Wednesday, April 3, 2013

KITUO CHA KULELEA WATOTO YATIMA TUNDURU, WAOMBA MSAADA



Na Steven Augustino,

Tunduru.

HALMASHAURI ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, imeahidi kutoa msaada wa shilingi milioni 2.8 katika kituo cha kulelea watoto yatima, kinachomilikiwa na Kanisa la Bibilia kijiji cha Mbesa  wilayani humo ikiwa ni juhudi yake ya kujali watoto hao.

Ahadi hiyo ilitolewa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Robert Nehatta wakati akizungumza kwenye  maadhimisho ya Wanawake wa kikristo yaliyofanyika mwishoni mwa wiki mjini hapa.

Tayari fedha hizo zimekwisha pewa Baraka na Baraza la madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo na kupitishwa katika bajeti ya mwaka 2013/2014.

Nehatta ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alilazimika kutoa kauli hiyo kufuatia maombi yaliyotolewa na Umoja wa wanawake wa Kikristo wilayani Tunduru, ambao pamoja na mambo mengine walibainisha kuwa hivi sasa kituo hicho kinalea watoto wachanga ambao hufiwa na mama zao wakati wa kujifungua, kwamba kipo katika hali mbaya kiasi cha kutishia kufungwa baada ya wafadhili kutoka Ujerumani kusitisha kutoa misaada.

Kufuatia kauli hiyo pia waumini waliohudhulia katika ibada hiyo wakajikamua kwa hali na mali kupitia mfumo wa changizo la papo kwa papo na kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi 210,000 ili kuwasaidia watoto hao.

Awali akisoma taarifa ya hali mbaya inayoikabili kituo hicho katibu wa kikundi hicho Sara Samatta alimweleza mgeni huyo kuwa hayo yalibainika wakati umoja huo, ulipokitembelea kituo hicho mwanzoni mwa mwaka huu ambapo pamoja na mambo mengine walibaini kupungua kwa kasi ya kupokea watoto hao kutokana na hali mbaya inayowakabili, ambapo kwa sasa kinapokea idadi ya watoto 30 tu kati ya 60 waliokuwa wakipokelewa awali tangu kituo hicho kianzishwe mwaka 1960.

Alisema katika ziara hiyo ambayo wanakikundi hao walitoa msaada wa vitu mbalimbali vyenyethamani ya shilingi 230,000 zilizotokana na michango ya waumini wa makanisa ya kikristo wilayani Tunduru, pia walibaini kuwepo kwa mahitaji makubwa ya msaada katika kituo hicho cha kulelea watoto yatima.

Kupitia maombi hayo pia umoja wa wanawake hao ulitumia nafasi hiyo kuwaomba watu wenye uwezo, mashirika na makundi mbalimbali kukiangalia kituo hicho kwa jicho la huruma kwa kutoa misaada ya hali na mali, ili kuwaokoa watoto hao wenye mahitaji makubwa ya mapenzi  ya wazazi katika katika kulelewa kwao.

No comments: