Saturday, January 16, 2016

WAZIRI WA NISHATI NA MADINI AITAKA TANESCO KUSHIRIKIANA NA ANDOYA HYDRO ELECTRIC POWER


Menas Mbunda Andoya enzi ya uhai wake, akiwa na mkewe na Waziri Mkuu Mizengo Pinda wakati wa uzinduzi wa mradi wa kuzalisha umeme vijijini, ambao ulibuniwa miaka 13 iliyopita.

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

SHIRIKA la ugavi nishati ya umeme Tanzania (TANESCO) limeagizwa kujenga ushirikiano na kampuni binafsi ya Andoya Hydro Electric Power (AHEPO) ambayo inazalisha umeme utokanao na nguvu ya maji wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, ili mradi huo uweze kuwa endelevu.

Aidha umeme huo wa maporomoko ya maji umeunganishwa katika njia kuu ya gridi ya TANESCO ambao husambazwa kwa wateja waliopo wilayani humo.

Waziri wa nishati na madini, Profesa Sospeter Muhongo alitoa agizo hilo juzi alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo.

Awali akisoma taarifa ya maendeleo ya mradi huo, Mkurugenzi wa kampuni ya AHEPO, Alex Andoya alimweleza Waziri Muhongo kuwa madhumuni ya kuzalisha umeme katika mradi huo ni Megawati 1 na umeunganishwa kwa wateja wa awali 922 kati ya 3,835 katika vijiji vya Lifakara, Kilimani na Mbangamao wilayani Mbinga na ziada huuzwa katika shirika hilo la ugavi wa umeme ukilenga kupata umeme kwa njia endelevu na bei nafuu.


“Hivi sasa tayari ujenzi wa njia kuu za kusafirisha umeme kutoka Mbinga mjini, hadi kituo kikuu cha uzalishaji na usambazaji katika vijiji hivyo umekwisha kamilika”, alisema Andoya.

Alifafanua kuwa mwaka 2005 kampuni hiyo ya Andoya Hydro Electric Power ilisajiliwa na upembuzi yakinifu wa mradi ulikamilika, hatimaye taarifa na mchanganuo wa mradi ulipitiwa na wataalamu mbalimbali wa taasisi za serikali ikiwamo Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Shirika la Umeme Tanzania TANESCO, NEMC, EWURA na wataalamu kutoka benki ya dunia nao wote waliafiki kuwa kiasi cha Megawati 1 kinaweza kupatikana katika maporomoko hayo yaliyopo katika mto Mtandasi.

Kufikia Novemba 2012 mradi ulifanikiwa kupata kibali na fedha za kutekeleza, ukiwa katika hatua mbalimbali ikiwemo ujenzi wa njia ya usafirishaji wa umeme yenye urefu wa kilometa 14 kwa kiwango cha HT kutoka kituo cha umeme cha Mbangamao hadi makao makuu ya wilaya ya Mbinga, na sasa umeunganishwa na gridi ya TANESCO wilayani humo, pamoja na vijiji vya Lifakara, Kilimani na Mbangamao.

Andoya alieleza kuwa awamu ya pili ilikuwa ni ujenzi wa njia za kusambaza nishati hiyo muhimu kwa wateja, ambapo gharama za ujenzi wa mradi huo umegharimu shilingi bilioni 4.5 na kwamba asilimia 30 zilichangwa kutoka mtaji wa kampuni hiyo ya AHEPO, asilimia 70 ni mkopo kutoka benki ya CRDB na mkopo wa benki ya dunia kupitia serikali na taasisi zake ikiwamo (REA) chini ya mpango wa Tanzania Energy Development and Access Project (TEDAP) ambapo pia UNIDO nao walichangia dola 250,000 za Marekani.

No comments: