kilimo kuwatembelea  na kuwapa utaalamu kuliko kumpitia mkulima mmoja mmoja.

Majira limezungumza na mtaalamu wa mimea na udongo Kaminyoge Mhamerd wa kampuni ya Sustainable Harvest, ya kutoka wilaya ya Moshi mkoani kilimanjaro, ambayo hujishughulisha na uboreshaji wa zao hilo ambapo anasema, ili uzalishaji wa kahawa bora uweze kufikiwa wakulima  wa zao hilo  hawana budi kuzingatia kanuni za kilimo bora.

Kaminyoge anasema kuwa ni pamoja na kuzingatia matumizi sahihi ya mbolea za asili katika uzalishaji wa zao hilo, vimekuwa vikisaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha na kuongeza uzalishaji, hivyo wakulima wametakiwa kujenga mazoea ya kutumia mbolea hizo mashambani mwao.

Anasisitiza kwamba, pia inashauriwa kutumia dawa za asili ambazo humfanya mkulima, kuvuna kahawa yenye kiwango cha juu na yenye ubora unaokubalika katika soko la dunia.


Mtaalamu huyo wa mimea na udongo anafafanua kuwa kwa kuzingatia hilo, wamekuwa wakitoa elimu kwa wakulima wa kahawa wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, juu ya utengenezaji wa mbolea hizo za asili.

Anasema mwitikio umekuwa mkubwa kutoka kwa wakulima wilayani humo, huku akieleza kuwa mbolea hiyo ina sifa ya kuwa na uwiano sahihi wa virutubisho vinavyotakiwa katika mmea wa kahawa.

Kadhalika elimu juu ya kudhibiti ubora wa kahawa ikiwa shambani na kwenye mitambo ya kukobolea zao hilo, imekuwa ikitolewa kwa wakulima hao.

Pia anasema wamekuwa wakitoa utaalamu wa jinsi ya kudhibiti magonjwa na wadudu wanaoshambulia mmea wa kahawa ukiwa shambani, kwa kutumia viuatilifu asilia ambavyo havina madhara kwa mkulima mwenyewe na mazingira.


Kaminyoge anatolea mfano kwamba dawa moja wapo ya asili ambayo hutumika kuulia wadudu wanaoshambulia zao hilo kama vile vidung'ata na vidugamba, ni mkojo wa ng'ombe ambao huchanganywa na jivu na kuvundikwa ndani ya siku 14 na baada ya hapo ndio hutumika kupuliza kwa siku saba, katika mashamba ya kahawa kwa ajili ya kuangamiza wadudu hao.


"Tangu tumeanza kuelimisha wakulima wa Mbinga, kumekuwa na mabadiliko kwa sababu wakulima wengi wamekuwa na uelewa wa kutosha juu ya matumizi sahihi ya njia za asili za kutunza zao la kahawa", anasema.


Pamoja na mambo mengine mtaalamu huyo wa mimea na udongo anaeleza kuwa tokea waanze kutoa elimu hiyo bure, asilimia 60 ya wakulima wilayani hapa, waliopata mafunzo hayo wamekwisha anza kutumia dawa hizo za viuatilifu na mbolea asilia.


Kutokana na hilo ubora wa uonjaji wa kikombe cha kahawa wilayani Mbinga, umeongezeka kutoka asilimia 83 hadi 86 katika msimu wa kilimo wa mwaka jana ambapo wakulima zaidi ya 253 kutoka vikundi vya Unango, Bagamoyo, Jitahidi, Lumeme na Jikwamue wilayani hapa wamefikiwa na elimu hiyo.

 
Anaeleza kuwa lengo kuu ni kuwajengea uwezo wakulima hao kuzalisha kahawa iliyo bora na ambayo itapata soko zuri katika masoko ya kimataifa.

Akizungumzia mikakati mbalimbali iliyojiwekea Sustainable Harvest anasema, ni pamoja na juhudi za kuimarisha mahusiano na masoko ya kahawa na kwamba mambo muhimu ya kutekeleza ili kufikia azma hiyo, ni kuendelea kuinua ubora wa kahawa na kuwawezesha wakulima kupata bei nzuri.
     
“Utunzaji wa mazingira katika maeneo ya kuandalia kahawa ni muhimu na kwamba elimu imekuwa ikitolewa kuhusiana na hilo sambamba na kushindanisha vikundi”, anasema Kaminyoge.

Vilevile anaongeza kuwa wakulima wa kahawa wanaelimishwa juu ya kudhibiti mmomonyoko wa udongo katika mashamba yao, kwa kutengeneza makinga maji ili kuzuia hali hiyo isiweze kutokea hasa kipindi cha masika, ambacho kinakuwa na mvua nyingi.
     
Anasema wakati umefika kwa mkulima anayezalisha kahawa wilayani Mbinga, kupunguza matumizi ya mbolea na madawa ya kutoka viwandani badala yake waendeleze mazoea ya kutumia viuatilifu asilia na mbolea za asili, ili kuweza kupata kahawa yenye muonjo na bei nzuri katika masoko ya kuuzia zao hilo.

Binafsi ninachoweza kusema hapa ni kwamba, ustawi wa maendeleo mahali popote pale hutokana na mipango iliyowekwa na wasimamizi husika, ili kufikia malengo hasa kwa kushirikisha watendaji kutoka sekta binafsi na serikali ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa wakati.

Asilimia 80 ya wananchi hapa Tanzania wanategemea kilimo ambacho kwa muda mrefu, hakina tofauti na kile cha zamani ambacho hakikuwa na tija yoyote na hili lilitokana na ukosefu wa wataalamu wa kilimo cha kisasa, ambacho kingeweza kuwafanya wapige hatua mbalimbali za kimaendeleo katika nyanja hii ya kilimo.


Hivyo basi yatupasa kujenga ushirikiano wa dhati, ili tuweze kufikia malengo tuliyojiwekea na kumfanya mkulima huyu aweze kunufaika na kuendeleza maisha yake kwa kupiga hatua mbalimbali za kimaendeleo.

Sote tunafahamu kuwa zao la kahawa limekuwa likiingizia fedha nyingi za kigeni serikali yetu, hivyo inatulazimu kutekeleza majukumu yetu ipasavyo ili kumwezesha mkulima huyu mwenye kipato duni, aweze kuendelea na kujikomboa kiuchumi.

Leo hii tukifanya mzaha na kupuuzia haya ninayosema, la hasha wilaya ya Mbinga haitaweza kuendelea kupiga hatua mbele za kimaendeleo, kama zao la kahawa halitaendelezwa kwa misingi inayotakiwa.





No comments: