Friday, January 8, 2016

MAJALIWA AMSIMAMISHA KAZI KIGOGO KIWANDA CHA KUSINDIKA TUMBAKU SONGEA


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa, amemsimamisha kazi Meneja Shughuli wa Kiwanda cha kusindika tumbaku mkoani Ruvuma (SONTOP) Paul Balegwa, na kuvunja bodi ya kiwanda hicho, akidaiwa kushiriki kwa namna moja au nyingine kufanya ubadhirifu wa fedha za wakulima wanaozalisha zao hilo na kusababisha kiwanda hicho, kusitisha uzalishaji kwa zaidi ya miaka 18 iliyopita.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa mikutano wa Ikulu ndogo ya Songea, Waziri Mkuu Majaliwa alisema kuwa amefikia uamuzi wa kumsimamisha kazi Meneja huyo kutokana na ubabaishaji mkubwa wa uendeshaji wa kiwanda hicho ambao ulikuwa ukifanywa kwa kushirikiana na mhasibu wake Nurdin Ponela, ambaye sasa inadaiwa amekimbia na kutokomea kusikojulikana.

Vilevile Waziri Mkuu huyo alifafanua kuwa wakulima wa zao la tumbaku kwa muda mrefu wamekuwa wakiulalamikia uongozi wa kiwanda hicho kwamba, viongozi wao kuwa ni wababaishaji huwakata fedha zao za mauzo ya tumbaku bila kufuata utaratibu.


“Katika kiwanda hiki upo ubabaishaji mkubwa, wa uendeshaji wa hata chama kikuu cha ushirika cha wakulima wa zao hili wilaya ya Songea na Namtumbo (SONAMCU) kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa matumizi ya fedha na leo hii natamka kwamba nimemsisha kazi Paul Balegwa na sheria zitafuata mkondo wake”, alisema Waziri MKuu Majaliwa.

Kiwanda hicho ambacho kwa hivi sasa kimegeuzwa kuwa ghala la kuhifadhia bidhaa mbalimbali za wafanyabiashara, hali hiyo ilimchukiza Waziri Mkuu Majaliwa alipotembelea kwa kushitukiza na kujionea madudu hayo.

Kadhalika katika eneo la nje ya kiwanda hicho, imegeuzwa kuwa sehemu ya kuegeshea magari yanayobeba makaa ya mawe kutoka mgodi wa Ngaka ambayo yanachimbwa katika kata ya Ruanda wilaya ya Mbinga mkoani humo.

Pamoja na mambo mengine, Waziri Mkuu Majaliwa alimuagiza Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu akae na wataalamu wake akiwemo Afisa biashara na uwekezaji wa Wizara ya viwanda na biashara Tanzania, Stella Lugongo kwamba asiondoke mpaka watafute njia mbadala ya kuwatafuta wawekezaji ambao wataweza kufufua kiwanda hicho, ambacho kilikuwa ni tegemeo kubwa kwa wakulima wanaozalisha zao hilo mkoani humo.

Alisema kuwa ufufuaji wa kiwanda cha SONTOP utasaidia kuongeza ajira kwa vijana zaidi ya 2,500 kama ilivyokuwa hapo awali, na kwamba kikisha anza kufanya kazi itasaida pia kuongeza thamani ya zao la tumbaku na kukuza uchumi wa mkoa huo na taifa kwa ujumla.

Mapema Waziri Mkuu Majaliwa kufuatia kuwepo kwa tuhuma hizo, alilazimika kumuagiza Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Mwambungu ahakikishe kwamba kabla hajamaliza ziara yake anahitaji kukutana na viongozi wa vyama vya msingi pamoja na bodi ya kiwanda hicho ili aweze kupata taarifa kamili juu ya hali hiyo ambayo ilisababisha kiwanda hicho kusimama.

Kwa nyakati tofauti baadhi ya wakulima pamoja na waliokuwa wafanyakazi wa kiwanda hicho ambao hawakutaka majina yao yatajwe wameeleza kuwa kiwanda cha kusindika tumbaku cha SONTOP kilichopo katika Manispaa ya Songea, kilisimama kusindika zao hilo kufuatia kuingiwa kwa mikataba mibovu kwa baadhi ya viongozi iliyoambatana na ubadhirifu wa fedha ambao ulisababisha kiwanda kishindwe kujiendesha.

Walisema kuwa katika mikataba hiyo, ina makampuni yanayonunua zao hilo, iliweka masharti ya kusindika tumbaku kwa kutumia viwanda vilivyoko mkoani Morogoro jambo ambalo lilisababisha kupoteza ajira za vijana wengi waliokuwa wakifanya kazi.

Hata hivyo Waziri Mkuu Majaliwa amemaliza ziara yake ya siku tatu mkoani Ruvuma, na kuondoka kurejea Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kutekeleza majukumu mengine ya kazi za kitaifa.

No comments: