Saturday, January 2, 2016

ELIAS MWALEWELA AKAMATWA AKISAFIRISHA KAHAWA KWA NJIA YA MAGENDO



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MFANYABIASHARA mmoja ambaye anajulikana kwa jina la Elias Mwalewela (46) anayeishi mtaa wa Manzese Mbinga mjini mkoani Ruvuma, amekamatwa akitorosha kahawa ya maganda isiyokobolewa kiwandani, kwenda Jijini Mbeya kwa njia ya magendo bila kufuata taratibu na sheria husika.  

Aidha imeelezwa kuwa wakati zao hilo analitorosha, alikuwa akitokea wilayani Mbinga mkoani humo kwa lengo la kuipeleka huko, huku akijua fika kahawa ya maganda hairuhusiwi kusafirishwa kutoka wilaya moja kwenda nyingine.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Venance Mwamengo alisema kuwa baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema juu ya utoroshaji huo, alichukua jukumu la kufuatilia suala hilo ndipo baadaye alifanikiwa kumkamata katika kijiji cha Liganga wilaya ya Songea vijijini mkoani hapa kwa kushirikiana na askari aliokuwa nao.

Alifafanua kuwa alimkamata Disemba 30 mwaka jana, majira ya saa tano usiku akiwa na gari aina ya Fuso lenye namba za usajili T 818 ADH ambalo lilikuwa likiendeshwa na Geati Mwajungwa mkazi wa Lujewa wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya.  


“Huyu mfanyabiashara na dereva wake, baada ya kuwakamata niliwafikisha kituo kikuu cha Polisi wilaya ya Mbinga na gari lenye mzigo wa kahawa tani nne ambalo linashikiliwa hapo kituoni, hivi sasa wanaendelea kuhojiwa na taratibu zingine zitafuata ikiwemo kufikishwa Mahakamani au wanapaswa kulipa faini ya shilingi milioni 20”, alisema Mwamengo.

Mwamengo aliongeza kuwa watoroshaji hao walipofika mpakani mwa wilaya yake ambako kuna geti la ukaguzi wa mazao, walitorosha gari hilo likiwa na kahawa hiyo ndipo jitihada zilifanyika za kuwasaka na kufanikiwa kuwakamata katika kijiji hicho cha Liganga.

Alieleza kuwa wakati anawakamata, aliwakuta wakiwa na kibali cha usafirishaji kahawa safi (Clean Coffee) ambacho ni cha kampuni ya Tutunze Kahawa Limited, iliyopo wilayani humo ambayo inajishughulisha pia na ununuzi wa zao hilo.

Vilevile aliongeza kuwa kwa mujibu wa taratibu husika, kibali hicho kinaruhusu kusafirishia kahawa iliyo safi tu, ambayo imekwisha kobolewa kiwandani na sio ya maganda kama walivyofanya watu hao.
 
Kufuatia tukio hilo Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga naye alithibitisha juu ya tukio hilo na kueleza kuwa mfanyabiashara huyo na dereva wa gari hilo wanahojiwa na Jeshi la Polisi wilayani humo, ili waweze kutolea maelezo ya kina juu ya kitendo hicho walichokifanya.

“Ni kweli taarifa nilizonazo wamekamatwa wakisafirisha kahawa ya maganda (Mbuni) na wapo Polisi wanahojiwa, wakimaliza kuhojiwa nitakuwa na taarifa kamili na kulitolea ufafanuzi mzuri jambo hili hapo baadaye”, alisema Ngaga.

Hata hivyo Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela alipoulizwa kwa njia ya simu juu ya tukio hilo alisema hataweza kutoa ufafanuzi wowote kuhusiana na jambo hilo, akidai kwamba ofisi yake bado halijamfikia.

No comments: