Wednesday, June 12, 2013

KATIBU WA CWT MBINGA AONJA JOTO YA JIWE, ANUSURIKA KUANGUSHIWA KIPIGO

Katibu wa chama cha walimu Tanzania (CWT) wilayani Mbinga Samwel Mhaiki akijibu tuhuma mbalimbali zinazomkabili ikiwemo matumizi mabaya ya ofisi na kuwachonganisha walimu na Serikali kwa kuandika barua zisizopata baraka kutoka kwa wanachama na kutowashirikisha viongozi wenzake ambapo alinusurika kipigo kutoka kwa walimu.


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KATIBU wa Chama cha walimu Tanzania (CWT) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma Samwel Mhaiki amenusurika kipigo kutoka kwa wanachama wa chama hicho, katika kikao na waratibu elimu kata wakimtuhumu kukitumia chama hicho kwa maslahi yake binafsi na kutotekeleza majukumu yake ipasavyo.

Kadhalika wanachama hao walidai kwamba amekuwa akiwachonganisha walimu pamoja na viongozi wa serikali wilayani humo.

Wakizungumza  huku wakiwa na  jazba na wengine kutoa lugha chafu kwa  Katibu huyo katika kikao kilichowakutanisha waratibu elimu kutoka kata zote za mbinga na nyasa, pia wamemtaka kuachia nafasi yake wakidai kuwa ameshindwa kuwasaidia katika kazi za utumishi wa umma.


Walisema badala yake amekuwa mmoja wa watu wanaotumika vibaya na baadhi ya viongozi wanaotaka kumuondoa afisa elimu ya msingi Mathias Mkali,  ambaye anaonekana ni mwiba kwa baadhi ya vigogo wa halmashauri ya Mbinga wanaotajwa kuhusika na matumizi mabaya ya fedha za malipo mbalimbali ya walimu.

Aidha Katibu huyo anadaiwa kuandika barua na kuzisambaza katika shule zote za Mbinga kuzuia mpango wa masomo ya ziada(makambi) hadi  serikali itakapowalipa madai yote wanayodai, pamoja na posho za kufundisha masomo hayo wakati wa likizo bila ya kupata ushauri kutoka kwa wanachama ambao ni walimu na hata kwa viongozi wenzake akiwemo mwenyekiti wake wa CWT.

Mwalimu Edmund Hyera wa shule ya msingi Juhudi kutoka kata ya Kigonsera alieleza kuwa, barua aliyoiandika  inaonesha bado anaendelea na uchochezi kati ya serikali na walimu jambo  ambalo lilishakwisha tangu mwaka jana kufuatia ahadi mbalimbali za viongozi akiwemo Rais Jakaya Kikwete, aliyehaidi kuyafanyia kazi madai yote ya walimu.

 Alisema Mhaiki amekuwa mstari wa mbele kutetea malsahi yake binafsi na sio ya walimu, ndiyo maana amefikia hatua hata ya kuwachonganisha na mwajiri wao jambo linaloweza kuirudisha nyuma wilaya yao kitaaluma, kwani muda mwingi viongozi wa serikali akiwemo afisa elimu ya msingi hutumia muda mwingi wa maendeleo kutafuta suluhu ya matatizo yaliyokuwepo jambo linaloashiria kutokuwepo kwa ushirikiano wa kutosha.

Aliongeza kuwa barua ya kuzuia makambi kwa vijana wanaojiandaa kufanya mitihani  yao ya kumaliza elimu ya msingi  miezi miwili ijayo, inaonesha jinsi gani Katibu huyo alivyokuwa adui namba moja wa elimu ya msingi Mbinga.

“Huyu katibu sio mtu mwema kwetu sisi walimu amekuwa msaliti mkubwa kwetu ona yeye badala ya kushughulikia matatizo yetu anajiingiza katika mambo yasiyomuhusu, ambayo ni sumu mbaya kwa maendeleo ya elimu hapa mbinga”, alisema Hyera.
   
Pia alisema hadi sasa walimu wamechoshwa na migogoro ya mara kwa mara inayosababisha kuwavunja moyo wa kazi  ambayo imedumu kwa muda mrefu sasa.  

Wanachama hao wamefika mbali zaidi na kutishia kutaka kujitoa uanachama  katika chama hicho na kuanza kufikiria kujiunga na chama cha walimu cha Msumbiji ambako ni jirani zaidi ikilinganishwa na Mbinga huku wengine zaidi ya walimu 40 kutoka kata ya Liparamba wamekwisha andika barua za kujitoa uanachama wa CWT wilayani Mbinga.

Hata hivyo Mratibu elimu kata ya Lipingo Alfred Chikoola amewataka viongozi wa chama hicho wilayani humo, kuacha unafiki na kujiingiza katika migogoro ambayo haina manufaa katika jamii  badala yake wawe wanaunga mkono maendeleo ya elimu wilayani hapa kwa kujenga ushirikiano endelevu.

No comments: