Saturday, July 19, 2014

RAIS KIKWETE AWATAKA WAKULIMA WA KAHAWA KUWA NA NIDHAMU YA MATUMIZI YA FEDHA

Rais Jakaya Kikwete akiangalia vikundi vya ngoma katika kituo kikuu cha Mabasi mjini Mbinga, mara baada ya kuwasili akitokea wilaya ya Nyasa. Upande wa kulia ni Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga.

 Rais Jakaya Kikwete upande wa kulia akisalimiana na Askofu wa Jimbo la Mbinga, John Ndimbo mara baada ya kuwasili katika wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma katika siku ya tatu ya ziara yake mkoani humo. (Picha zote na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,


Mbinga.  

RAIS wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete amewataka wakulima wanaozalisha zao la kahawa wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kutumia fedha walizokopeshwa na shirika la hifadhi ya jamii (NSSF) kwa makusudio yaliyowekwa na sio vinginevyo.

Kikwete alisema hayo baada ya kukabidhi hundi ya shilingi bilioni 2 kwa vyama vinne vya ushirika ambavyo hujishughulisha na uzalishaji wa zao hilo wilayani humo, ambavyo kila kimoja vimekopeshwa shilingi milioni 500.

Aliwataka viongozi na wanachama wa ushirika husika, kuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha hizo ili waweze kurejesha kwa wakati na wanachama waweze kunufaika na mkopo huo.


Awali akisoma taarifa ya NSSF juu ya mpango wa kuwafikia wakulima wote wa wilaya hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa shirika hilo Chiku Matessa alisema wazo la kuanzisha mpango huo ni msukumo uliotokana na changamoto wanazokabiliana nazo wakulima katika kuendeleza kilimo kutoka na kukosa fedha.

Matessa alieleza kwamba baada ya kuona hilo, shirika liliona ni vyema lianze kutoa mikopo kwa wakulima wadogo wadogo yenye gharama nafuu ili waweze kuondokana na  adha hiyo wanayoipata sasa, hatimaye waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na lindi la umasikini.

Alisema changamoto hizo ni pamoja na kukosa uhakika wa huduma za afya, kutokuwa na uwezo wa kununua pembejeo ili kuongeza uzalishaji na uhakika wa kipato baada ya kufikia umri wa uzee ambapo husababisha kushindwa kuendelea na shughuli za kilimo.

Mkurugenzi huyo alivitaja vyama vinne vya ushirika wilayani Mbinga ambavyo vilipatiwa mkopo huo ni Mahilo, Ngaka, Ngima na Pilikano.

Hata hivyo alisema shirika linatoa wito kwa wakulima wote wa wilaya hiyo ambao hawajajiunga na vyama vya ushirika wajiunge, na NSSF ili waweze kunufaika na mafao ikiwemo hata na mikopo yenye riba nafuu.


No comments: