Saturday, June 15, 2013

UCHAMBUZI: MGOGORO WA ELIMU MBINGA UTAENDELEA HADI LINI ?

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Nyoni kata ya Nyoni, Adolph Komba akifundisha wanafunzi wa darasa la saba wanaosoma katika shule hiyo wakati huu wa likizo ambao wapo katika kambi, alisema kuwa lengo la walimu hao kufundisha wakati huu wa likizo ni kuongeza kiwango cha ufaulu na maendeleo ya elimu ya msingi wilayani Mbinga.(Picha na Kassian Nyandindi)



 Na Kassian Nyandindi,

WAHENGA siku zote husema elimu ndio ufunguo wa maisha, na hakuna sehemu ambayo inaweza ikawa na maendeleo pasipo kuwa na elimu.

Katika hili hatuna budi viongozi tukawa na mipangilio mizuri ya kukuza sekta ya elimu katika maeneo yetu tunayofanyia kazi, kwa kujenga ushirikiano na kubuni njia mbadala za kukuza taaluma mashuleni.

Ni aibu kuona viongozi siku zote tumekuwa tukilumbana na kujenga migogoro ambayo inarudisha nyuma sekta hiyo muhimu, ambayo ndio msingi wa maendeleo katika jamii.

Katika makala haya napenda kuelezea mgogoro wa idara ya elimu shule za msingi, ambao umekuwa ukiendelea wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, na kusababisha baadhi ya vigogo kulumbana pasipo kuwa na sababu zozote za msingi.


Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wetu umebaini kuwa vigogo wachache wilayani humo, wameanzisha mgogoro huu kwa maslahi yao binafsi ambayo hayana tija katika jamii.

Hivyo basi, kutokana na kushamiri kwa upuuzi huo kunasababisha kuwavunja moyo baadhi ya watendaji wa idara ya elimu msingi wilayani hapa, ambao wanaonekana kujituma katika kufanya kazi zao kwa umakini.

Upuuzi huo ni ule wa kuandikiana barua za kuchafuana ambazo imefikia hatua zinaleta mtafaruku ambao naweza kusema, tusipokuwa makini taifa la Wanambinga tutalifikisha pabaya.

Nashauri ni vyema sasa tukaacha mambo haya tubakie katika mstari wa kuendeleza sekta hii muhimu, na sio kuishia wakati wote kulumbana na kujengeana bifu ambazo hazina mantiki yoyote ile.

Nimebaini pia ugonvi huu wakuandikiana mabarua ya kuchafuana yanatokana na kigogo mmoja(Jina tunalo) hapa wilayani, kuendekeza tabia ya kukataa watumishi wanaohamishiwa hapa na kutaka apange safu yake anayoitaka yeye, ili aweze kufuja vizuri fedha za idara hiyo ya elimu.

Ndugu zangu hili halingii akilini, haya mambo yamepitwa na wakati kinachotakiwa sasa ni kukaa pamoja na kufanya kazi kama timu, vinginevyo tusipozingatia hili mwisho wa siku elimu hapa wilayani itaendelea kudorola na kufikia mahali pabaya.

Kama tutafikia hapo taifa hili la kizazi cha sasa na kijacho, halitatuelewa badala yake litatuadhibu kwa kutupiga viboko kutokana na dhambi hii tunayoifanya sasa.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, kilio cha Wanambinga wanakutaka udhibiti tatizo hili lisiweze kuendelea, maana wewe ndio mhimili mkuu wa maendeleo hapa wilayani.

Wanambinga wanasema viongozi wanaofanya vurugu hizo za kutaka kurudisha nyuma maendeleo ya elimu unawafahamu na wapo katika mafaili yako mezani, hivyo wanakuomba usiwafumbie macho wachukulie hatua ikiwezekana hata kuwahamisha waondoke hapa Mbinga.

Pia wanasema wamechoshwa na tabia hii, na endapo wataona inaendelea wapo tayari kuandamana hadi ofisini kwako, wakipinga vitendo hivyo ambavyo vinarudisha nyuma maendeleo katika sekta ya elimu.

Nionavyo, leo wilaya ya Mbinga maendeleo ya elimu ya msingi yanaanza kuonekana kung’ara, sasa najihoji mwenyewe ni mdudu gani ambaye anataka kuturudisha nyuma tulikotoka, ambako kulikuwa kubaya kiasi ambacho ilikuwa ni aibu tupu?

Leo walimu huko vijijini wilayani Mbinga, nimeshuhudia jinsi gani wanavyojituma wakati huu walikizo kufundisha watoto wanaotarajia kumaliza darasa la saba, wanapaswa kupongezwa katika hili.

Vituo vya kufundishia vimewekwa kwa kila kata, watoto wanasoma vizuri bila matatizo yoyote yale, wazazi wanashiriki vyema katika kutoa michango yao ili ufanisi mzuri uweze kuwepo.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, natambua kilio chetu umekisikia na utakifanyia kazi hivyo tunachotarajia sasa ni kuona matunda mema na mgogoro huu hatutaki kuuona ukiendelea, yule ambaye utambaini anaendekeza mambo haya ni vyema awajibishwe kwa namna moja au nyingine, ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Mungu ibariki Mbinga, Ruvuma na Tanzania kwa ujumla,

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa simu namba 0762578960.

No comments: