Friday, January 8, 2016

SERIKALI KUWEKA MPANGO WA MATUMIZI YA TREKTA KWA WAKULIMA



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

SERIKALI hapa nchini imesema kuwa, itaweka mpango mzuri wa kuhakikisha kwamba kila mwananchi katika maeneo anayozalisha kilimo cha mazao ya chakula na biashara, anahamasishwa alime mazao yake shambani kwa kutumia matrekta na kuachana na jembe la mkono ili mazao hayo waweze kuzalisha kwa wingi.

Aidha imeelezwa kuwa mpango huo unaweza kuwafikia wakulima hao kwa urahisi, endapo viongozi waliopo madarakani katika ngazi za halmashauri ya wilaya hadi mkoa, wataweza kuweka mikakati madhubuti katika bajeti zao kwa kuhakikisha kwamba wakulima wanapewa matrekta hayo ya kulimia kwa gharama nafuu.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Majaliwa Kassim Majaliwa alisema hayo hivi karibuni mjini Songea akiwa katika ziara yake ya siku tatu mkoani humo, akiwajibika kupita katika maeneo mbalimbali kuona hali halisi ya maendeleo na kuweka msisitizo wa namna ya utendaji kazi.

“Tutatumia mkoa wenu wa Ruvuma kama mfano ndani ya nchi, kupitia kilimo mmeweza kuwa watano kitaifa katika kukuza pato la mwananchi mmoja mmoja, hivyo basi nasisitiza maeneo yote ya mabondeni, tuwahamasishe pia wananchi waendeshe kilimo cha umwagiliaji, kuna kila sababu kwenye eneo hili tuhakikishe tunajikita zaidi”, alisisitiza Waziri Mkuu Majaliwa.

Pia alieleza kuwa kutokana na wananchi wa mkoa huo kuonekana wengi wao wana kipato kizuri, hivyo wanapaswa kuwa na matumizi mazuri ya fedha ili waweze kujiletea maendeleo kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.


Licha ya kujishughulisha na kilimo, pia ameuagiza uongozi wa mkoa huo kupitia viongozi husika wa halmashauri uelekeze wananchi katika suala la ufugaji nyuki ili nalo liweze kuwaingizia mapato makubwa.

Waziri Mkuu huyo amewaagiza pia Wakurugenzi wa Halmashauri hapa nchini, kupima mashamba ya wakulima wa kawaida ili waweze kupata hati miliki na hatimaye mwananchi aweze kukopesheka na taasisi za kifedha kwa lengo la kusukuma maendeleo yake mbele.

“Naagiza mkae kwenye halmashauri zenu na kutekeleza jambo hili haraka, tuache tabia ya kuazima wapimaji ardhi kutoka maeneo mengine vifaa vya kupimia iwe agenda muhimu katika bajeti zenu ni wajibu kuwa navyo, ili viweze kuturahisishia utekelezaji wa jambo hili”, alisema.

Awali akisoma taarifa ya maendeleo ya mkoa wa Ruvuma, Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu alisema kuwa mkoa wake kwa mwaka unazalisha tani 689,123 za mazao ya chakula na hilo linatokana na kuimarika kwa matumizi ya pembejeo, zana za kilimo na matumizi bora ya ugani.

Sekta ya elimu:

Kadhalika Waziri Mkuu Majaliwa, alipozungumzia juu ya sekta ya elimu Wakuu wilaya mkoani humo amewataka kuchukua hatua madhubuti, juu ya kumaliza tatizo la uhaba wa madawati ya kukalia wanafunzi darasani kwa kutumia rasilimali za misitu waliyonayo katika maeneo yao, ili kuwaondolea adha watoto hao ya kukaa chini.

Alisema lazima wafanye uhakiki wa matengenezo ya madawati hayo kwa shule zote za msingi na sekondari, ili tatizo hilo katika kipindi cha mwaka huu liweze kwisha na serikali haitarajii kusikia tena mkoa huo, unakuwa na mapungufu ya madawati ya kukalia watoto shuleni.

Alisema kuwa wakuu wa wilaya, wakae na Wakurugenzi wao katika halmashauri kupitia vikao husika na kuona namna gani wanatumia sheria za uvunaji misitu iliyopo katika maeneo yao, ili waweze kupata mbao za kutengenezea madawati hayo.

Vilevile alisisitiza kwamba kila mtoto mwenye umri wa miaka minne hadi mitano, wahakikishe wanaandikishwa na kupelekwa shule kwa ajili ya kuanza chekechea na kila ilipo shule ya msingi, wahakikishe panakuwa na darasa la chekechea ili kuweza kumsaidia mwananchi wa kawaida aweze kupeleka mtoto wake shule.

Aliongeza kuwa zoezi hilo liendane sambamba na ujenzi wa nyumba za walimu na huku akisisitiza shule za msingi hadi sekondari, serikali imefuta ada na baadhi ya mlundikano wa michango ambapo fedha zote za kuendeshea shule hizo, serikali itapeleka moja kwa moja katika shule husika na tayari akaunti za shule zote hapa nchini, zimekwisha chukuliwa kwa ajili ya utekelezaji wa zoezi hilo.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma:

Said Mwambungu ambaye ni Mkuu wa mkoa huo, awali akisoma taarifa ya maendeleo ya mkoa katika sekta ya elimu alisema kuwa kutokana na watoto wengi kuandikishwa kujiunga na darasa la kwanza, kuna upungufu mkubwa wa madawati ambapo mahitaji ni 120,812 yaliyopo ni 76,025 na kufanya upungufu wake kuwa ni 44,787.

Mwambungu alifafanua kwamba kumekuwa pia na upungufu wa nyumba za walimu, ambapo mkoa unahitaji nyumba za walimu wa shule za msingi 7,499 na sekondari 2,655 na zilizopo kwa shule za msingi kwa sasa ni 2,574 upungufu wake ni 4,925 kwa sekondari zilizopo sasa ni 515 pungufu yake ni 2,140.

Alieleza kuwa katika kutatua tatizo hilo, mkoa umejipanga kuhamasisha wananchi na halmashauri zake kuwa na benki ya tofari 100,000 kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa nyumba hizo.

Tatizo la mimba lipo katika shule za sekondari ambapo kwa mwaka 2014, wanafunzi 56 walishindwa kuendelea na masomo yao kutokana na kupata ujauzito, na kwa upande wa shule za msingi wanafunzi 9 walikuwa na hali hiyo katika kipindi cha mwaka jana na wote, hawakuweza kufanya mitihani yao ya mwisho kutokana na kukumbwa na hali hiyo.

No comments: