Saturday, July 5, 2014

TAKUKURU YALIA NA VITENDO VYA RUSHWA KATIKA MIRADI YA MAENDELEO

Aliyevaa traki suti yenye rangi ya bluu, ni Kamanda wa TAKUKURU wilaya ya Mbinga Ditram Mhoma, akiteta jambo na watu ambao walikuwa wakiwasili katika banda la taasisi hiyo kwenye mkesha wa Mwenge wa Uhuru kata ya Maguu wilayani humo, kwa ajili ya kupata elimu namna ya kupambana na vitendo vya rushwa.

Baadhi ya wadau wa kupambana na rushwa wakiwa ndani ya banda la TAKUKURU katika mkesha wa Mwenge wa Uhuru kata ya Maguu wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakipewa elimu na mmoja kati ya makamanda wa takukuru wa wilaya hiyo aliyekuwa upande wa kulia, namna ya kupambana na vitendo vya rushwa. (Picha na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

TAASISI ya Kuzuia, Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma imesema, wilaya hiyo inakabiliwa kwa kiasi kikubwa na vitendo vya rushwa katika miradi ya maendeleo ya wananchi ikiwemo ujenzi wa majengo ya shule, barabara na miradi mbalimbali ya kilimo.

Aidha rushwa kubwa imetawala hasa kwenye kitengo cha manunuzi, ambapo jitihada zinaendelea kufanyika kuchunguza matatizo husika yaliyopo na tayari baadhi ya vigogo wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga wamefikishwa Mahakamani kujibu makosa yanayowakabili.

Hayo yalisemwa jana na Kamanda wa TAKUKURU wa wilaya hiyo Ditram Mhoma alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari, ambao walitembelea banda la taasisi hiyo la kuelimisha jamii namna ya kupambana na rushwa, katika uwanja wa mkesha wa mbio za mwenge wa Uhuru kata ya Maguu wilayani humo.


Mhoma alifafanua kuwa viongozi sita wamefikishwa katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga, wakikabiliwa na tuhuma za matumizi mabaya ya fedha za miradi ikiwemo ujenzi wa barabara na majengo ya kutolea huduma za afya.

Alibainisha kuwa kuna baadhi ya miradi ambayo iligharimu fedha nyingi imejengwa chini ya kiwango na kusababisha kufikia hatua ya kubomoka.

Pamoja na mambo mengine alisema changamoto kubwa wanayokabiliana nayo katika kuendesha kesi mahakamani, ni ushirikiano mdogo unaotolewa kutoka kwa wananchi ambapo wengi wao wamekuwa hawataki kwenda kutoa ushahidi.

“Wakati tunapofanya uchunguzi wananchi wamekuwa wakitupatia ushirikiano wa kutosha, lakini tunapofikia hatua ya kuendesha kesi mahakamani hawataki kuja kutoa ushahidi, hii ndiyo changamoto kubwa tunayokabiliana nayo na kuonekana kesi nyingi zinaishia mahakamani kwa watuhumiwa kutopatikana na makosa hatimaye huachiwa huru bila kuchukuliwa hatua”, alisema.

Hata hivyo Mhoma aliiomba jamii kwa ujumla ishiriki kikamilifu dhidi ya mapambano ya rushwa kwenye maeneo yao, hasa katika kutoa ushahidi mahakamani pale wanapotakiwa ikiwemo pia wakemee vitendo hivyo hasa kwenye maeneo yao ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya wananchi.


No comments: